Muhtasari wa Utunzaji wa Baada ya Kujifungua

(Utunzaji Baada ya Ujauzito na Kuzaa)

NaJulie S. Moldenhauer, MD, Children's Hospital of Philadelphia
Imekaguliwa naOluwatosin Goje, MD, MSCR, Cleveland Clinic, Lerner College of Medicine of Case Western Reserve University
Imepitiwa/Imerekebishwa Aug 2024 | Imebadilishwa Feb 2025
v811318_sw

Kipindi cha wiki 6 baada ya ujauzito na kujifungua mtoto huitwa kipindi cha baada ya kujifungua, ambapo mwili wa mama hurudi katika hali yake ya kabla ya ujauzito.

Baada ya kujifungua, mwanamke anaweza kutarajia kupata mabadiliko ya kimwili na hisia nyingi tofauti, ambazo baadhi yake ni za kawaida na nyingine huenda zikahitaji matibabu. Matatizo makubwa ya kiafya ni nadra baada ya kujifungua. Madaktari, wakunga na wauguzi hujadiliana na wanawake kuhusu mabadiliko ya baada ya kujifungua na nini cha kutarajia. Kwa kawaida ziara ya ufuatiliaji na mtaalamu wa huduma ya afya hupangwa kwa wiki 6 baada ya kuzaliwa kwa mtoto (na wakati mwingine pia wiki 2 baada ya kuzaliwa kwa mtoto). Wanawake pia hupewa maagizo kuhusu wakati wa kumpigia simu daktari kuhusu dalili zinazoweza kuwa ishara ya tatizo.

Matatizo ya kawaida baada ya kujifungua ni yafuatayo:

Kutokwa na damu baada ya kujifungua kunaweza kutokea muda mfupi baada ya kujifungua lakini kunaweza kutokea hadi wiki 6 baadaye.

Hatari ya kuganda damu huongezeka kwa takriban wiki 6 baada ya kujifungua (angalia Matatizo ya Kuganda Damu Wakati wa Ujauzito). Kuganda kwa damu kwenye vena kubwa ndani ya miguu (kuganda damu ndani ya vena kubwa) inaweza kupita kwenye mapafu (kuziba kwa mishipa ya mapafu), ambayo ni hali inayohatarisha maisha.

Jedwali
Jedwali

Utunzaji Katika Siku 2 za Kwanza Baada ya Kujifungua

Kwa saa 1 hadi 4 baada ya kujifungua, mwanamke hufuatiliwa kwa karibu na daktari, mkunga au muuguzi. Ikiwa alitiwa ganzi (kama vile sindani ya kupunguza uchungu wa uzazi) au ikiwa alikuwa na matatizo yoyote wakati wa uchungu wa uzazi na kujifungua, anaweza kufuatiliwa kwa muda mrefu zaidi, kwa kawaida katika chumba cha hospitali chenye vifaa vya kutosha chenye upatikanaji wa oksijeni, viowevu vinavyowekwa kupitia sindano ya mshipa (kwa njia ya mishipa), na dawa, ikiwa inahitajika.

Wakati wa ufuatiliaji wa karibu, shinikizo la damu la mwanamke, mapigo ya moyo, na halijoto hupimwa. Kwa kawaida, ndani ya saa 24 za kwanza baada ya kujifungua, mapigo ya moyo ya mwanamke huanza kupungua kuelekea kawaida na halijoto yake inaweza kuongezeka kidogo, kwa kawaida kurudi katika hali ya kawaida katika siku chache za kwanza.

Wahudumu wa hospitali hufanya kila juhudi kupunguza maumivu na hatari ya kuvuja damu na maambukizi.

Kuvuja damu ukeni

Mara tu baada ya kujifungua, njia kuu ambayo kuvuja damu hudhibitiwa ni kupitia mikazo ya uterasi. Uterasi kwa kawaida imeundwa kwa misuli, na inapokaza misuli hubana mishipa ya damu ambayo hupunguza kasi ya kuvuja damu.

Timu ya huduma ya afya huchukua hatua za kuzuia kuvuja damu nyingi. Dawa inayoitwa oxytocin kwa kawaida huwekwa kwa njia ya mishipa au kama sindano kwenye misuli ili kuchochea mikazo ya uterasi.

Baada ya kutoka kwa kondo la nyuma (baada ya kujifungua), muuguzi anaweza kukanda tumbo la mwanamke mara kwa mara ili kusaidia uterasi kukaza na kubaki imekaza.

Ikiwa mwanamke atapoteza damu nyingi wakati na baada ya kujifungua, kipimo cha damu hufanywa ili kuchunguza upungufu wa damu.

Maumivu au uvimbe wa uke, vulva, na msamba

Eneo linalozunguka uwazi wa uke kwa kawaida huwa na maumivu, na eneo hili linaweza kuuma wakati wa kukojoa. Mipasuko kwenye msamba (eneo kati ya uke na mkundu) au urekebishaji wa episiotomia unaweza kuchangia maumivu na pia unaweza kusababisha uvimbe.

Mara tu baada ya kujifungua na kwa saa 24 za kwanza, vifurushi vya barafu au baridi vinaweza kutumika kupunguza maumivu na uvimbe. Krimu au dawa za kupuliza za kutia ganzi zinaweza kutumika kwenye ngozi ikiwa inahitajika. Kutumia chupa ya kupuliza maji ya uvuguvugu pia kunaweza kutuliza.

Wanawake wanapaswa kuwa waangalifu wanapoketi na, ikiwa kuketi kunauma, keti kwenye mto (mto wenye tundu katikati, kama donati, unaweza kusaidia).

Kukojoa

Utoaji wa mkojo mara nyingi huongezeka sana baada ya kujifungua lakini hurudi katika hali ya kawaida baada ya siku chache.

Kiwango cha hisi katika kibofu kinaweza kupungua kutokana na shinikizo kwenye kibofu kutokana na kichwa cha kijusi wakati wa kujifungua, kwa hivyo mwanamke anahimizwa ajaribu kukojoa mara kwa mara, angalau kila baada ya saa 4. Kufanya hivyo huepuka kujaza kibofu kupita kiasi na husaidia kuzuia maambukizi ya kibofu.

Wauguzi au wahudumu wengine wa matibabu wanaweza kubana tumbo la mwanamke kwa upole au kutumia kifaa kinachobebeka cha picha ya mawimbi ya sauti ili kuchunguza kibofu cha mkojo na kubaini kama kimejaa.

Mara kwa mara, ikiwa mwanamke anashindwa kukojoa peke yake, katheta lazima iingizwe kwa muda kwenye kibofu cha mkojo ili kutoa mkojo. Mara chache, katheta inayokaa ndani (katheta inayoachwa kwenye kibofu cha mkojo kwa muda) inahitajika.

Kusonga kwa tumbo

Wanawake wanahimizwa kwenda haja kubwa ndani ya siku 3 za kwanza baada ya kujifungua. Ikiwa hili halitatokea, madaktari wanaweza kupendekeza mwanamke atumie dawa za kulainisha kinyesi au dawa za kuharisha. Ikiwa ngozi au misuli inayozunguka mkundu ilichana wakati wa kujifungua, vilainishi vya kinyesi ni muhimu ili kuepuka shinikizo kwenye eneo hilo.

Kwenda haja kubwa mara ya kwanza baada ya kujifungua kunaweza kuwa vigumu, wakati mwingine huwa na kinyesi kigumu au maumivu katika eneo la mkundu au msamba. Wanawake waliojifungua kwa upasuaji au kwa sababu nyinginezo wana maumivu makali wanaweza kuagiziwa dawa za maumivu za afyuni, zinazoweza kusababisha kuvimbiwa.

Pia, kwenda haja kubwa kwa mara ya kwanza kunaweza kuchelewa kwa siku chache, wakati mwingine kwa sababu mwanamke ana wasiwasi kuhusu kuinama na kukaza mishono au kwa sababu uke au msamba unahisi uchungu au kuvimba.

Kusukuma wakati wa kujifungua au kufunga choo baada ya kujifungua kunaweza kusababisha au kuzorotesha bawasiri, ambayo inaweza kuwa chungu wakati wa kwenda haja kubwa au kwa ujumla. Maumivu yanaweza kupunguzwa kwa kuoga sitz kwa maji ya joto na/au kutumia vitia ganzi vya kupaka sehemu ya juu. Bawasiri kwa kawaida huisha ndani ya wiki 2 hadi 4.

Mlo na shughuli

Kwa kawaida, wanawake wanaweza kula na kunywa wakati wowote baada ya kujifungua, isipokuwa kama wanahisi kichefuchefu.

Wanawake wanapaswa kuamka na kutembea haraka iwezekanavyo.

Kujimiminia maji na kuoga

Baada ya kujifungua kwa njia ya uke, mwanamke anaweza kuoga kwenye bafu la manyunyu mara tu anapoweza kusimama bila kuhisi kizunguzungu.

Baada ya kujifungua kwa upasuaji, mwanamke anaweza kuoga kwenye bafu la manyunyu baada ya bendeji kuondolewa na akiweza kusimama bafuni bila kuhisi kizunguzungu. Anapaswa kuwa mwangalifu asisugue eneo la mkato. Kuoga kwenye hodhi kunapaswa kuepukwa hadi vibanio au mishono iondolewe na mkato upone kabisa, takribani wiki 6 baada ya kujifungua.

Baada ya kujifungua kwa njia ya uke au upasuaji, hakuna kitu chochote, ikiwa ni pamoja na sodo zinazotiwa ndani ya uke wala msukumo wa maji ya kupiga bomba, kinapaswa kutiwa ndani ya uke kwa angalau wiki 2. Shughuli nzito na kunyanyua mizigo mizito zinapaswa kuepukwa kwa takriban wiki 6.

Dawa

Baada ya kujifungua, wanawake mara nyingi hupata maumivu ya eneo la uke au sehemu ya upasuaji na wanaweza kutumia dawa za kutuliza maumivu kama walivyoshauriwa na daktari wao.

Kwa wanawake wanaonyonyesha, acetaminophen na ibuprofen ni dawa salama za kutuliza maumivu. Wanawake wanaohitaji kutumia dawa wakati wa kunyonyesha wanapaswa kuzungumza na daktari wao kabla ya kuitumia.

Uchanjaji

(Angalia pia Chanjo Wakati wa Ujauzito, CDC: Mwongozo ya Kuwachanja Wanawake Wajawazito, na CDC: Chanjo za COVID-19 Ukiwa Mjamzito au Unanyonyesha.)

Chanjo zinapendekezwa kwa baadhi ya wanawake baada ya kujifungua na kwa kawaida hutolewa ndani ya siku 2 za kwanza (au kabla ya kuruhusiwa kuondoka hospitalini). Mwanamke anaweza kuchanjwa ikiwa vipimo vya ujauzito vimeonyesha hana kinga dhidi ya maambukizi fulani au ikiwa anatarajia kupewa chanjo za kawaida. Baadhi ya chanjo (kwa mfano, chanjo hai au chanjo hai iliyopunguzwa nguvu) haziwezi kutolewa wakati wa ujauzito, kwa hivyo hutolewa baada ya kujifungua, ikiwa inahitajika. Chanjo nyingi, isipokuwa baadhi (kama vile chanjo ya ndui na matumizi mengi ya chanjo ya homa ya manjano), ni salama kupokea ikiwa unanyonyesha.

Wanawake hupewa chanjo ya surua-matumbwitumbwi-rubela ikiwa hawana kinga dhidi ya kirusi 1 au zaidi kati ya hivi (wakati mwingine mtu amewahi kuchanjwa hapo awali, lakini kinga haikukua).

Wanawake wajawazito ambao hawajawahi kupata tetekuwanga au kupewa chanjo ya tetekuwanga (varisela) wanapaswa kupewa dozi ya kwanza ya chanjo ya tetekuwanga baada ya kujifungua na dozi ya pili wiki 4 hadi 8 baadaye.

Kwa kawaida, chanjo ya pepopunda-dondakoo-kifaduro (Tdap) hutolewa wakati wa kila ujauzito, ikiwezekana kati ya wiki 27 na 36. Ikiwa mwanamke hajawahi kupewa chanjo ya Tdap wakati wa ujauzito huu au uliopita au akiwa kijana au mtu mzima, anapaswa kupewa chanjo hiyo ndani ya siku chache za kwanza baada ya kujifungua, iwe ananyonyesha au la. Ikiwa wanafamilia watakaoingiliana na mtoto mchanga hawajawahi kupewa chanjo ya Tdap, wanapaswa kupewa Tdap angalau wiki 2 kabla ya kuingiliana na mtoto mchanga. Chanjo ya Tdap huwapa chanjo dhidi ya ugonjwa wa pertussis (kifaduro) na hivyo kupunguza hatari ya kueneza kifaduro kwa watoto wachanga ambao hawajachanjwa.

Wanawake wanaostahiki kupata chanjo ya virusi vya papiloma vya binadamu na ambao hawajachanjwa au hawajakamilisha mfululizo wa chanjo wanaweza kuchanjwa baada ya kujifungua.

Aina ya damu ya Rh-hasi

Ikiwa mwanamke ana damu ya Rh-hasi na mtoto wake ana damu ya Rh-chanya (inayoitwa kukosa kuoana kwa Rh), mwanamke hupewa globulini ya kinga ya Rho(D) kwa sindano ya misuli ndani ya siku 3 baada ya kujifungua. Dawa hii hujiunganisha na seli zozote nyekundu za damu za mtoto ambazo huenda zimepitishwa kwa mama ili seli nyekundu za damu zisisababishe mama kuzalisha kingamwili. Kingamwili kama hizo zinaweza kuhatarisha mimba zinazofuata.

Kabla ya kutoka hospitalini au kituo cha uzazi

Kabla ya kuondoka hospitalini au kituo cha kujifungulia, mama huchunguzwa. Ikiwa yeye pamoja na mtoto wana afya njema, kwa kawaida huwa wanaruhusiwa kuondoka ndani ya saa 24 hadi 48 baada ya kujifungua kwa njia ya uke na ndani ya saa 96 baada ya kujifungua kwa njia ya upasuaji. Wakati mwingine kuruhusiwa kuondoka hutokea mapema kama saa 6 baada ya kujifungua, ikiwa hakuna ganzi ya mwili wote iliyotumika na hakuna matatizo yaliyotokea.

Ziara za ufuatiliaji wa mara kwa mara huratibiwa, kwa kawaida huanza wiki 2 hadi 8 baada ya kujifungua. Ikiwa kulikuwa na matatizo wakati wa ujauzito au kujifungua, ziara ya kwanza inaweza kuratibiwa mapema zaidi.

Utunzaji Katika Wiki 6 za Kwanza Baada ya Kujifungua

Baada ya kujifungua, wanawake hupata mabadiliko mengi ya kimwili, na wakati mwingine kihisia. Madaktari hutoa mwongozo kwa wanawake kuhusu mabadiliko wanayoweza kutarajia, hutoa maelekezo kuhusu jinsi ya kudhibiti mabadiliko haya nyumbani, na kuelezea ni lini wanawake wanapaswa kutafuta msaada wa kimatibabu.

Kuvuja damu ukeni na kutokwa vitu

Kwa hadi wiki 6 baada ya kujifungua, mwanamke atavuja damu na kisha kutoka uchafu ukeni ambao hupungua kwa wingi na kubadilisha rangi. Mchanganyiko wa damu na kutoka uchafu baada ya kujifungua huitwa lochia, ambayo ina awamu 3: lochia rubra, lochia serosa na lochia alba. Kuvuja damu ukeni ni kawaida baada ya kujifungua, lakini ni muhimu kutambua wakati kuvuja damu ni kunapita kiasi au wakati kunaweza kuwa ishara ya tatizo (kama vile damu ilisitisha kuvuja kwa wiki moja kisha kuanza tena). Mwanamke aliye na wasiwasi kuhusu kuvuja damu nyingi au bila kutarajia anapaswa kuwasiliana na daktari wake.

Kuvuja damu kunaweza kupita kiasi katika saa chache za kwanza, kisha wingi hupungua hadi kiwango cha hedhi nzito. Kuvuja damu huendelea kwa siku 3 hadi 4 (lochia rubra).

Uchafu kutoka ukeni kisha hubadilika na kuwa uchafu wa rangi ya waridi au kahawia ukeni (lochia serosa), ambao hudumu kwa takriban siku 14. Karibu wiki 1 hadi 2 baada ya kujifungua, kigaga juu ya eneo ndani ya uterasi ambapo kondo la nyuma lilikuwa limeunganishwa hutoka, na kusababisha kutokwa na damu nyingi na kisha kutokwa na damu kidogo ambayo hudumu kwa takribani saa 1 hadi 2.

Kisha, uchafu unakuwa mweupe wa manjano (lochia alba), ambao hudumu hadi siku 14.

Pedi za usafi, zinazobadilishwa mara kwa mara, zinaweza kutumika kunyonya damu au uchafu unaotoka. Sodo zinazotiwa ndani ya uke hazipaswi kutumika hadi wiki 6 baada ya kujifungua.

Utunzaji wa vulva, uke na msamba

Baada ya kujifungua kwa njia ya uke, hasa ikiwa kulikuwa na mpasuko au episiotomia na mishono iliwekwa, wanawake kwa kawaida hupata maumivu au uvimbe wa uke, uke wa nje na msamba.

Kuoga sitz kwa maji ya joto kunaweza kusaidia kupunguza maumivu. Kuoga sitz kwa maji ya joto hufanywa ukiwa umeketi huku maji yakifunika angalau msamba na makalio. Baada ya kuoga sitz, eneo hilo linapaswa kuruhusiwa kukauka kabisa kabla ya kuvaa chupi.

Utunzaji wa chale ya upasuaji

Ikiwa mwanamke alijifungua kwa upasuaji, bendeji huondolewa baada ya siku 1 hadi 2. Vibanio vya upasuaji au mishono isiyoweza kufyonzwa kwa kawaida huondolewa ndani ya wiki 1. Mishono inayoweza kufyonzwa au gundi ya upasuaji haihitaji kuondolewa.

Sehemu ya ngozi iliyokatwa inapaswa kuwekwa safi na kavu. Ikiwa kuna uwekundu wowote karibu na mkato au utoaji wa damu au umajimaji kutoka kwenye mkato, mwanamke anapaswa kumpigia daktari wake.

Maumivu karibu na eneo la mkato hupungua baada ya muda. Mwanamke anaweza kupewa dawa za maumivu za afyuni kwa siku chache za kwanza baada ya kujifungua. Baada ya hapo, maumivu yanaweza kudhibitiwa kwa kutumia dawa za kupunguza uvimbe zisizo za steroidi (kama vile ibuprofen). Eneo linalozunguka mkato linaweza kuwa nyeti kwa mguso au shinikizo kwa miezi michache, na ganzi linaweza kudumu kwa muda mrefu zaidi.

Wanawake wanapaswa kuepuka kunyanyua vitu vizito (kwa kawaida hufafanuliwa kama kitu chochote kizito kuliko mtoto) kwa wiki 6 baada ya kujifungua kwa upasuaji.

Sehemu zingine za mwili zinaweza kuathiriwa

Uterasi bado imepanuka kwa hadi wiki 4 baada ya kujifungua. Kwa kawaida imeundwa kwa misuli, ambayo huendelea kukaza, na kufanya uterasi kuwa ndogo zaidi hadi itakaporudi kwenye ukubwa usio wa ujauzito. Mikazo hii inaweza kuwa chungu katika siku chache za kwanza baada ya kujifungua. Kwa kawaida, bado unaweza kuhisi uterasi kupitia tumbo kwa wiki 1 hadi 2 baada ya kujifungua, hadi iwe ndogo vya kutosha hadi sehemu ya juu (fundasi) iwe chini ya kiwango cha mfupa wa kinena. Mikazo huongezeka kwa kunyonyesha. Kunyonyesha huchochea uzalishaji wa homoni ya oksitosini. Oksitosini huchochea mtiririko wa maziwa (inayoitwa tendohisia la kuachilia) na pia huchochea mikazo ya uterasi.

Ngozi na misuli ya tumbo hunyooshwa na kulegea baada ya kujifungua, na hali yake ya kawaida hurejea polepole baada ya wiki kadhaa. Hata hivyo, ngozi na misuli ya tumbo kwa kawaida hairudi katika hali ya kabla ya ujauzito kwa miezi kadhaa, bila kujali kama unafanya mazoezi. Hata baada ya miezi kadhaa, kwa wanawake wengi, tumbo huendelea kutokeza zaidi kuliko kabla ya ujauzito.

Alama za kunyoosha kwenye ngozi ya tumbo au matiti haziondoki, lakini zinaweza kufifia taratibu baada ya mwaka mmoja.

Wanawake wengi hupoteza nywele katika wiki chache za kwanza baada ya kujifungua. Wanaweza kuona nywele zikitoka kwenye kitana au brashi au kwenye bomba la kuogea. Wakati wa ujauzito, viwango vya juu zaidi vya estrojeni husababisha vinyweleo vichache vya nywele kuingia katika awamu ya kupumzika (nywele huanguka wakati wa awamu hii), hivyo nywele huhisi kuwa nene kuliko kawaida. Hata hivyo, baada ya kujifungua, viwango vya estrojeni na mzunguko wa ukuaji wa nywele hurejea katika hali ya kawaida, na nywele za ziada huanguka.

Jedwali
Jedwali

Hisia

Huzuni (mabadiliko ya hisia baada ya kujifungua) ni jambo la kawaida siku chache baada ya kujifungua. Wanawake wanaweza pia kuhisi kukasirika, hisia kali, au wasiwasi na wanaweza kuwa na ugumu wa kumakinika au kupata matatizo ya kulala (kulala kidogo au sana). Dalili hizi kwa kawaida huisha baada ya wiki 1 hadi 2. Hata hivyo, ikiwa dalili hizi zitaendelea kwa zaidi ya wiki 2 au zinaathiri utunzaji wa mtoto au shughuli za kila siku, wanawake wanapaswa kuzungumza na daktari wao. Katika hali kama hizo, huenda una mfadhaiko wa baada ya kujifungua au tatizo lingine la afya ya akili.

Uzito

Wanawake wengi hawapunguzi uzito mara baada ya kujifungua na uzito unaweza hata kuongezeka katika siku chache za kwanza. Ingawa mtoto na kondo la nyuma vinatolewa, bado uterasi inaongezeka kwa ukubwa. Pia, uzito unaweza kuongezeka kutokana na ongezeko la majimaji katika damu kutokana na ujauzito, ongezeko la majimaji kutokana na majimaji yoyote uliyowekwa kwenye mishipa ya damu wakati wa uchungu wa uzazi na maziwa ya mama.

Viowevu vya ziada hutoka mwilini kwa kukojoa katika wiki 2 za kwanza. Kurejesha uzito wa kabla ya ujauzito kwa kawaida huchukua miezi 6 hadi 12, ukizingatia kula chakula bora na kufanya mazoezi.

Mazoezi

Wanawake wanaweza kuanza mazoezi ya kuimarisha misuli ya tumbo au misuli ya sehemu ya chini ya fupanyonga (mazoezi ya Kegel) ndani ya siku chache baada ya kujifungua kwa njia ya ukeni, ikiwa hakukuwa na jeraha kwenye misuli ya mkundu wakati wa kujifungua.

Kujifungua kwa upasuaji huwa upasuaji mkubwa, na wanawake hawapaswi kuanza kufanya mazoezi hadi watakapopona kikamilifu na kuruhusu uponyaji wa mkato wa upasuaji, ambao kwa kawaida huchukua takribani wiki 6.

Wanawake wanaweza kuendelea na ratiba yao ya mazoezi ya kabla ya ujauzito baada ya kupata idhini kutoka kwa daktari wao katika ziara yao ya baada ya kujifungua.

Shughuli za ngono na kupanga uzazi (kuzuia mimba au kupanga uzazi)

Unaweza kuanza shughuli za ngono ukitaka na ukihisi sawa, ingawa ushauri wa kawaida ni kusubiri hadi angalau wiki 6 baada ya kujifungua au hadi upone mpasuko wowote au uponyaji wa episiotomia umekamilike. Shughuli za ngono baada ya kujifungua kwa njia ya upasuaji zinapaswa kuahirishwa hadi mkato wa upasuaji utakapopona.

Ikiwa ngono inauma, mwanamke anapaswa kuacha kufanya ngono na kuwasiliana na daktari wake ili kutathminiwa. Wakati mwingine ngono ya uke huwa si raha ikiwa mwanamke ananyonyesha kwa sababu kunyonyesha kunaweza kupunguza viwango vya estrojeni, ambayo inaweza kusababisha ukavu wa uke.

Wanawake ambao hawanyonyeshi kwa kawaida huanza kutoa yai tena takriban wiki 4 hadi 6 baada ya kujifungua. Mara tu utoaji wa yai ukitokea, watapata hedhi takriban wiki 2 baadaye. Hata hivyo, utoaji yai unaweza kutokea mapema; wanawake wamekuwa wajawazito hata wiki 2 baada ya kujifungua. Wanawake wanaonyonyesha maziwa ya mama pekee (wanawanyonyesha watoto wao maziwa ya mama pekee) kwa kawaida hutoa yai na kupata hedhi baadaye, kwa kawaida karibu na miezi 6 baada ya kujifungua, ingawa wachache hutoa yai na kupata hedhi (na kupata mimba) haraka kama wale ambao hawanyonyeshi.

Ili kupunguza uwezekano wa kupata mimba, wanawake wanaofanya ngono na wanaume wanapaswa kuanza kutumia njia za kupanga uzazi kabla ya kuanza tena ngono. Wataalamu wa afya wanapendekeza kusubiri kupata mimba nyingine kwa angalau miezi 6 lakini ikiwezekana miezi 18 baada ya kujifungua.

Wanawake ambao wamepewa chanjo dhidi ya rubela na/au tetekuwanga (varisela) lazima wasubiri angalau mwezi 1 kabla ya kupata mimba tena ili kuepuka kuhatarisha kijusi.

Madaktari mara nyingi hujadili chaguo za kupanga uzazi kabla na baada ya kujifungua.

Baadhi ya njia za kupanga uzazi zinaweza kuanza mara tu baada ya kujifungua, ikiwa ni pamoja na:

  • Mbinu za projestini pekee (vipandikizi, sindano au tembe): Unaweza kuanza mara baada ya kujifungua kwa njia ya uke au upasuaji

  • Vifaa vya kuwekwa ndani ya uterasi: Uingizaji wa mara moja unawezekana baada ya kujifungua kwa njia ya ukeni, ndani ya dakika 10 baada ya kondo la nyuma kutolewa

  • Uhasi wa kike: Unaweza kufanywa wakati wa utaratibu sawa na upasuaji wa kujifungua au ndani ya siku 1 hadi 2 baada ya kujifungua kwa njia ya uke.

Aina nyingi za kupanga uzazi zinaweza kutumika hata kama mwanamke ananyonyesha, ingawa tembe za kupanga uzazi (au pete au viraka) zinazojumuisha estrojeni hazipaswi kuanza hadi wiki 3 baada ya kujifungua kwa sababu estrojeni inaweza kuongeza hatari ya kuganda kwa damu (kuganda kwa damu ya vena kubwa au kuziba wa mishipa ya mapafu). Pia, kupanga uzazi ukitumia estrojeni kunaweza kupunguza kwa muda kiasi cha maziwa ambacho mwanamke hutoa. Baadhi ya wanawake hupendelea kusubiri kuanza mbinu hizi hadi baada ya kunyonyesha kuimarika.

Mbinu za homoni ambazo ni projestini-pekee, kama vile aina fulani za tembe za kupanga uzazi, sindano za medroxyprogesterone acetate, na vipandikizi vya projestini, havina athari kubwa au havina athari yoyote kwenye uundaji wa mgando wa damu na haziathiri uzalishaji wa maziwa. 

Kifaa cha kuwekwa ndani ya uterasi (IUD) kinaweza kuwekwa mara baada ya kujifungua kwa njia ya ukeni au wakati mwingine wowote baada ya kujifungua.

Wanawake ambao hawataki kupata mimba siku zijazo wanaweza kuchagua uhasi wa kike. Taratibu hizi za upasuaji zinahusisha kukata au kuziba mirija ya falopio ili kuzuia manii kufikia na kutungisha yai. Uhasi wa kike unaweza kufanywa ndani ya siku 1 hadi 2 baada ya kujifungua kwa njia ya uke (kupitia mkato mdogo chini ya kitovu), wakati wa utaratibu sawa na kujifungua kwa upasuaji, au baada ya kipindi cha baada ya kujifungua (wiki 6 baada ya mtoto kuzaliwa). Taratibu hizi zinachukuliwa kuwa za kudumu na zisizoweza kubadilishwa. Wenzi wa kiume wanaweza pia kuchagua uhasi wa kiume (vasektomi).

Kiwambo kinaweza kuwekwa tu baada ya uterasi kurudi kwenye ukubwa usio wa ujauzito, kwa kawaida baada ya takribani wiki 6 hadi 8. Ikiwa mwanamke alitumia kiwambo kabla ya ujauzito, anapaswa kuwa na kiwango kingine baada ya kujifungua, kwa sababu ukubwa tofauti wa kiwambo unaweza kuhitajika. Ikiwa atafanya ngono kabla ya hapo, povu, jeli na kondomu zinaweza kutumika.

Je, Ulijua...

  • Wanawake wanaweza kupata mimba hata wiki 2 baada ya kujifungua.

Nyonyesha

Madaktari wanapendekeza kwamba wanawake wanyonyeshe kwa angalau miezi 6 bila kujumuisha vyakula vingine. Kisha wanawake wanapaswa kuendelea kunyonyesha kwa miezi mingine 6 huku mtoto pia akianza kupewa vyakula vingine. Baada ya hapo, wanawake wanahimizwa kuendelea kunyonyesha hadi wao wenyewe au mtoto atakapokuwa hapendelei tena.

Ikiwa mama hawawezi kunyonyesha au wameamua kutonyonyesha, watoto wanaweza kulishwa maziwa ya unga ya watoto kwa chupa badala yake.

Wanawake wengi hupata kwamba kujifunza kuhusu kunyonyesha kabla ya kujifungua kunasaidia. Taarifa kuhusu kunyonyesha zinaweza kutoka kwenye vitabu au tovuti au kupitia hospitali ya karibu, shirika la usaidizi wa kunyonyesha, au mshauri wa kunyonyesha. Mara nyingi baada ya kujifungua, muuguzi au mkunga anaweza kumsaidia mwanamke kujifunza jinsi ya kunyonyesha.

Kuanza kunyonyesha

Kwa siku 2 hadi 6 za kwanza baada ya kujifungua, matiti hutoa kolostramu, ambayo ni nzito na kwa kawaida huwa ya manjano. Kisha matiti huanza kutoa maziwa. Wakati mabadiliko haya yanapotokea (inayoitwa "maziwa yanapokuja"), matiti hujaa na huwa na joto, na maziwa huwa na rangi nyeupe na uthabiti mwembamba kuliko kolostramu.

Utunzaji wa matiti

Akina mama wanaonyonyesha wanahitaji kujifunza jinsi ya kumshika mtoto wakati wa kunyonyesha. Ikiwa mtoto hajashikwa vizuri, chuchu za mama zinaweza kuuma na kupasuka. Kwa mfano, wakati mwingine mtoto huvuta mdomo wake wa chini na kuunyonya, na hivyo kuwasha chuchu. Katika hali kama hizo, mama anaweza kuondoa mdomo wa mtoto mdomoni kwa kidole gumba. Ili kuondoa chuchu yake mdomoni mwa mtoto, mama anapaswa kwanza kuingiza kidole chake kinywani mwa mtoto ili kuondoa uvutaji unaosababishwa na kunyonya.

Baada ya kunyonyesha, mama anaweza kuacha maziwa yakauke yenyewe kwenye chuchu au kuyapapasa taratibu. Akitaka, anaweza kukausha chuchu zake kwa kutumia mashine ya kukaushia nywele iliyowekwa katika hali ya ukaushaji wa chini. Baada ya kunyonyesha, wanawake wanaweza kupaka lanolini 100% kwenye chuchu ili kupunguza maumivu na kusaidia kulinda chuchu.

Mama anaponyonyesha, matiti yanaweza kuvuja maziwa. Pedi za pamba zinaweza kuvaliwa ili kufyonza maziwa. Pedi ya plastiki za sidiria zinaweza kuwasha chuchu na hazipaswi kutumika.

Lishe wakati wa kunyonyesha

Wakati wa kunyonyesha, mama anahitaji kuongeza ulaji wake wa kalori kwa takriban kalori 300 hadi 500 kwa siku. Pia anapaswa kuongeza ulaji wake wa vitamini na madini mengi, kama vile kalsiamu. Kwa kawaida, kula lishe bora (ikiwa ni pamoja na bidhaa za maziwa na mboga za majani mabichi za kutosha) na kuendelea kutumia vitamini ya kabla ya kujifungua yenye folati mara moja kwa siku ndio msingi wa vitu ambavyo mama anahitaji kufanya. Vitamini za kabla ya kujifungua zinapaswa kuwa na angalau mikrogramu 400 za folati. Wanawake wanaonyonyesha wanapaswa kunywa maji ya kutosha ili kuhakikisha upatikanaji wa maziwa ya kutosha. Akina mama wanakula lishe maalum wanapaswa kushauriana na daktari wao kuhusu hitaji la virutubisho vingine vya vitamini na madini, kama vile vitamini B12 kwa walaji mboga.

Ikiwa wanawake wanaonyonyesha wanakula samaki, wanapaswa kuchagua aina za samaki ambazo zina kiwango cha chini cha zebaki. Angalia Zebaki katika vyakula vya baharini kwa maelezo zaidi.

Kuvimba matiti

Matiti yanaweza kuwa makubwa, magumu, yanayokaza na yenye maumivu ikiwa yamejaa maziwa mengi (kuvimba). Kuvimba kwa matiti kunaweza kutokea katika hatua yoyote ya uzalishaji wa maziwa (kunyonyesha).

Kwa wanawake wanaonyonyesha, yafuatayo yanaweza kusaidia ikiwa matiti yatakuwa yamevimba:

  • Kumnyonyesha mtoto mara kwa mara

  • Kuvaa sidiria ya kusaidia kunyonyesha saa 24 kwa siku

  • Kukamua maziwa kwa mkono au kutumia pampu ya matiti kati ya kunyonyesha (hata hivyo, hii inaweza kuchochea uzalishaji wa maziwa na kuongeza muda wa kuvimba)

Ikiwa matiti yamevimba sana, mwanamke anaweza kulazimika kukamua maziwa kabla tu ya kunyonyesha ili kupunguza ugumu wa matiti na kuwezesha mdomo wa mtoto kutoshea karibu na areola (eneo lenye rangi kuzunguka chuchu).

Kwa wanawake ambao hawatanyonyesha au wameacha kunyonyesha, yafuatayo yanaweza kusaidia:

  • Kuvaa sidiria inayobana vizuri ili kuweka shinikizo kwenye matiti na hivyo kusaidia kukandamiza uzalishaji wa maziwa

  • Kutumia pakiti za barafu na kutumia dawa za kutuliza maumivu (kama vile acetaminophen au ibuprofen) ili kupunguza usumbufu hadi uzalishaji wa maziwa utakapokoma wenyewe

  • Kujizuia kukamua maziwa kwa mikono, jambo linaloweza kuongeza uzalishaji wa maziwa kwa sababu kukamua maziwa huambia mwili maziwa zaidi yanahitajika

Katika hali fulani, daktari wa mwanamke anaweza kupendekeza atumie dawa, kama vile cabergoline, ili kukandamiza uzalishaji wa maziwa.

Je, Ulijua...

  • Wakati matiti yanapovimba kwa maziwa, kukamua maziwa kati ya kunyonyesha hupunguza shinikizo kwa muda lakini kwa ujumla kunaweza kufanya kuvimba kuwa kubaya zaidi kwa sababu kukamua maziwa huambia mwili maziwa zaidi yanahitajika.