Njia za Kupata Mimba Kwa Kudhibiti Homoni

NaFrances E. Casey, MD, MPH, NYU Grossman Long Island School of Medicine
Imekaguliwa naOluwatosin Goje, MD, MSCR, Cleveland Clinic, Lerner College of Medicine of Case Western Reserve University
Imepitiwa/Imerekebishwa Aug 2023 | Imebadilishwa Apr 2024
v8951249_sw

Homoni za uzazi wa mpango zinaweza

  • Kumezwa kwa mdomo (vidonge vya kuzuia mimba)

  • Huingizwa ukeni (pete ya kutia ukeni)

  • Kupandikwa kwenye ngozi (kiraka)

  • Kupandikizwa chini ya ngozi

  • Kudungwa kwenye misuli

Homoni zinazotumika kuzuia mimba ni pamoja na estrojeni na projestini (dawa zinazofanana na homoni za projesteroni). Estrojeni na projestini ndizo homoni kuu zinazohusika katika mzunguko wa hedhi. Mbinu za homoni huzuia mimba hasa kwa kuzuia ovari kutoa mayai au kwa kufanya ute kwenye mlango wa kizazi kuwa mzito ili mbegu za kiume zisiweze kupenya kwenye mlango wa kizazi kwenda kwenye uterasi. Hivyo, mbinu za homoni huzuia yai kutungishwa.

Mbinu zote za homoni zinaweza kuwa na madhara na vikwazo sawia vya matumizi.

Vidonge vya Uzazi wa Mpango

Vidonge vya uzazi wa mpango vya kumeza, vinavyojulikana kama vidonge vya uzazi wa mpango au "tembe" tu, vina homoni, ama mchanganyiko wa estrojeni na projestini au projestini pekee.

Vidonge vya mchanganyiko (vidonge vyenye estrojeni na projestini) kwa kawaida humezwa mara moja kwa siku kwa siku 21 hadi 24, kisha vinakosa kutumiwa kwa siku 4 hadi 7 (kuruhusu kipindi cha hedhi kutokea), kisha huanza kutumiwa tena. Vidonge visivyo amilifu (placebo) kwa kawaida hutumika kwa siku ambazo vidonge vya mchanganyiko havitumiwi ili kuanzisha utaratibu wa kutumia kidonge kimoja kwa siku. Kidonge kisicho amilifu kinaweza kuwa na chuma na folate. Chuma kimejumuishwa ili kusaidia kuzuia au kutibu upungufu wa chuma kwa sababu chuma hupotea katika damu ya hedhi kila mwezi. Folate hujumuishwa endapo wanawake, ambao bila kujua wanaweza kuwa na upungufu wa folate, watapata mimba. Upungufu wa folate kwa mwanamke mjamzito huongeza hatari ya mtoto kupata kasoro za kuzaliwa nazo kama vile spina bifida.

Wakati mwingine vidonge vya uzazi wa mpango vya estrojeni-projestini humezwa kila siku kwa wiki 12, kisha havimezwi kwa wiki 1. Kwa hivyo, hedhi hutokea mara 4 tu kwa mwaka. Au hutumia kama kidonge amilifu kila siku. Kwa aina hii, hakuna kutokwa na damu kulikoratibiwa (hakuna hedhi), lakini kutokwa damu kusiko kwa kawaida kuna uwezekano mkubwa wa kutokea.

Takriban asilimia 0.3 ya wanawake wanaotumia vidonge vya mchanganyiko kama ilivyoelekezwa hupata mimba wakati wa mwaka wa kwanza wa matumizi. Hata hivyo, uwezekano wa kupata mimba huongezeka sana endapo wanawake wataacha kutumia kidonge, hasa cha kwanza katika mzunguko wa hedhi. Kwa matumizi ya kawaida (jinsi watu wengi wanavyotumia), takriban asilimia 9 ya wanawake wanapata mimba katika kipindi cha mwaka wa kwanza wa matumizi.

Kiwango cha estrojeni katika vidonge vya mchanganyiko hutofautiana. Katika vidonge vya mchanganyiko, kipimo cha estrojeni huanzia mikrogramu 10 hadi 35. Wanawake wenye afya njema ambao hawavuti sigara wanaweza kutumia vidonge vya mchanganyiko vya dozi ndogo hadi watakapokoma hedhi.

Ikiwa wanawake watakosa kumeza kidonge cha mchanganyiko siku moja, wanapaswa kutumia vidonge viwili siku inayofuata. Ikiwa watasahau kumeza kidonge kwa siku 2, wanapaswa kuendelea kutumia kidonge kimoja kila siku na wanapaswa kutumia njia mbadala ya uzazi wa mpango kwa siku 7 zijazo. Endapo wanawake watasahau kumeza kidonge kwa siku 2 na wamefanya ngono bila kinga ndani ya siku 5 kabla ya siku hizo 2, wanaweza kuzingatia kutumia kingamimba ya dharura.

Wanawake walio na saratani ya matiti kwa sasa hawapaswi kutumia vidonge vilivyochanganywa vya estrojeni-projestini, viraka au pete.

Vidonge vya projestini pekee hutumiwa kila siku ya mwezi, na ni muhimu kutumia aina hii ya kidonge cha uzazi wa mpango kwa wakati mmoja wa siku. Mara nyingi husababisha kutokwa na damu kusiko kawaida. Viwango vya ujauzito kwa kutumia vidonge hivi na kwa kutumia vidonge mchanganyiko ni sawia, kama vitatumika kama ilivyoelekezwa. Vidonge vya projestini pekee kwa kawaida huandikiwa tu wanawake ambao hawapaswi kutumia estrojeni. Kwa mfano, vidonge vyenye projestini pekee vinaweza kutumiwa na wanawake ambao wana kipandauso chenye dalili zinazotokea kabla ya maumivu ya kichwa, shinikizo la damu, au kisukari kibaya (angalia Masharti Yanayokataza Matumizi ya Vidonge Mchanganyiko vya Kuzuia Mimba) na, kwa hivyo, hawapaswi kutumia estrojeni. Endapo zaidi ya saa 27 zinapita kati ya kutumia vidonge vya projestini pekee, wanawake wanapaswa kutumia njia mbadala ya uzazi wa mpango kwa siku 7 zijazo pamoja na kutumia kidonge cha projestini pekee kila siku. Wanawake walio na saratani ya matiti kwa sasa hawapaswi kutumia vidonge, vipandikizi, au sindano zenye projestini pekee.

Kunzia tembe za kupanga uzazi

Kabla ya kuanza kutumia vidonge vya uzazi wa mpango, mwanamke lazima amuone daktari. Madaktari humwuliza mwanamke huyo kuhusu historia yake ya kimatibabu, kijamii, na kifamilia ili kubaini kama ana matatizo yoyote ya kiafya ambayo yangefanya kutumia dawa hizi za uzazi wa mpango kuwa hatari kwake. Wanapima shinikizo la damu yake. Ikiwa lipo juu, vidonge mchanganyiko vya kuzuia mimba (estrojeni pamoja na projestini) havipaswi kutolewa. Kipimo cha ujauzito kinaweza kujua kama kuna ujauzito. Madaktari pia mara nyingi hufanya uchunguzi wa kimwili, ingawa uchunguzi huu si lazima kabla ya mwanamke kuanza kutumia vidonge vya uzazi wa mpango. Miezi mitatu baada ya kuanza kutumia dawa za kuzuia mimba, mwanamke anapaswa kufanyiwa uchunguzi mwingine ili kubaini endapo shinikizo la damu limebadilika. Kama hailijabadilika, basi anapaswa kufanyiwa uchunguzi mara moja kwa mwaka. Vidonge vya uzazi wa mpango vinaweza kutolewa kwa miezi 13 kwa wakati mmoja.

Wanawake wanaweza kuanza kutumia vidonge vya uzazi wa mpango wakati wowote wa mwezi. Hata hivyo, wakianza kuvitumia zaidi ya siku 5 baada ya siku ya kwanza ya hedhi yao, wanapaswa kutumia njia mbadala ya uzazi wa mpango kwa siku 7 zijazo pamoja na kutumia vidonge vya uzazi wa mpango.

Wakati ambapo wanawake wanaweza kuanza kutumia vidonge mchanganyiko vya uzazi wa mpango baada ya ujauzito hutofautiana:

  • Baada ya kuharibika kwa mimba au kutoa mimba wakati wa trimesta ya kwanza ya ujauzito: Kuanza mara moja

  • Baada ya kuharibika kwa mimba, kujifungua, au kutoa mimba wakati wa trimesta ya pili ya ujauzito: Kuanza ndani ya wiki 1 ikiwa hawana sababu nyingine za hatari za kuganda kwa damu (kama vile uvutaji sigara, kisukari, au shinikizo la damu)

  • Baada ya kujifungua mimba iliyofikisha wiki 28: Subiri siku 21 (subiri siku 42 ikiwa wanawake wananyonyesha au wana hatari ya kuganda kwa damu, ikiwa ni pamoja na kujifungua kwa njia ya upasuaji)

Wanawake wenye viashiria hatarishi vya kuganda kwa damu wanapaswa kusubiri kwa sababu kuganda kwa damu kuna uwezekano mkubwa wa kutokea wakati wa ujauzito na baada ya kujifungua. Kutumia dawa mchanganyiko za uzazi wa mpango pia hufanya damu kuganda zaidi.

Vidonge vya uzazi wa mpango vya kumeza vyenye projestini pekee vinaweza kumezwa mara baada ya kujifungua mtoto.

Kwa wanawake wengi ambao wamejifungua hivi karibuni na wananyonyesha pekee na ambao hawajapata hedhi, kuna uwezekano mdogo wa kupata mimba kwa miezi 6 baada ya mtoto kuzaliwa, hata kama hakuna njia ya kuzuia mimba inayotumika. Hata hivyo, kuanza kutumia uzazi wa mpango ndani ya miezi 3 baada ya kujifungua kunapendekezwa endapo kulisha kwa kutumia chupa kumeanzishwa au kuna ukatikazi wowote katika kunyonyesha.

Ikiwa mwanamke ana ugonjwa wa ateri ya moyo au kisukari au ana vihatarishi vya magonjwa hayo (kama vile ndugu wa karibu mwenye lolote kati ya hayo mawili), kipimo cha damu kwa kawaida hufanywa ili kupima viwango vya lehemu, mafuta mengine (lipidi), na sukari (glukosi) kabla ya kuandikiwa vidonge mchanganyiko vya kuzuia mimba. Hata kama viwango hivi si vya kawaida, madaktari bado wanaweza kuwaandikia vidonge mchanganyiko vya kuzuia mimba vya estrojeni kwa dozi ndogo. Hata hivyo, mara kwa mara huwa wanafanya vipimo vya damu ili kufuatilia viwango vya mafuta na sukari vya mwanamke. Wanawake wenye kisukari kwa kawaida wanaweza kutumia vidonge mchanganyiko vya uzazi wa mpango isipokuwa kama kisukari kimeharibu mishipa ya damu au wamekuwa na kisukari kwa zaidi ya miaka 20.

Ikiwa mtu amewahi kuwa na tatizo la ini, madaktari hufanya vipimo ili kutathmini kama ini linafanya kazi vizuri. Endapo matokeo ni ya kawaida, wanaweza kutumia dawa za kuzuia mimba kwa njia ya mdomo.

Pia kabla ya kuanza kutumia vidonge vya kuzuia mimba kwa njia ya mdomo, mwanamke anapaswa kuzungumza na daktari wake kuhusu faida na hasara za njia za uzazi wa mpango kwa hali yake.

Faida

Faida kuu ya vidonge vya uzazi wa mpango vya kumeza (tembe za uzazi wa mpango) ni uzazi wa mpango unaotegemeka na unaoendelea endapo vidonge vitamezwa kama ilivyoelekezwa.

Pia, kutumia vidonge vya uzazi wa mpango hupunguza kutokea kwa yafuatayo:

Hatari ya kupata saratani ya uterasi na saratani ya ovari hupunguzwa kwa angalau miaka 20 baada ya dawa za uzazi wa mpango kusimamishwa. Dawa za uzazi wa mpango za kumeza hupunguza hatari ya saratani ya uterasi kwa asilimia 60 baada ya angalau miaka 10 ya matumizi na saratani ya ovari kwa takriban miaka 50 baada ya kuzitumia kwa miaka 5 na kwa asilimia 80 baada ya kuzitumia kwa miaka 10 au zaidi.

Vidonge vya uzazi wa mpango vinavyomezwa mapema katika ujauzito havidhuru kijusi. Hata hivyo, vinapaswa kusitishwa mara tu mwanamke anapogundua kuwa ni mjamzito. Dawa za uzazi wa mpango za kumeza hazina athari yoyote ya muda mrefu kwenye uwezo wa kuzaa, ingawa mwanamke anaweza asitoe yai kwa miezi kadhaa baada ya kuacha kutumia dawa.

Je, Ulijua...

  • Vidonge vya uzazi wa mpango vya homoni vina faida kadhaa za kiafya (kama vile kupungua kwa hatari ya kupata saratani ya ovari kwa wanawake wanaotumia aina fulani za vidonge vya uzazi wa mpango).

Hasara

Ingawa vidonge vya kuzuia mimba vinaweza kuwa na madhara fulani, hatari ya jumla ya madhara haya ni ndogo. Kufura tumbo, maumivu ya matiti, kichefuchefu, na maumivu ya kichwa ndiyo madhara yanayotokea sana.

Vidonge vyenye projestini pekee mara nyingi husababisha kutokwa na damu ukeni bila mpangilio.

Kutokwa na damu nyingi na kukosa hedhi (amenorrhea) ni jambo la kawaida katika kipindi cha miezi kadhaa ya mwanzo ya kutumia vidonge mchanganyiko vya uzazi wa mpango, hasa endapo wanawake wanasahau kumeza vidonge, lakini kwa kawaida huacha mwili unapozoea homoni. Kutokwa na damu nyingi ni kuvuja damu kunakotokea wakati usio wa hedhi, wakati wanawake wanatumia kidonge kinachofanya kazi. Madaktari wanaweza kuongeza dozi ya estrojeni kudhibiti matatizo ya kutokwa na damu nyingi na kukoma kwa hedhi.

Baadhi ya madhara yanahusiana na estrojeni kwenye kidonge. Yanaweza kujumuisha kichefuchefu, kufura tumbo, ubakizaji wa maji mwilini, ongezeko la shinikizo la damu, uchungu wa matiti, na maumivu ya kichwa yanayosababishwa na kipandauso. Zingine, kama vile chunusi na mabadiliko ya hamu ya kula na hisia, zinahusiana zaidi na aina au kipimo cha projestini. Baadhi ya wanawake wanaotumia vidonge vya uzazi wa mpango wanaongezeka uzito kwa pauni 3 hadi 5 kwa sababu huhifadhi maji mwilini au kwa sababu hamu ya kula huongezeka. Madhara mengi kati ya haya hayatokei sana kwa vidonge vya dozi ya chini.

Dawa za uzazi wa mpango za kumeza pia zinaweza kusababisha kutapika, maumivu ya kichwa, mfadhaiko, na matatizo ya usingizi.

Kwa baadhi ya wanawake, dawa za uzazi wa mpango za kumeza husababisha sehemu nyeusi usoni (melasma), sawa na yale yanayoweza kutokea wakati wa ujauzito. Kuathiriwa na jua hufanya sehemu hizo kuwa nyeusi zaidi. Ikiwa sehemu nyeusi zitatokea, madaktari kwa kawaida huacha kutumia vidonge vya kuzuia mimba vya kumeza. Sehemu hizo hufifia polepole baada ya kusitisha kutumia vidonge vya kuzuia mimba.

Kutumia vidonge vya kuzuia mimba huongeza hatari ya kupata matatizo fulani.

Hatari ya kupata tatizo la kuganda kwa damu kwenye mishipa inaweza kuwa mara 2 hadi 4 zaidi kwa wanawake wanaotumia vidonge mchanganyiko vya uzazi wa mpango kuliko ilivyokuwa kabla ya kuanza kutumia vidonge vya uzazi wa mpango. Endapo wanawake wana tatizo linalosababisha kuganda kwa damu au wana wanafamilia ambao wamewahi kuwa na tatizo la kuganda kwa damu, tathmini zaidi inahitajika. Wanawake hawa huenda wasiweze kutumia dawa za kuzuia mimba zenye estrojeni. Ikiwa mwanamke anayetumia vidonge vya uzazi wa mpango atapata uvimbe kwenye mguu mmoja, maumivu ya kifua, au upungufu wa pumzi, anapaswa kumuona daktari mara moja. Ikiwa madaktari wanashuku kuwa mwanamke anayetumia dawa za kuzuia mimba ana thrombosis ya mshipa mrefu (damu iliyoganda, kwa kawaida kwenye mguu) au embolism ya mapafu (damu kuganda kwenye mapafu), dawa za uzazi wa mpango husitishwa mara moja. Kisha vipimo hufanywa ili kuthibitisha au kubaini tatizo.

Upasuaji huongeza hatari ya kuganda kwa damu, kwa hivyo wanawake wanapaswa kuacha kutumia dawa za kuzuia mimba kabla ya upasuaji. Wanapaswa kumuuliza daktari wao kuhusu muda wanaopaswa kuacha na kuanza tena kutumia vidonge vya uzazi wa mpango. Vizuizi vya mwendo (kutoweza kutembea) kutokana na jeraha au kusafiri pia huongeza hatari ya kuganda kwa damu. Hivyo, endapo mwendo wa mwanamke umepungua, anaweza kuhitaji kujaribu kuzunguka-zunguka kadiri iwezekanavyo au kuchukua hatua zingine ili kuzuia kuganda kwa damu. Kwa mfano, wanawake wanaweza kuinua miguu yao, kukunja na kupanua vifundo vya miguu yao takriban mara 10 kila baada ya dakika 30, na/au kutembea na kujinyoosha kila baada ya saa 2 wanaposafiri.

Saratani ya shingo ya kizazi ina uwezekano mkubwa zaidi wa kutokea kwa wanawake ambao wanatumia tembe za kuzuia mimba kwa zaidi ya miaka 5. Lakini miaka 10 baada ya kuacha kutumia, hatari hii inapungua kurudi ilivyokuwa kabla ya kuanza kutumia dawa za kumeza za kuzuia mimba. Pia, haijulikani wazi kama hatari iliyoongezeka inahusiana na tembe za kuzuia mimba. Wanawake wanaotumia dawa za kuzuia mimba za kumeza wanapaswa kufanya vipimo vya Papanicolaou (Pap) kama ilivyopendekezwa na daktari wao. Vipimo hivyo vinaweza kugundua mabadiliko ya kabla ya saratani kwenye shingo ya kizazi mapema, kabla hayajasababisha saratani.

Dawa za kuzuia mimba za kumeza kwa mdomo hazipaswi kutumiwa ikiwa kolestasisi au homa ya manjano imetokea kutokana na matumizi ya awali. Wanawake ambao wamewahi kupata kolestasisi ya ujauzito wanaweza kupata homa ya manjano wakimeza vidonge vya uzazi wa mpango, na vidonge vya uzazi wa mpango vinapaswa kutumiwa kwa tahadhari.

Mawe ya nyongo hayana uwezekano mkubwa wa kutokea kwa wanawake wanaotumia vidonge vya uzazi wa mpango vya kumeza kwa dozi ndogo.

Hatari ya kuwa na mshtuko wa moyo huongezeka ikiwa wanawake wenye umri wa miaka 35 au zaidi ambao wanavuta sigara wanatumia vidonge vya uzazi wa mpango. Kwa kawaida, wanawake hao hawapaswi kutumia dawa za kuzuia mimba za kumeza kwa mdomo.

Ikiwa wanawake wana kiwango cha juu cha triglyceride (mafuta), kutumia vidonge vya mchanganyiko vya uzazi wa mpango kunaweza kuongeza kiwango hicho zaidi. Kiwango cha juu cha triglyceride kinaweza kuongeza hatari ya mshtuko wa moyo au kiharusi kwa watu ambao wana vihatarishi vya matatizo haya. Dawa za uzazi wa mpango za kumeza kwa mdomo huongeza hatari ya kuganda damu (ambayo inaweza pia kuchangia mshtuko wa moyo na kiharusi). Kwa hivyo, wanawake walio na kiwango cha juu cha triglyceride hawapaswi kutumia vidonge mchanganyiko vya kuzuia mimba.

Kwa nadra, uvimbe wa ini usio na saratani (adenoma ya seli ya ini) hutokea. Endapo uvimbe huu utapasuka ghafla na kutoa damu kwenye tumbo, upasuaji wa dharura unahitajika. Hata hivyo, kutokwa na damu kwa aina hiyo ni nadra. Kutumia dawa za kumeza za kuzuia mimba kwa muda mrefu na kwa dozi kubwa huongeza hatari ya kupata uvimbe huu. Uvimbe kwa kawaida hutoweka baada ya dawa za kuzuia mimba kusitishwa.

Kutumia dawa fulani kunaweza kufanya dawa za uzazi wa mpango za kumeza zisiwe na ufanisi. Dawa hizi ni pamoja na zifuatazo:

Endapo wanawake wanaotumia dawa za kuzuia mimba kwa njia ya mdomo watalazimika kutumia mojawapo ya dawa hizi, wanapaswa pia kutumia njia nyingine ya kuzuia mimba wanapotumia dawa, na wanapaswa kuendelea kutumia njia nyingine ya kuzuia mimba hadi hedhi yao ya kwanza itakapotokea baada ya kuacha kutumia dawa. Wanawake hawapaswi kutumia lamotrigine (dawa ya kuzuia kifafa) pamoja na dawa za uzazi wa mpango za kumeza kwa mdomo. Dawa za uzazi wa mpango za kumeza kwa mdomo zinaweza kufanya lamotrigine isiwe na ufanisi mkubwa katika kudhibiti vifafa.

Hali ambazo zinazuia matumizi ya muunganisho wa tembe za kupanga uzazi

Mwanamke hapaswi kutumia dawa mchanganyiko za uzazi wa mpango za kumeza (vidonge vyenye estrojeni na projestini) ikiwa kuna yoyote kati ya hali zifuatazo:

Mazingatio mengine

Mambo mengine yanaweza kusababisha hatari za kiafya kwa kutumia tembe mchanganyiko za uzazi wa mpango, na yanapaswa kujadiliwa na daktari kabla ya kuanza kutumia njia hii ya uzazi wa mpango. Hizi zinajumuisha

  • Vihatarishi vya damu kuganda (hasa muda mfupi baada ya ujauzito)

  • Uvutaji sigara

  • Shinikizo la juu la damu

  • Ugonjwa wa moyo

  • Matatizo ya kibofu cha nyongo au ini

  • Historia ya upasuaji wa bariatric

  • Saratani ya matiti ya zamani

  • Sklerosisi nyingi pamoja na matatizo ya kutembea

  • Matumizi ya dawa fulani za antibiotiki au dawa za kuzuia kifafa

Vidonge vya uzazi wa mpango vyenye projestini pekee vina hatari chache na mara nyingi hutumiwa na wanawake ambao hawawezi kutumia estrojeni. Baadhi ya mambo yanayoweza kusababisha hatari za kiafya kwa kutumia dawa ya uzazi wa mpango yenye projestini pekee na yanapaswa kujadiliwa na daktari ni pamoja na

  • Kutokwa na damu ukeni kusiko kawaida kwa sasa

  • Shinikizo la juu la damu

  • Ugonjwa wa moyo

  • Matatizo ya mishipa ya damu yanayosababishwa na kisukari au lupus

  • Matatizo ya ini

  • Upasuaji wa bariatric

  • Historia ya saratani ya matiti

Vidonge vya uzazi wa mpango vya kumeza havisababishi ongezeko lolote, au pengine vinasababisha ongezeko dogo, la hatari ya kupata saratani ya matiti kwa wanawake wanaovitumia kwa sasa au waliovitumia miaka michache iliyopita.

Kwa wanawake wenye afya njema ambao hawavuti sigara, kutumia vidonge mchanganyiko vya dozi ndogo vyenye dozi ndogo ya estrojeni hakuongezi hatari ya kupata kiharusi au mshtuko wa moyo.

Viraka vya Ngozi vya Kupanga Uzazi na Pete za Kutia Ukeni

Dawa za uzazi wa mpango zenye mchanganyiko wa estrojeni na projestini zinapatikana kama viraka vya ngozi na pete za kutia ukeni. Zinapaswa kutumiwa kwa wiki 3, kisha zisitumike kwa wiki 1 ili kuruhusu hedhi kutokea. Endapo wanawake hawataanza kutumia kiraka au pete wakati wa siku 5 za kwanza za hedhi yao, lazima watumie njia mbadala ya uzazi wa mpango wakati wa siku 7 za kwanza wanazotumia kiraka au pete.

Viraka vya ngozi na pete za kutia ukeni za uzazi wa mpango ni njia zenye ufanisi. Takriban asilimia 0.3 ya wanawake wanaotumia mojawapo ya njia hizi kama ilivyoelekezwa hupata mimba katika kipindi cha mwaka wa kwanza wa matumizi. Kwa matumizi ya kawaida (jinsi watu wengi wanavyotumia), karibu asilimia 9 hupata mimba katika kipindi cha mwaka wa kwanza. Ufanisi ni sawa na ule wa vidonge vya uzazi wa mpango vya kumeza. Ufanisi wa kiraka unaweza kuwa chini kwa wanawake wenye uzito kupita kiasi ikilinganishwa na wanawake wenye uzito mdogo.

Wanawake wana uwezekano mkubwa wa kutumia kiraka au pete kama ilivyoelekezwa ikilinganishwa na vidonge vya uzazi wa mpango vya kumeza, kwa sababu kipimo ni kila baada ya wiki 1 hadi 3 badala ya kila siku.

Kutokwa na damu kwa kasi si jambo linalotokea sana wakati kiraka au pete inatumiwa. Kutokwa na damu kusiko kwa kawaida kunakuwa jambo la kawaida zaidi kadiri wanawake wanavyozidi kutumia kiraka au pete za uzazi wa mpango.

Wanawake wenye hali fulani ambao hawapaswi kutumia tembe mchanganyiko za uzazi wa mpango pia hawapaswi kutumia viraka au pete za kutia ukeni za uzazi wa mpango.

Viraka vya Ngozi

Kiraka cha ngozi cha kuzuia mimba huunganishwa kwenye ngozi kwa gundi. Kinapaswa kuachwa mahali pake kwa wiki 1, kisha kuondolewa na kubadilishwa na kuwekwa kiraka kipya, ambacho huwekwa kwenye eneo tofauti la ngozi. Kiraka kipya huwekwa mara moja kwa wiki (siku ile ile kila wiki) kwa wiki 3, ikifuatiwa na wiki ambayo hakuna kiraka kinachotumika.

Ikiwa zaidi ya siku 2 zitapita bila kutumia kiraka, wanawake wanapaswa kutumia njia mbadala ya uzazi wa mpango kwa siku 7 pamoja na kiraka. Ikiwa siku 2 zitapita na wanawake wamefanya ngono bila kinga ndani ya siku 5 kabla ya siku hizo 2, wanaweza kuzingatia kutumia kingamimba ya dharura.

Mazoezi na matumizi ya sauna au mabeseni ya maji moto hayaondoi kiraka.

Kiraka kinaweza kisifanye kazi vizuri kwa wanawake wenye uzito wa zaidi ya pauni 198 au wenye kielezo cha uzito wa mwili (BMI) cha 30 au zaidi.

Kuvuja damu kati ya hedhi (kuvuja damu kwa kasi) si jambo la kawaida. Kutokwa na damu kusiko kawaida huwa jambo la kawaida zaidi kadiri wanawake wanavyozidi kutumia kiraka.

Ngozi iliyo chini na inayozunguka kiraka inaweza kuwasha.

Pete za kutia ukeni

Pete ya kutia ukeni ni kifaa kidogo kinachonyumbulika, laini, na chenye uwazi kinachowekwa ndani ya uke.

Aina mbili za pete zinapatikana:

  • Pete ambayo lazima ibadilishwe kila mwezi

  • Pete ambayo lazima ibadilishwe mara moja tu kwa mwaka

Aina zote mbili za pete kwa kawaida huachwa mahali pake kwa wiki 3, kisha huondolewa kwa wiki 1 ili kuruhusu hedhi kutokea. Pete ya mwaka mzima huondolewa, kutotumiwa kwa wiki 1, kisha pete hiyo hiyo huingizwa tena.

Mwanamke anaweza kuweka na kuondoa pete ya kutia ukeni yeye mwenyewe. Pete zote huwa za ukubwa sawa na zinaweza kuwekwa popote ukeni.

Huenda wanawake wakapendelea kuondoa pete ya kutia ukeni wakati mwingine tofauti na baada ya wiki 3. Hata hivyo, ikiwa pete itaondolewa kwa zaidi ya saa 3, wanawake wanapaswa kutumia njia mbadala ya uzazi wa mpango kwa siku 7 pamoja na pete.

Kwa kawaida, mwenzi wa mwanamke hawezi kuhisi pete ya kutia ukeni wakati wa tendo la ndoa. Pete haiyeyuki na haiwezi kusukumwa juu sana.

Athari Mbaya

Ikiwa wanawake wanatumia kiraka au pete kwa wiki 3 (kuibadilisha kila wiki), ikifuatiwa na wiki 1 ambapo kiraka au pete haitumiki, kwa kawaida huwa na hedhi ya kawaida. Kuvuja damu kati ya hedhi (kuvuja damu kwa kasi) si jambo la kawaida. Kutokwa na damu kusiko kawaida huwa jambo la kawaida zaidi kadiri wanawake wanavyozidi kutumia pete.

Madhara, athari kwenye hatari ya kupata matatizo, na vikwazo vya matumizi ni sawa na zile za tembe mchanganyiko za uzazi wa mpango.

Vipandikizi vya kupanga uzazi

Kipandikizi cha uzazi wa mpango ni kijiti kimoja chenye ukubwa wa njiti la kiberiti chenye projestini. Kipandikizi hicho hutoa projestini polepole kwenye damu. Aina ya kipandikizi kinachopatikana Marekani kinafaa kwa miaka 3 na pengine hadi miaka 5. Vipandikizi vingine vya uzazi wa mpango vinapatikana kwingineko duniani.

Asilimia ndogo sana (asilimia 0.05) ya wanawake hupata mimba katika kipindi cha mwaka wa kwanza wa matumizi.

Baada ya ngozi kuwekewa ganzi, daktari anatumia kifaa kinachofanana na sindano (trocar) kuweka kipandikizi chini ya ngozi ya sehemu ya ndani ya mkono juu ya kiwiko. Hakuna haja ya kuchana au kushona. Madaktari lazima wapate mafunzo maalum kabla ya kufanya kazi hii.

Endapo wanawake hawajafanya ngono bila kinga tangu hedhi yao ya mwisho, kipandikizi kinaweza kuwekwa wakati wowote wakati wa mzunguko wa hedhi. Endapo wanawake wamefanya ngono bila kinga, wanapaswa kutumia aina nyingine ya uzazi wa mpango hadi hedhi yao inayofuata itakapotokea au hadi kipimo cha ujauzito kitakapofanyika na kuthibitisha kuwa ujauzito haupo. Ikiwa wanawake si wajawazito, kipandikizi kinaweza kuwekwa. Kipandikizi kinaweza pia kuwekwa mara tu baada ya kuharibika mimba, kutoa mimba, au kujifungua mtoto.

Ikiwa kipandikizi hakitaingizwa ndani ya siku 5 baada ya mwanamke kuanza hedhi, anapaswa kutumia njia mbadala ya uzazi wa mpango kwa siku 7 pamoja na kipandikizi.

Madhara yanayofahamika sana ni vipindi visivyo vya kawaida vya hedhi au kutokuwepo kwa hedhi na maumivu ya kichwa. Madhara haya husababisha baadhi ya wanawake waondolewe kipandikizi. Kwa sababu kipandikizi hakiyeyuki mwilini, daktari lazima achane kwenye ngozi ili kukiondoa. Kuondoa ni vigumu zaidi kuliko kuingiza kwa sababu tishu zilizo chini ya ngozi hutanuka kwenye sehemu iliyowekwa kipandikizi.

Mara tu kipandikizi kinapoondolewa, ovari hurudi katika utendakazi wake wa kawaida, na wanawake wanapata uwezo wa kupata mimba tena.

Sindano za Kupanga Uzazi

Sindano mbalimbali za projestini za uzazi wa mpango zinapatikana duniani kote.

Depot medroxyprogesterone acetate (DMPA) inapatikana Marekani na hudungwa na mtaalamu wa afya mara moja kila baada ya miezi 3 kwenye msuli wa mkono au matako au chini ya ngozi.

Sindano za DMPA zina ufanisi sana. Endapo wanawake watapata sindano kama ilivyoelekezwa, ni takriban asilimia 0.2 tu kati yao hupata mimba katika kipindi cha mwaka wa kwanza wa matumizi. Kwa matumizi ya kawaida (jinsi watu wengi wanavyotumia, pamoja na uchelewaji kati ya sindano), karibu asilimia 6 hupata mimba.

Sindano inaweza kutolewa mara tu baada ya kuharibika kwa mimba, kutoa mimba, au kujifungua mtoto. Ikiwa muda kati ya sindano ni zaidi ya miezi 4, kipimo cha ujauzito kinafanywa ili kuthibitisha kuwa hakuna mimba kabla ya sindano kutolewa. Endapo wanawake hawatapata sindano ya kwanza ndani ya siku 5 hadi 7 baada ya hedhi kuanza, lazima watumie njia mbadala ya uzazi wa mpango kwa siku 7 baada ya kupata sindano.

Noristerat (NET-EN), ambayo inapatikana katika nchi nyingi lakini si Marekani, ni njia ya uzazi wa mpango inayofanya kazi kwa muda mrefu. Viwango vya kupata ujauzito ni sawa na vya DMPA. NET-EN inaweza kutolewa kama sindano ndani kabisa ya misuli ya matako, kwa kawaida kila baada ya wiki 8, lakini muda unaweza kuongezwa hadi wiki 12 baada ya miezi 6 ya kwanza ya matumizi. Endapo muda kati ya sindano ni zaidi ya wiki 13, kipimo cha ujauzito kinafanywa ili kuthibitisha kuwa hakuna mimba kabla ya sindano kutolewa. Kama ilivyo DMPA, endapo wanawake hawatapata sindano ya kwanza ndani ya siku 5 hadi 7 baada ya hedhi kuanza, lazima watumie njia mbadala ya uzazi wa mpango kwa siku 7 baada ya kupata sindano. Na kama DMPA, NET-EN inaweza pia kutolewa mara tu baada ya kuharibika mimba, kutoa mimba, au kujifungua mtoto.

Athari Mbaya

Projestini huvuruga kabisa mzunguko wa hedhi. Takriban theluthi moja ya wanawake wanaotumia njia hii ya uzazi wa mpango hawapati hedhi katika kipindi cha miezi 3 baada ya sindano ya kwanza, na theluthi nyingine hupata hali ya kutokwa na damu na madoa ya damu yasiyo ya kawaida kwa zaidi ya siku 11 kila mwezi. Baada ya njia hii ya uzazi wa mpango kutumika kwa muda, kutokwa na damu isivyo kawaida hutokea mara chache. Baada ya miaka 2, takriban asilimia 70 ya wanawake hawatoi damu kabisa. Sindano zinapositishwa, mzunguko wa kawaida wa hedhi huanza tena kwa karibu nusu ya wanawake ndani ya miezi 6 na karibu robo tatu ndani ya mwaka 1. Uwezo wa kupata mimba unaweza usirudi kwa hadi miezi 18 baada ya sindano kusimamishwa. Kwa wanawake wanaotumia NET-EN, hali ya kutoa mayai hurejea kwa kasi zaidi, kwa wastani wa miezi 3, na kurudi kwenye uwezo wa kushika mimba ndani ya miezi 6. 

Kwa kawaida wanawake huongezeka uzito wa pauni 3 hadi 9 wakati wa mwaka wa kwanza wa matumizi na huzidi kuongezeka uzito. Kuongezeka uzito huenda kunatokana na mabadiliko ya hamu ya kula. Kwa hivyo ili kuzuia ongezeko hili, wanawake wanahitaji kupunguza kalori na kuongeza kiwango cha kufanya mazoezi.

DMPA haionekani kuzidisha mfadhaiko kwa wanawake walio na mfadhaiko kabla ya kuanza kutumia dawa hii. Baadhi ya tafiti zimeripoti hatari iliyoongezeka ya mfadhaiko baada ya ujauzito (mfadhaiko baada ya kujifungua) kwa watumiaji wa NET-EN.

Maumivu ya kichwa yanatokea sana, lakini kwa kawaida hupungua baada ya muda. Endapo wanawake wamewahi kuwa na maumivu ya kichwa yanayovuta au kipandauso hapo awali, sindano hazizidishi maumivu hayo.

Uzito wa mifupa hupungua kwa muda. Hata hivyo, hatari ya kuvunjika kwa mifupa haiongezeki, na mifupa kwa kawaida hurudi kwenye uzito wake wa awali baada ya sindano kusitishwa. Kushiriki katika shughuli za kimwili na mazoezi ya kunyanyua vitu vizito, na kupata kalsiamu na vitamini D ya kutosha kila siku ili kusaidia kudumisha uzito wa mifupa ni muhimu kwa wanawake wote, lakini ni muhimu hasa kwa vijana na wanawake vijana wanaopata sindano za projestini. Vijalizo vya kalsiamu na vitamini D mara nyingi huhitajika ili kupata kiasi kinachohitajika.

Kwa baadhi ya wanawake, DMPA huongeza viwango vya triglycerides na lehemu ya lipoproteini ya uzito mdogo (LDL). Hata hivyo, athari hii inaonekana kuwa ya muda mfupi na hali inakuwa nzuri ndani ya miezi 36 ya matumizi ya DMPA. Athari kama hiyo ingetarajiwa kwa kutumia NET-EN.

Manufaa

DMPA haiongezi hatari ya kupata saratani ya matiti, ovari, au shingo ya kizazi.

Sindano za uzazi wa mpango zinaweza kupunguza hatari ya kupata

Mwingiliano na dawa zingine si jambo linalotokea.

Tofauti na tembe mchanganyiko za uzazi wa mpango, sindano za projestini hazionekani kuongeza hatari ya shinikizo la damu au kuganda kwa damu.

Sindano za uzazi wa mpango kwa sasa zinachukuliwa kuwa salama kwa wanawake ambao hawapaswi kutumia estrojeni na inaweza kuwa chaguo zuri kwa wanawake walio na ugonjwa wa kifafa.