Ujana ni kipindi cha kuanzia utoto hadi utu uzima. Ingawa vijana wengi waliobalehe wana afya njema kimwili na kiakili, ujana ni wakati ambapo changamoto au masuala yanaweza kutokea. Ili kuwaweka vijana waliobalahe katika hali nzuri ya afya na kutambua na kutibu matatizo wanayokumbana nayo, vijana waliobalehe wanapaswa kupokea usaidizi na mwongozo kutoka kwa wazazi (au walezi) na huduma ya afya ya kinga ya mara kwa mara.
Mambo ya kawaida ya kuzingatia kuhusu afya na ukuaji kwa vijana waliobalehe yanahusisha ukuaji wa kimwili na maendeleo ya kisaikolojia. Masuala yanayohusiana yanaweza kuhusisha yafuatayo:
Maendeleo ya utambuzi, hisia na kijamii, pamoja na maendeleo ya kujitegemea (uhuru)
Masuala ya kimatibabu kama vile unene kupita kiasi, magonjwa ya utotoni yanayoendelea au kukua wakati wa kubalehe, na majeraha
Matatizo ya Kawaida ya Afya kwa Balehe
Majeraha yasiyo ya kukusudia yanayotokana na silaha za moto, ajali za magari, na kutumia dawa kupita kiasi ndizo sababu kuu za vifo na majeraha ya muda au ya kudumu miongoni mwa vijana waliobalehe nchini Marekani.
Majeraha ya kukusudia yanayotokana na, kwa mfano, mauaji au kujiua, pia ni kawaida sana miongoni mwa vijana waliobalehe.
Majeraha ya kimwili, kama vilemajeraha ya ubongo kutokana na kupigwa, au jeraha la ubongo linalotokana na jeraha la kichwa, ni ya kawaida, hasa miongoni mwa wanariadha (angalia pia Majeraha ya Ubongo Yanayohusiana na Spoti). Vijana wanaopata jeraha la kichwa wanapaswa kupimwa na mtaalamu mwenye uzoefu katika tathmini na matibabu ya aina hii ya jeraha. Baada ya jeraha la ubongo kutokana na kupigwa, vijana waliobalehe wanapaswa kupewa muda wa kupona kabla ya kurudi kwenye shughuli za kawaida, ikiwa ni pamoja na matumizi ya vifaa vya kielektroniki, kazi za shule na spoti. Kurejea kwenye shughuli hizi kunapaswa kusimamiwa na mtu mzima mwenye ujuzi.
Matumizi ya vilevi pia ni jambo muhimu la kiafya. Uchunguzi na utambuzi wa mapema ni njia muhimu za kuepuka matatizo makubwa na matokeo ya kudumu.
Matatizo ya afya ya akili, kwa mfano, mfadhaikomatatizo ya wasiwasi na matatizo mengine (kama vile skizofrenia), yanaweza kutokea au kudhihirika wakati wa kubalehe. Zaidi ya hayo, janga la COVID-19 liliathiri sana afya ya akili ya vijana wengi waliobalehe.
Masuala yanayohusiana na afya ya ngono na uzazi yamekuwa mada muhimu ya mazungumzo kadri vijana waliobalehe wanavyochunguza ngono na wanaweza kukabiliwa na matarajio au tabia za ngono kutoka kwa wenzao au wengine.
Mada maalum zinazoweza kuibuka ni pamoja na
Kukuza mahusiano bora ya karibu
Destruri za ngono salama
Maambukizi ya zinaa (STI)
Unyanyasaji wa kingono au aina nyingine za majeraha yanayohusiana na ngono
Ugunduzi wa utambulisho wa kijinsia pia inaweza kutokea wakati huu.
Unene kupita kiasi ni jambo la kawaida wakati wa kubalehe na mara nyingi huhusishwa na matatizo mengine yanayotokea kwa wakati mmoja, ikiwa ni pamoja na kisukari, shinikizo la juu la damu, na viwango vya juu vya mafuta katika damu. Pia, vijana wengi waliobalehe wanaishi kwa muda mrefu zaidi baada ya kupona ugonjwa mbaya ulioanza utotoni.
Tabia nyingi zisizofaa zinazoanza wakati wa kubalehe, kama vile kula lishe duni, ukosefu wa mazoezi, na uvutaji sigara, zinaweza kusababisha matatizo ya kiafya ya papo hapo, matatizo ya muda mrefu, na afya mbaya baadaye maishani.
Nchini Marekani, takriban 40% ya vijana waliobalehe wanaishi na hali sugu ya kiafya kama vile pumu, kisukari au ugonjwa wa utumbo wenye uvimbe.
Saratani kwa watoto si jambo la kawaida, lakini aina zinazotokea mara nyingi kwa vijana waliobalehe ni pamoja na leukemia, limfoma, saratani ya mifupa, rhabdomyosarcoma, saratani ya kikoromeo na uvimbe wa ubongo na uti wa mgongo.