Maumivu ya Fupanyonga Wakati wa Ujauzito wa Mapema

NaEmily E. Bunce, MD, Wake Forest School of Medicine;
Robert P. Heine, MD, Wake Forest School of Medicine
Imekaguliwa naSusan L. Hendrix, DO, Michigan State University College of Osteopathic Medicine
Imepitiwa/Imerekebishwa Jul 2023 | Imebadilishwa Feb 2024
v1536152_sw

Mwanzoni mwa ujauzito, wanawake wengi hupata maumivu ya fupanyonga. Maumivu ya fupanyonga hurejelea maumivu katika sehemu ya chini kabisa ya tumbo (nyonga). Maumivu katika sehemu ya kati au ya juu ya fumbatio, katika eneo la tumbo na utumbo, huitwa maumivu ya tumbo. Hata hivyo, wakati mwingine wanawake hupata tatizo kutambua iwapo maumivu hayo yapo hasa tumboni au kwenye fupanyonga. Visababishi vya maumivu ya tumbo wakati wa ujauzito viinaweza kuwa vinahusiana au havihusiani na ujauzito.

Maumivu ya fupanyonga wakati wa ujauzito yanaweza kuhusishwa na mabadiliko ya kawaida ya ujauzito au yanaweza kuwa ishara ya tatizo. Inaweza kutokea kwa kawaida mifupa na mishipa inapobadilika na kunyooshwa ili kijusi kipate nafasi. Maumivu ya kawaida yanaweza kuwa makali au yenye ukakamavu (kama vile maumivu ya hedhi) na yanaweza kutokea na kutoweka. Kwa kawaida, maumivu ya fupanyonga ambayo si makali au yanayoendelea si sababu ya kuwa na wasiwasi.

Maumivu ambayo yanasababishwa na matatizo ya ujauzito yanaweza kuambatana na dalili zingine, ikiwa ni pamoja na kutokwa na damu ukeni. Wanawake wanapaswa kuwasiliana na daktari wao iwapo wana uvujaji damu wowote wakati wa ujauzito. Katika baadhi ya matatizo, uvujaji damu kama huo unaweza kuwa mkali, wakati mwingine kusababisha shinikizo la damu kuwa chini sana (mshtuko). Maumivu makali, yanayoendelea, au katika tumbo ya kati au ya juu yanaweza kusababishwa na matatizo ya ujauzito au ugonjwa mwingine na pia ni sababu ya kuwasiliana na daktari.

Sababu za Maumivu ya Fupanyonga Wakati wa Ujauzito wa Mapema

Wakati wa ujauzito, maumivu ya fupanyonga yanaweza kusababishwa na matatizo yanayohusiana na

  • Ujauzito

  • Mfumo wa uzazi wa kike lakini si mimba

  • Viungo vingine, hasa njia ya kusaga chakula na njia ya mkojo

Wakati mwingine hakuna sababu maalum inayotambuliwa.

Visababishi vya kawaida zaidi vya maumivu ya fupanyonga vinavyohusiana na ujauzito wa mapema ni

  • Mabadiliko ya kawaida ya ujauzito

  • Kuharibika kwa mimba (mimba kutoka ghafla)

  • Mimba ya nje ya uterasi(ujauzito unaopandikizwa nje ya uterasi, kwa mfano, kwenye mrija wa falopio)— kisababishi kikuu zaidi cha maumivu ya nyonga wakati wa ujauzito wa mapema

Ujauzito wa nje ya kizazi ni wa kutishia maisha. Mimba iliyopandikizwa nje ya uterasi haitakua kwa njia ya kawaida. Kadri mimba inavyokua kwenye mrija wa falopio au sehemu nyingine ya mwili (kama vile ovari, seviksi, au tumbo), inaweza kusababisha sehemu hiyo kupasuka. Hii husababisha maumivu makali na kuvuja damu nyingi, ambayo inaweza kusababisha madhara makubwa au hata kifo kwa mwanamke mjamzito. Wakati ujauzito wa nje ya kizazi inapogunduliwa, matibabu ni kumaliza ujauzito kwa dawa au kuiondoa kwa upasuaji.

Maumivu ya fupanyonga yanaweza pia kutokea ovari inaposokotana na ligamenti na tishu zinazoishikilia, huku ikikatiza usambazaji wa damu kwa ovari. Ugonjwa huu, unaoitwa adnexal torsion, haihusiani na ujauzito lakini ni kawaida zaidi wakati wa ujauzito. Wakati wa ujauzito, ukubwa wa ovari huongezeka, na kufanya ovari iwe rahisi zaidi kusokotana.

Visababishi vya kawaida vya maumivu ya nyonga kwa ujumla, ambavyo pia ni visababishi vya kawaida wakati wa ujauzito, ni matatizo ya utumbo na njia ya mkojo, ikiwa ni pamoja na yafuatayo:

Maambukizi ya njia ya mkojo hutokea mara nyingi zaidi wakati wa ujauzito na kuna hatari kubwa ya maambukizi kuenea kutoka kibofu hadi kwenye figo na kuwa maambukizi hatari zaidi.

Viashiria vya hatari

Sifa mbalimbali (viashiria vya hatari) huongeza hatari ya baadhi ya matatizo yanayohusiana na ujauzito ambayo husababisha maumivu ya fupanyonga.

Kwa kuharibika mimba, sababu za hatari ni pamoja na zifuatazo:

  • Umri wa zaidi ya miaka 35

  • Kuharibika mimba mara moja au zaidi katika mimba zilizopita

  • Uvutaji sigara

  • Matumizi ya dawa za kulevya haramu, kama vile kokeini, au kwa uwezekano wa mihadarati mingine, kama vile pombe

  • Matatizo katika uterasi, kama vile fibroma (fibroid), kovu, au umbo lisilo la kawaida la uterasi

Kwa mimba ya nje ya uterasi, viashiria vya hatari ni pamoja na vifuatavyo:

  • Ujauzito wa nje ya kizazi wa awali (hali ya hatari ile muhimu zaidi)

  • Upasuaji wa awali wa tumbo, hasa upasuaji wa kuzuia kushika mimba wa kudumu (kufunga mirija ya uzazi)

  • Matatizo ya mirija ya falopio (kwa mfano, mirija ya falopio iliyovimba, inayoitwa hydrosalpinx)

  • Matumizi ya sasa ya intrauterine device (IUD)

  • Matumizi ya mbinu za uzazi zilizosaidiwa (utungishaji mimba kwenye maabara) ili kupata mimba ya sasa

Sababu zingine hatari kwa mimba ya nje ya uterasi ni pamoja na historia ya maambukizi ya ngono au ugonjwa wa kuchochewa kwa fupanyonga, matumizi ya sasa ya vidonge vya kupanga uzazi vya estrojeni/projestini, uvutaji sigara, utasa, kuharibika kwa mimba kwa awali au kutoa mimba kimakusudi (kutoa mimba kwa hiari).

Tathimini ya Maumivu ya Fupanyonga Wakati wa Ujauzito wa Mapema

Ikiwa mwanamke mjamzito ana maumivu ya fupanyonga au tumbo, daktari atatathmini iwapo hii inasababishwa na mabadiliko ya kawaida ya ujauzito au iwapo kuna shida. Ikiwa kuna maumivu ya ghafla na makali sana kwenye tumbo la chini au fupanyonga, madaktari lazima wajaribu haraka kubaini ikiwa upasuaji wa haraka unahitajika—kama ilivyo wakati kisababishi ni mimba iliyopasuka nje ya uterasi au ugonjwa wa kidole tumbo.

Ishara za onyo

Kwa wanawake wajawazito wenye maumivu ya fupanyonga, dalili zifuatazo husababisha wasiwasi:

  • Kuvuja damu ukeni

  • Homa na baridi, hasa ikiwa inaambatana na maumivu ya kukojoa, maumivu ya mgongo wa juu (ubavuni), au kutokwa na uchafu ukeni ulio na usaha

  • Maumivu makali na yanayozidi kuwa mabaya wakati wa mwendo

  • Kuzimia, kizunguzungu, au mapigo ya moyo ya haraka—dalili zinazoashiria shinikizo la chini sana la damu

Wakati wa kuona daktari

Wanawake wenye dalili za hatari wanapaswa kumuona daktari mara moja.

Wanawake wasio na dalili za hatari wanapaswa kujaribu kumuona daktari ndani ya siku moja au zaidi ikiwa wana maumivu au kuwashwa wakati wa kukojoa au maumivu yanayotatiza shughuli za kila siku. Wanawake wenye usumbufu mdogo tu na wasio na dalili nyingine wanapaswa kuwasiliana na daktari. Daktari anaweza kuwasaidia kuamua ikiwa wanahitaji kuonekana na kwa haraka kiasi gani.

Anachofanya daktari

Ili kubaini iwapo upasuaji wa dharura unahitajika, madaktari kwanza huchunguza shinikizo la damu na halijoto ya mwanamke na kuuliza kuhusu dalili kuu, kama vile kutokwa na damu ukeni. Kisha madaktari huuliza kuhusu dalili zingine na historia ya kimatibabu. Pia hufanya uchunguzi wa kimwili. Kile wanachopata wakati wa historia na uchunguzi wa kimwili mara nyingi huonyesha kisababishi na vipimo vinavyoweza kuhitajika (tazama jedwali ).

Madaktari wanauliza kuhusu maumivu:

  • Iwapo maumivu yanaanza ghafla au polepole

  • Ikiwa yatokea katika eneo maalum au yameenea zaidi

  • Ikiwa kusonga au kubadilisha mkao kunaongeza maumivu

  • Ikiwa maumivu ni ya mikakamao na ikiwa ni ya kudumu au inakuja na kutoweka

Madaktari pia huuliza yafuatayo:

  • Dalili zingine, kama vile kutokwa na damu ukeni, kutokwa na uchafu ukeni, haja ya kukojoa mara kwa mara au haraka, kutapika, kuhara, na kuvimbiwa

  • Matukio ya awali yanayohusiana na ujauzito (historia ya uzazi), ikiwa ni pamoja na mimba za awali, kuharibika kwa mimba, na utoaji mimba kimakusudi (utoaji mimba kwa hiari) kwa sababu za kimatibabu au nyinginezo

  • Viashiria vya hatari kwa kuharibika kwa mimba na mimba ya nje ya uterasi

Uchunguzi wa kimwili hulenga uchunguzi wa fupanyonga (uchunguzi wa viungo vya nje na vya ndani vya uzazi na wakati mwingine rektamu). Madaktari pia hufinya tumbo polepole ili kuona iwapo kuifinya kunasababisha maumivu yoyote.

Jedwali
Jedwali

Kupima

Kipimo cha ujauzito kwa kutumia sampuli ya mkojo kwa kawaida hufanywa. Ikiwa kipimo cha ujauzito kinaonyesha kuwa ni chanya, uchunguzi wa ultrasonografia wa fupanyonga hufanywa ili kuthibitisha kuwa ujauzito kwa kawaida upo kwenye uterasi badala ya mahali pengine (mimba ya nje ya uterasi). Kwa kipimo hiki, kifaa cha miale ya sauti (ultrasound) kinachoshikiliwa kwa mkono huwekwa kwenye tumbo, ndani ya uke, au kwenye sehemu zote mbili. Ikiwa mimba ni ya mapema sana, wakati mwingine haiwezekani kuthibitisha iwapo mimba iko kwenye uterasi.

Kwa kawaida vipimo vya damu hufanywa. Ikiwa mwanamke anatokwa na damu ukeni, upimaji kwa kawaida hujumuisha hesabu kamili ya seli za damu na aina ya damu pamoja na Hali ya Rh (chanya au hasi), ikiwa mwanamke atahitaji kuongezewa damu. Kujua hali ya Rh pia husaidia madaktari kuzuia matatizo katika ujauzito unaofuata.

Iwapo madaktari watashuku kuwa kuna mimba ya nje ya uterasi, upimaji pia hujumuisha kipimo cha kupima homoni inayotengenezwa na kondo la nyuma mapema wakati wa ujauzito (human chorionic gonadotropin, au hCG). Ikiwa dalili (kama vile shinikizo la chini sana la damu au mapigo ya moyo ya haraka) zinaonyesha kuwa mimba iliyotungwa nje ya uterasi inaweza kuwa imepasuka, vipimo vya damu hufanywa ili kubaini iwapo damu ya mwanamke inaweza kuganda kwa kawaida.

Daktari hufanya vipimo vingine kulingana na matatizo yanayoshukiwa kuwepo. Ultrasonografia ya Doppler (Doppler ultrasonography), ambayo huonyesha mwelekeo na kasi ya mtiririko wa damu, husaidia madaktari kutambua ovari iliyosokotana, ambayo inaweza kukatiza usambazaji wa damu kwenye ovari. Vipimo vingine vinaweza kujumuisha ukuzaji wa sampuli ya damu, mkojo, au uchafu kutoka ukeni na vipimo vya mkojo (uchanganuzi wa mkojo) ili kuchunguza maambukizi.

Ikiwa maumivu yanaendelea kuwa magumu na chanzo hakijulikani, madaktari hufanya mkato mdogo chini ya kitovu na kuingiza mrija wa kutazama (laparoskopu) ili kuona moja kwa moja uterasi, mirija ya falopio, na ovari ili kutathmini zaidi chanzo cha maumivu. Mara chache, upasuaji mkubwa zaidi (utaratibu unaoitwa laparatomi) unahitajika.

Matibabu ya Maumivu ya Fupanyonga Wakati wa Ujauzito wa Mapema

Matatizo maalum hutibiwa, kama ilivyo katika mifano ifuatayo:

  • Ujauzito wa nje ya uterasi: Dawa ya kuzuia ukuaji wa mimba ya nje ya kizazi au upasuaji wa kuiondoa

  • Kuharibika kwa mimba: Dawa za kupunguza maumivu, dawa ya kusaidia ujauzito kupita, au utaratibu wa kupanua na kupunguza maumivu (D & C) ili kuondoa tishu za ujauzito

  • Utoaji mimba wa septiki (maambukizi ya yaliyomo kwenye uterasi kabla, wakati, au baada ya kuharibika kwa mimba): Antibiotiki hutolewa kwa njia ya mishipa na D & C ili kuondoa vitu vilivyo kwenye uterasi haraka iwezekanavyo

  • Msokoto wa Adnexal (Adnexal torsion) (ovari au mirija wa falopio uliojikunja): Upasuaji wa kufungua (ikiwezekana) au kuondoa ovari au mrija

Ikiwa dawa za kupunguza maumivu zinahitajika, acetaminophen ndiyo salama zaidi kwa wanawake wajawazito, lakini ikiwa haifanyi kazi, opioid inaweza kuhitajika.

Maumivu kutokana na mabadiliko ya kawaida wakati wa ujauzito

Ili kusaidia kuepuka au kupunguza aina fulani za maumivu wakati wa ujauzito, huenda wanawake wakashauriwa

  • Kuwa na utaratibu wa mazoezi ya viungo pamoja na mazoezi ambayo ni salama wakati wa ujauzito

  • Kujiepusha na kuinua au kusukuma vitu vizito

  • Kudumisha mkao mzuri

  • Kulala na mto kati ya magoti yao

  • Kupumzika inapohitajika

  • Kuvaa nguo zenye mpira unaoshikilia mgongo au tumbo

  • Mwone mtaalamu wa tiba ya mazoezi mwenye utaalamu kuhusu ujauzito

  • Labda jaribu tiba ya sindano (acupuncture)

Mambo Muhimu

  • Maumivu ya fupanyonga wakati wa ujauzito wa mapema kwa kawaida hutokana na mabadiliko yanayotokea kawaida wakati wa ujauzito.

  • Wakati mwingine hutokana na matatizo yanayohusiana na ujauzito au yanayohusiana na viungo vya uzazi vya kike lakini si ujauzito, au viungo vingine.

  • Kipaumbele cha kwanza kwa madaktari ni kutambua matatizo yanayohitaji upasuaji wa dharura, kama vile mimba iliyo nje ya uterasi au ugonjwa wa kidole tumbo.

  • Ultrasonografia kwa kawaida hufanywa.

  • Hatua za jumla (kama vile kupumzika na kushinikiza joto) zinaweza kusaidia kupunguza maumivu kutokana na mabadiliko ya kawaida wakati wa ujauzito.