Mimbo ngumu kwa Watoto

NaDeborah M. Consolini, MD, Thomas Jefferson University Hospital
Imekaguliwa naAlicia R. Pekarsky, MD, State University of New York Upstate Medical University, Upstate Golisano Children's Hospital
Imepitiwa/Imerekebishwa Mar 2025 | Imebadilishwa Oct 2025
v820180_sw

Kufunga choo ni kuchelewa au ugumu wa kutoa kinyesi. Kinyesi ni kigumu na wakati mwingine kikubwa kuliko kawaida na hali hii inaweza kusababisha maumivu. Kufunga choo ni jambo la kawaida sana miongoni mwa watoto. Kunachangia hadi 5% ya ziara za watoto kwa daktari.

Marudio na uthabiti wa haja kubwa (BMs) hutofautiana katika utoto wote, na hakuna ufafanuzi mmoja wa kile kilicho cha kawaida. Watoto wachanga kwa kawaida hupata haja kubwa mara 4 au zaidi kwa siku. Katika mwaka wa kwanza, watoto wachanga hupata BM 2 hadi 4 kwa siku. Watoto wachanga wanaonyonyeshwa kwa kawaida huwa na BM nyingi zaidi kuliko watoto wanaonyonyeshwa kwa fomyula na wanaweza kupata moja baada ya kila unyonyeshaji. Kinyesi cha watoto wachanga wanaonyonyeshwa ni legelege, cha manjano, na chenye mbegu. Baada ya mwezi mmoja au miwili, baadhi ya watoto wachanga wanaonyonyeshwa hupata BM mara chache, lakini kinyesi hubaki laini au legevu. Baada ya umri wa mwaka 1, watoto wengi huwa na haja kubwa moja au mbili laini lakini kinyesi yenye umbo kwa siku. Hata hivyo, baadhi ya watoto wachanga na watoto wadogo kwa kawaida hupata BM mara moja tu kila baada ya siku 3 hadi 4.

Watoto wanaweza kuwa na hali ya kufunga choo ikiwa wana mojawapo ya yafuatayo:

  • Hakuna BM kwa siku 2 au 3 zaidi kuliko kawaida

  • BM ngumu au yenye chungu

  • Kinyesi kikubwa ambacho kinaweza kuziba choo

  • Matone ya damu nje ya kinyesi

Kwa watoto wachanga, dalili za juhudi kama vile kujikaza na kulia kabla ya kufanikiwa kutoa kinyesi laini kwa kawaida hazionyeshi kufunga choo. Dalili hizi kwa kawaida hutokea kwa sababu watoto wachanga hukua polepole misuli inayohitajika kusaidia BM.

Mara nyingi wazazi huwa na wasiwasi kuhusu BM ya watoto wao, lakini kufunga choo kwa kawaida hakuna madhara makubwa. Baadhi ya watoto wenye kufunga choo huwa na dalili za maumivu ya tumbo mara kwa mara, hasa baada ya kula. Mara kwa mara, kutoa kinyesi kikubwa na kigumu kunaweza kusababisha kuchanika kidogo kwenye tundu la haja kubwa (mpasuko wa tundu la haja kubwa). Mipasuko ya tundu la haja kubwa ni vyenye uchungu na inaweza kusababisha michirizi ya damu nyekundu angavu nje ya kinyesi au kwenye karatasi laini ya chooni. Mara chache, hali sugu ya kufunga choo kunaweza kuchangia matatizo ya mkojo kama vile maambukizi ya njia ya mkojo na kukojoa kitandani.

(Tazama pia Kufunga choo kwa watu wazima.)

Sababu za Kufunga Choo kwa Watoto

Sababu za kawaida

Watoto wachanga na watoto huwa na uwezekano mkubwa wa kufunga choo mara 3 kwa vipindi vifuatavyo:

Katika 95% ya watoto, kufunga choo husababishwa na

  • Matatizo ya lishe

  • Matatizo ya kitabia

Kufunga choo kunakosababishwa na matatizo ya lishe au kitabia huitwa kufunga choo kwa utendaji kazi.

Masuala ya lishe yanayosababisha kufunga choo ni pamoja na lishe yenye kiwango kidogo cha majimaji na/au nyuzinyuzi (nyuzinyuzi zipo katika matunda, mboga, na nafaka nzima).

Masuala ya kitabia ambayo yanaweza kuhusishwa na kufunga choo ni pamoja na msongo wa mawazo (kama inavyoweza kuhisiwa wakati ndugu anapozaliwa), upinzani dhidi ya mafunzo ya kutumia choo, na hamu ya kudhibiti. Pia, watoto wanaweza kuahirisha kimakusudi kuwa na BMs (inaitwa kuzuia kinyesi) kwa sababu wana mpasuko unaouma kwenye tundu la haja kubwa au kwa sababu hawataki kuacha kucheza. Unyanyasaji wa kingono unaweza kusababisha msongo wa mawazo au jeraha linalosababisha watoto kuzuia kinyesi.

Ikiwa watoto hawaendi choo wakati wanapohisi hamu asilia ya kufanya hivyo, rektamu hatimaye huvutika ili iweze kutosha kinyesi kilichopo. Pale rektamu inapovutika, hamu ya kwenda choo hupungua, na kinyesi zaidi na zaidi hujikusanya na kuwa kigumu. Mzunguko mbaya wa kufunga choo unaozidi kuwa mbaya unaweza kutokea. Ikiwa kinyesi kilichokusanyika kinakuwa kigumu, wakati mwingine huzuia kupita kwa kinyesi kingine—hali inayoitwa usonganishaji wa kinyesi. Kinyesi laini kilicho juu ya kinyesi kigumu kinaweza kuvuja karibu na mgongano huo kwenye chupi ya mtoto na kusababisha hali ya kushindwa kuzuia kinyesi (encopresis). Wazazi wanaweza kufikiria kwamba mtoto anahara wakati tatizo halisi ni kufunga choo.

Sababu zisizo za kawaida

Katika takriban 5% ya watoto, hali ya kufunga choo husababishwa na tatizo la kimwili, dawa, au sumu. Matatizo yanaweza kuwepo wakati wa kuzaliwa au kutokea baadaye. Kufunga choo kunakosababishwa na maradhi, dawa, au sumu huitwa hali ya kufunga choo ya kimaumbile na kunahitaji kuchunguzwa na daktari.

Kwa watoto waliozaliwa hivi karibuni na watoto wachanga, matatizo yanayosababisha hali ya kufunga choo ya kimaumbile ni

Sababu zingine za hali ya kufunga choo ya kimaumbile ni pamoja na

Watoto wenye matatizo makubwa ya tumbo (kama vile ugonjwa wa kidole tumbo au kizuizi kwenye utumbo) mara nyingi hawana BM. Hata hivyo, watoto hawa kwa kawaida huwa na dalili zingine zinazoonekana zaidi, kama vile maumivu ya tumbo, uvimbe wa tumbo, kutapika, au mchanganyiko. Dalili hizi kwa kawaida huwafanya wazazi kutafuta huduma ya matibabu kabla idadi ya BM haijapungua.

Tathimini ya Kifunga Choo kwa Watoto

Madaktari kwanza hujaribu kubaini kama kufunga choo kunatokana na matatizo ya lishe au ya kitabia (ya utendaji kazi) au yanatokana na maradhi, sumu, au dawa (ya kimaumbile).

Ishara za onyo

Dalili fulani ni chanzo cha wasiwasi na zinapaswa kukupa mashaka kuhusu sababu za kimaumbile za kufunga choo:

  • Kukosa choo (BMs) katika saa 24 hadi 48 za kwanza baada ya kuzaliwa

  • Kupungua uzito au ukuaji duni

  • Kupungua kwa hamu ya kula

  • Damu kwenye kinyesi

  • Homa

  • Kutapika

  • Kuvimba tumbo

  • Maumivu ya tumbo (kwa watoto wenye umri wa kutosha huzungumza kuhusu hali hii)

  • Kwa watoto wachanga, misuli hupungua (mtoto huonekana mdhaifu au asiye na nguvu) na uwezo mdogo wa kunyonya

  • Kwa watoto wakubwa, mkojo kutoka bila hiari (kushindwa kujizuia kukojoa), maumivu ya mgongo, udhaifu wa miguu, au matatizo ya kutembea

Wakati wa kuona daktari

Watoto wanapaswa kuchunguzwa na daktari mara moja ikiwa wana dalili zozote za tahadhari. Ikiwa hakuna ishara za tahadhari lakini mtoto anapata BM ngumu, kwa chungu au mara chache, daktari anapaswa kuitwa. Kulingana na dalili zingine za mtoto (ikiwa zipo), daktari anaweza kushauri kujaribu matibabu rahisi ya nyumbani au akaomba wazazi wamlete mtoto kwa uchunguzi.

Anachofanya daktari

Madaktari kwanza huuliza maswali kuhusu dalili za mtoto na historia ya matibabu. Kisha madaktari hufanya uchunguzi wa kimwili. Wanachokipata wakati wa historia na uchunguzi wa kimwili mara nyingi huonyesha kisababishi cha kufunga choo na vipimo vinavyoweza kuhitajika kufanywa (tazama jedwali ).

Madaktari huamua kama watoto waliozaliwa karibuni wamewahi kupata BM (BM ya kwanza inaitwa mekoni). Watoto waliozaliwa karibuni ambao hawajapata BM ndani ya saa 24 hadi 48 baada ya kuzaliwa wanapaswa kufanyiwa uchunguzi wa kina ili kuondoa uwezekano wa ugonjwa wa Hirschsprung, kasoro za tundu la haja kubwa na rektamu au tatizo lingine hatarishi.

Kwa watoto wachanga na wakubwa, madaktari huuliza kama kufunga choo kulianza baada ya tukio maalum, kama vile kutumia nafaka au vyakula vingine vigumu, kula asali (kwa watoto walio chini ya miezi 12), kuanza mazoezi ya choo au kuanza shule. Kwa makundi yote ya umri, madaktari huuliza kuhusu lishe na kuhusu matatizo, sumu, na dawa zinazoweza kusababisha kufunga choo.

Kwa uchunguzi wa kimwili, madaktari kwanza humtazama mtoto kwa ujumla kwa dalili za ugonjwa na hupima urefu na uzito ili kuangalia dalili za ukuaji uliochelewa. Kisha madaktari huzingatia tumbo, tundu la haja kubwa (ikiwa ni pamoja na uchunguzi wa rektamu kwa kutumia kidole kilichovalishwa glavu), na utendakazi wa neva (ambao unaweza kuathiri jinsi njia ya mmeng'enyo wa chakula inavyofanya kazi).

Kupima

Ikiwa chanzo cha kufunga choo kinaonekana kuwa ni utenda kazi, hakuna vipimo vinavyohitajika isipokuwa pale ambapo matibabu yatashindwa kuwasaidia watoto. Ikiwa matibabu hayasaidii au ikiwa madaktari wanashuku kuwa chanzo ni maradhi mengine, eksirei ya tumbo inaweza kuchukuliwa, na vipimo vya matatizo mengine hufanywa kulingana na matokeo ya uchunguzi.

Jedwali
Jedwali

Matibabu ya Kufunga Choo kwa Watoto

Matibabu ya kufunga choo hutegemea chanzo.

Kwa hali ya kufunga choo kimaumbile, chanzo cha tatizo, dawa au sumu hutibiwa, husitishwa au huondolewa.

Kwa hali ya kufunga choo kwa utendaji kazi, hatua zinajumuisha

  • Kubadilisha lishe

  • Kuboresha tabia

  • Wakati mwingine kutumia dawa za kulainisha kinyesi au dawa za kuharisha

Kubadilisha lishe

Mabadiliko ya lishe kwa watoto wachanga na watoto wakubwa ni pamoja na kuwapa wakia 1 hadi 4 (mililita 30 hadi 120 [mL]) za juisi ya plamu kavu, pea au tufaha kila siku.

Watoto wachanga na watoto wakubwa wanapaswa kunywa maji zaidi, kula matunda, mboga mboga zaidi, na nafaka zenye nyuzinyuzi nyingi, na kula vyakula vichache vinavyosababisha kufunga choo kama vile maziwa na jibini.

Kuboresha tabia

Marekebisho ya tabia yanaweza kuwasaidia watoto wakubwa. Hatua zinajumuisha

  • Kuwahimiza watoto waliofunzwa kutumia choo kukaa kwenye choo kwa dakika 5 hadi 10 baada ya kula na kuwapa zawadi wanapopiga hatua (kwa mfano, kuandika maendeleo kwenye chati ya ukutani)

  • Kuwapa watoto wanaofundishwa kutumia choo mapumziko ya mafunzo ya choo hadi pale hali ya kufunga choo itakapotoweka

Kuketi chooni baada ya kula kunaweza kusaidia kwa sababu kula chakula huchochea hisia ya BM. Mara nyingi, watoto hupuuza ishara kutoka kwa tendohiari hili na kuahirisha kuwa na BM. Mbinu hii hutumia tendohiari kusaidia kufunza upya njia ya mmeng'enyo wa chakula, kuanzisha utaratibu wa kutoa choo, na kuhimiza BM za kawaida zaidi.

Dawa za kulainisha kinyesi na kuchochea kuharisha

Ikiwa kufunga choo hakuondoki baada ya marekebisho ya kitabia na mabadiliko katika lishe, madaktari wanaweza kupendekeza dawa fulani zinazosaidia kulainisha kinyesi (vilainishi vya kinyesi) na/au kuongeza mwendo wa ghafla wa njia ya mmeng'enyo wa chakula (vilainishi). Dawa kama hizo ni pamoja na polyethilini glikoli, laktulosi, mafuta ya madini, maziwa ya magnesi (hidroksidi ya magnesi), senna na bisacodyl. Wakati mwingine, enema za chumvi pia hutumiwa. Dawa nyingi kati ya hizi zinapatikana bila kuagizwa na daktari Hata hivyo, dozi zinapaswa kutegemea umri na uzito wa mwili wa mtoto pamoja na ukali wa hali ya kufunga choo. Kwa hivyo, wazazi wanapaswa kushauriana na daktari kuhusu kipimo kinachofaa na idadi ya dozi kwa siku kabla ya kutumia matibabu haya. Lengo la matibabu ni kupitisha kinyesi laini mara 1 kwa siku.

Ikiwa watoto wana msongamano wa kinyesi, chaguzi ni pamoja na enema laini na ajenti (kama vile mafuta ya madini au polyethilini glikoli) inayomezwa na kiasi kikubwa cha majimaji. Ikiwa matibabu haya hayafanyi kazi, watoto wanaweza kuhitaji kulazwa hospitalini ili kuondoa msongamano.

Kwa kawaida watoto wachanga hawahitaji matibabu yoyote kati ya haya. Kwa kawaida, kidonge cha gliserini cha kutiwa tupuni kinatosha.

Ili kudumisha BM za kawaida, madaktari wanaweza kupendekeza kwamba watoto watumie virutubisho vya nyuzinyuzi (kama vile psyllium), ambavyo vinaweza kupatikana bila agizo la daktari. Ili virutubisho hivi viwe na ufanisi, watoto lazima wanywe wakia 32 hadi 64 (takriban lita 1 hadi 2) za maji kwa siku.

Mambo Muhimu

  • Kwa kawaida, kufunga choo husababishwa na matatizo ya kitabia au lishe (yanayoitwa kufunga choo kwa utendaji kazi).

  • Watoto wanapaswa kuchunguzwa na daktari ikiwa muda kati ya BM moja na nyingine umekuwa siku 2 au 3 zaidi ya kawaida, ikiwa kinyesi chao ni kigumu au kikubwa, ikiwa kinyesi husababisha maumivu au kutokwa na damu, au ikiwa wana dalili zingine.

  • Watoto waliozaliwa karibuni ambao hawajapata BM ndani ya saa 24 hadi 48 baada ya kuzaliwa wanapaswa kufanyiwa uchunguzi wa kina ili kuondoa uwezekano wa ugonjwa wa Hirschsprung, kasoro za tundu la haja kubwa na rektamu, au ugonjwa mwingine mbaya.

  • Kuongeza nyuzinyuzi kwenye lishe au marekebisho ya kitabia kunaweza kusaidia wakati matatizo ya lishe au kitabia ndiyo chanzo.