Tatizo la kupungua kwa ukuaji na uzani (zamani kulijulikana kama kushindwa kustawi) ni ukosefu wa ongezeko la uzani linalotarajiwa na ukuaji wa kimwili ambao unaweza kusababisha kuchelewa kwa ukuaji na kukomaa.
Magonjwa ya kiafya na ukosefu wa lishe bora ni sababu za kutokea kwa tatizo la kupungua kwa ukuaji na uzani.
Utambuzi huo unategemea tarakimu za chati ya ukuaji wa mtoto, uchunguzi wa kimwili, historia ya afya, na mazingira ya nyumbani.
Watoto ambao wana lishe duni wakati wa mwaka wa kwanza wa maisha wanaweza kuwa na ucheleweshaji wa ukuaji.
Matibabu yanajumuisha lishe bora na matibabu ya matatizo ya kiafya.
Katika mwaka wa kwanza wa maisha, uzani na urefu wa mtoto hurekodiwa kwenye chati katika kila ziara ya daktari ili kuhakikisha kwamba ukuaji unaendelea kwa kasi thabiti (tazama Ukuaji wa Kimwili wa Watoto Wachanga na Watoto). Asilimia ni njia ya kulinganisha watoto wachanga wa umri na jinsia sawa. Kwa mfano, kusema kwamba mtoto mchanga yuko katika asilimia 10 kwa uzani kunamaanisha kwamba kati ya watoto 100 wa umri na jinsia moja, karibu 90 wana uzani zaidi na karibu 10 wana uzani mdogo. Ingawa baadhi ya watoto wachanga ni wadogo na wengine ni wakubwa, watoto wachanga kwa kawaida hubaki katika kiwango sawa cha asilimia wanapokua.
Tatizo la kupungua kwa ukuaji na uzani linaozingatiwa kwa watoto ambao uzani au indeksi ya uzito wa mwili hupungua chini ya kipimo kinachotarajiwa au ambao kimo au urefu wao hushuka chini ya kipimo kinachotarajiwa ikilinganishwa na watoto wa rika na jinsia moja. Kupungua kwa uzani pia huzingatiwa kwa watoto wachanga ambao wana kupungua kwa kasi kwa asilimia ya uzani wao ingawa uzani wao halisi si mdogo. Kwa mfano, madaktari wangekuwa na wasiwasi kuhusu mtoto mchanga ambaye amepungua kutoka asilimia 90 hadi asilimia 50 (uzani wa wastani) katika kipindi kifupi.
Kuna sababu nyingi.
Visababishaji vya Kupungua kwa Ukuaji na Uzito kwa Watoto
Vyanzo vya tatizo la kupungua kwa ukuaji na uzani vinaweza kuhusisha
Mambo ya kimazingira na kijamii
Matatizo ya Kiafya
Sababu yoyote, lishe isiyotosha inaweza kuathiri ukuaji wa mwili na ubongo wa mtoto.
Mambo ya kimazingira na kijamii ndiyo sababu za kawaida kwa nini watoto hawapati lishe wanayohitaji. Tatizo la kupungua kwa ukuaji na uzani kwa sababu hizi hutokana na kutokula kalori za kutosha.
Mlezi kumtelekeza au kumnyanyasa, hali za afya ya akili ya wazazi (kama vile unyogovu), ukosefu wa uhakika wa kula chakula, na hali za kifamilia zenye migogoro yote huongeza hatari kwamba milo ya kawaida na yenye lishe haitatolewa. Hali kama hizo zenye mfadhaiko au mazingira yasiyochochea pia yanaweza kupunguza hamu ya mtoto na kupunguza ulaji wa chakula wa mtoto.
Wakati mwingine walezi hutoa chakula chenye thamani duni ya lishe, jambo ambalo linaweza kusababisha ulaji duni na kuongezeka uzani mdogo. Walezi wanaweza wasielewe kikamilifu mbinu za kulisha watoto wachanga na wanaweza kuandaa maziwa ya watoto ya kopo yasiyofaa, au mtoto anaweza kuwa na matatizo ya kulisha ambayo walezi hawawezi kuyashughulikia. Walezi wanapohitaji msaada katika ujuzi wa kulisha watoto wachanga na mtoto wao ana matatizo ya kulisha, ukuaji na uzani hupungua.
Mara chache, baadhi ya akina mama hawazalishi maziwa ya kutosha ya mama (maziwa ya mama) au, mara chache zaidi, hutoa maziwa yenye kalori chache.
Watoto wachanga na watoto ambao wana hali zenye mfadhaiko katika familia au wana uhusiano usiofaa na mlezi wanaweza kuwa na tatizo la kupungua kwa ukuaji na uzani kwa sababu mfadhaiko wanaouhisi unaweza kuwafanya watoe homoni zinazopunguza athari za homoni za ukuaji. Kupungua huku kwa homoni ya ukuaji kutokana na mfadhaiko kunaweza kusababisha ukuaji duni.
Matatizo ya kiafya wakati mwingine husababisha tatizo la kupungua kwa ukuaji na uzani. Matatizo ya kiafya, kama vile ugumu wa kutafuna au kumeza (kama vile mdomo wazi au kaakaa wazi), refluksi gastroesofajia, kupungua kwa ukubwa wa umio, au hali ya kushindwa kunyonya virutubishi kwa utumbo, kunaweza pia kuathiri uwezo wa mtoto kula, kuhifadhi, kufyonza au kusindika chakula. Matatizo ya kula yanaweza pia kusababisha tatizo la kupungua kwa ukuaji na uzani.
Maambukizi, uvimbe, matatizo ya homoni au umetaboli (kama vile kisukari au sisti fibrosisi), ugonjwa wa moyo, ugonjwa wa figo, ugonjwa wa ini, matatizo ya kijenetiki (kama vile ugonjwa wa Down au ugonjwa wa umetaboli wa kurithi), matatizo ya mmeng'enyo wa chakula (kama vile ugonjwa wa seliaki na ugonjwa wa uchochezi wa matumbo), kiwewe, na maambukizi ya virusi vya UKIMWI (VVU) ni sababu zingine za kimatibabu zinazosababisha tatizo la kupungua kwa ukuaji na uzani.
Kwa baadhi ya watoto, tatizo la kupungua kwa ukuaji na uzani husababishwa na mchanganyiko wa mambo ya kimazingira na kijamii na matatizo ya kiafya. Kwa mfano, watoto wenye matatizo ya kiafya wanaweza pia kuwa na mazingira ya nyumbani yenye mkfadhaiko au mahusiano yasiyofaa na walezi. Vilevile, watoto wenye tatizo la kupungua kwa ukuaji na uzani unaosababishwa na mambo ya kimazingira na kijamii wanaweza kupata matatizo ya kiafya.
Kutambua Tatizo la Kupungua kwa Ukuaji na Uzito kwa Watoto
Ufuatiliaji wa uzani na kimo au urefu
Maswali kuhusu ulishaji na historia ya kimatibabu, kijamii, na familia
Vipimo vya maabara ikiwa inahitajika
Madaktari huzingatia utambuzi wa tatizo la kupungua kwa ukuaji na kudumaa kwa uzani wakati uzani wa mtoto au indeksi ya uzito wa mwili (BMI) uko chini sana ya kile kinachopaswa kuwa ikilinganishwa na vipimo vya zamani au chati za kawaida za kimo na uzani (tazama Ukuaji wa Kimwili wa Watoto Wachanga na Watoto). Ikiwa tatizo la kupungua kwa ukuaji na uzani huathiri uzani wa mtoto mchanga vya kutosha, viwango vya ukuaji wa kimo na kichwa (ubongo) pia huathiriwa.
Ili kubaini ni kwa nini mtoto anaweza kuwa na tatizo la kupungua kwa ukuaji na uzani, madaktari huwauliza walezi maswali mahususi kuhusu
Kulisha (kwa watoto wachanga) na kula (kwa watoto wakubwa)
Tabia za kwenda choo
Utulivu wa kijamii, kihisia, makazi, na kifedha wa familia, ambao unaweza kuathiri upatikanaji wa chakula kwa mtoto.
Magonjwa ambayo mtoto ako nayo, amekuwa nayo, au ambayo yanatokea katika familia
Daktari anamchunguza mtoto, akitafuta dalili za hali zinazoweza kuelezea uzani mdogo wa mtoto au ukuaji uliopungua. Daktari hufanya maamuzi kuhusu kufanya vipimo vya damu, kinyesi, na mkojo na eksirei kulingana na tathmini hii. Upimaji wa kina zaidi hufanywa ikiwa daktari anashuku kuwa kuna ugonjwa wa msingi.
Matibabu ya Tatizo la Kupungua kwa Ukuaji na Uzito kwa Watoto
Milo au vyakula vyenye lishe
Matibabu maalum kwa matatizo ya kiafya
Matibabu ya tatizo la kupungua kwa ukuaji na uzani hutegemea chanzo. Ikiwa ugonjwa wa kiafya utagunduliwa, matibabu maalum ya ugonjwa huo hutolewa. Bila kujali sababu, watoto wote ambao wana tatizo la kupungua kwa ukuaji na uzani hupatiwa lishe yenye virutubisho vya kutosha pamoja na kalori zinazohitajika kukuza ukuaji na ongezeko la uzani.
Tatizo la ukuaji kwa kiwango kidogo hadi cha wastani na kupungua kwa uzani hutibiwa kwa kutumia lishe yenye kalori nyingi au milo inayotolewa kwa ratiba ya kawaida. Walezi wanaweza kushauriwa kuhusu mwingiliano wa kifamilia unaomdhuru mtoto na kuhusu rasilimali za kifedha na kijamii zinazopatikana kwao.
Tatizo la kupungua kwa ukuaji na uzani hutibiwa hospitalini ambapo wafanyakazi wa kijamii, wataalamu wa lishe, wataalamu wa chakula, wataalamu wa magonjwa ya akili, na wataalamu wengine hufanya kazi kwa pamoja ili kubaini sababu zinazoweza kusababisha ukuaji wa polepole sana na ongezeko la uzani kwa kasi ya polepole kwa mtoto na njia bora ya kulisha au milo.
Watoto ambao tatizo la kupungua kwa ukuaji na uzani hutokana na unyanyasaji au kutelekezwa wanaweza kuhitaji kuwekwa katika mipango ya utunzaji wa watoto iliyoidhinishwa na serikali. Ikiwa watarudishwa kwa wazazi wao au hali ya awali ya nyumbani, maendeleo ya ukuaji wa watoto yanafuatiliwa.
Ubashiri wa Tatizo la Kupungua kwa Ukuaji na Uzito kwa Watoto
Kwa sababu mwaka wa kwanza wa maisha ni muhimu kwa ukuaji wa ubongo, watoto wana lishe duni wakati huu wanaweza kusalia nyuma ya wenzao kabisa katika ukuaji, hata kama ukuaji wao wa kimwili unaboreshwa.
Katika takriban nusu ya watoto hawa, ukuaji wa akili, hasa ujuzi wa lugha na hisabati, unabaki chini ya kiwango cha kawaida.