Kingamimba ya Dharura

NaFrances E. Casey, MD, MPH, NYU Grossman Long Island School of Medicine
Imekaguliwa naOluwatosin Goje, MD, MSCR, Cleveland Clinic, Lerner College of Medicine of Case Western Reserve University
Imepitiwa/Imerekebishwa Imebadilishwa Aug 2023
v8951650_sw

Kingamimba ya dharura inaweza kutumika kuzuia mimba kwa muda mfupi baada ya kufanya ngono isiyo salama.

Kingamimba ya dharura hupunguza uwezekano wa kupata mimba baada ya kipindi kimoja cha kufanya ngono isiyo salama, ikiwa ni pamoja na wakati tendo linapotokea karibu na wakati yai linapotolewa (ovulation), wakati kuna uwezekano wa kupata mimba. Kwa ujumla, uwezekano wa kupata mimba ni takriban asilimia 5 baada ya kipindi kimoja cha ngono isiyo salama, lakini ikiwa karibu na wakati wa yai kutolewa, ni takriban asilimia 20 hadi 30. Kadiri kingamimba ya dharura inavyotumika mapema, ndivyo kunakuwa na uwezekano wa kuwa na ufanisi zaidi.

Chaguo zilizopo za kingamimba za dharura ni pamoja na dawa zinazomezwa kwa mdomo na kifaa cha ndani ya uterasi (IUD) cha shaba. Dawa hizi (zinazoitwa vidonge vya asubuhi baada ya ngono) ni pamoja na levonorgestrel, ulipristal acetate, na vidonge mchanganyiko vya uzazi wa mpango (estrogen pamoja na levonorgestrel). Huzuia au kuchelewesha utoaji wa yai. Zinatumika zaidi kama kingamimba ya dharura kuliko IUD, ingawa kifaa cha ndani ya uterasicha shaba ndiyo aina bora zaidi ya kingamimba ya dharura. IUD ya shaba huzuia yai lililorutubishwa kupandikizwa kwenye uterasi.

  • Kuingizwa IUD ya shaba: Ili iwe yenye ufanisi, IUD lazima iingizwe ndani ya siku 5 baada ya kufanya ngono isiyo salama au, endapo muda wa kutoa yai unaweza kukadiriwa, ndani ya siku 5 baada ya kutoa yai (kutolewa kwa yai kutoka kwenye ovari). Uwezekano wa kupata mimba baada ya kuweka IUD ni asilimia 0.1, sawa na ilivyo wakati IUD inatumika kwa ajili ya uzazi wa mpango wa kawaida. Pia, baada ya kuwekwa, IUD inaweza kuachwa mahali pake ili kufanya uzazi wa mpango unaoendelea kwa hadi miaka 10. Ufanisi wa IUD ya shaba kama njia ya dharura ya uzazi wa mpango haiathiriwi na uzito. Kwa hivyo, kwa wanawake walio na unene kupita kiasi ambao wanatamani sana kuepuka mimba, IUD ya shaba ndiyo njia inayopendelewa zaidi ya kingamimba ya dharura.

  • Kuingizwa kwa IUD yenye dozi ya juu ya levonorgestrel: Ili iwe na ufanisi, IUD hii inapaswa kuwekwa ndani ya siku 5 za kufanya ngono isiyo salama au, ikiwa muda wa kutoa yai unaweza kukadiriwa, ndani ya siku 5 za kutoa yai. Uwezekano wa kupata mimba baada ya kuwekwa IUD hii ni asilimia 0.3.

  • Ulipristal acetate: Dozi moja ya dawa hii hutumiwa. Ina ufanisi zaidi kuliko levonorgestrel. Lazima itumiwe ndani ya siku 5 (saa 120) baada ya kufanya ngono bila kinga. Uwezekano wa kupata mimba ni takriban asilimia 1.5. Ulipristal acetate ina ufanisi zaidi kuliko levonorgestrel kwa wanawake walionenepa kupita kiasi, lakini kuwa na unene kupita kiasi hupunguza ufanisi wake. Agizo la dawa linahitajika. Baada ya wanawake kutumia ulipristal acetate, lazima wasubiri siku 6 kabla ya kutumia uzazi wa mpango wa homoni ulio na projestini. Wanapaswa kutumia njia mbadala ya uzazi wa mpango (kama vile kondomu) kwa siku 7 baada ya kuanza kutumia njia ya uzazi wa mpango ya homoni.

  • Levonorgestrel ikimezwa kwa mdomo: Levonorgestrel hutumika sana. Ni projestini ambayo mara nyingi hutumiwa katika dozi ndogo kwa ajili ya uzazi wa mpango. Wanawake wanaweza kutumia dozi moja, ikifuatiwa na dozi nyingine baada ya saa 12. Au wanaweza kutumia dozi moja ya juu zaidi. Uwezekano wa kupata mimba ni takriban asilimia 2 hadi 3. Hata hivyo, kingamimba ya dharura ya levonorgestrel inaweza kuwa na ufanisi mdogo kwa wanawake walio na unene kupita kiasi. Dozi hiyo huwa na ufanisi zaidi inapotumiwa mapema. Lazima itumiwe ndani ya siku 5 (saa 120) baada ya kufanya ngono bila kinga (ingawa ufanisi wake hupungua ikitumiwa baada ya siku 3). Nchini Marekani, vidonge hivi vinapatikana bila vikwazo kwa wanawake wa rika zote ambao wamewahi kufanya ngono bila kinga. Njia ya kupanga uzazi ya homoni inaweza kuanza wakati uo huo. Mbinu mbadala (kama vile kondomu) inapendekezwa kwa siku 7 baada ya kuanza kutumia njia ya kupanga uzazi ya homoni.

  • Mbinu ya Yuzpe: Kwenye mbinu hii, vidonge mchanganyiko vya uzazi wa mpango, ethinyl estradiol (aina ya estrojeni) pamoja na levonorgestrel, hutumika, lakini haina ufanisi mkubwa kuliko levonorgestrel au ulipristal acetate. Vidonge viwili vya mchanganyiko humezwa, vikifuatiwa na vidonge vingine viwili baada ya saa 12 lakini humezwa ndani ya saa 72 baada ya kufanya ngono isiyo salama. Dozi kubwa ya estrojeni hutumika. Dozi kubwa mara nyingi husababisha kichefuchefu na wakati mwingine husababisha kutapika. Madaktari wanaweza kupendekeza dawa zinazoweza kusaidia kuzuia kichefuchefu na kutapika. Njia hii haina ufanisi mkubwa kuliko njia zingine na hutumika tu pale ambapo wanawake hawana njia zingine. Njia ya kupanga uzazi ya homoni inaweza kuanza wakati uo huo. Mbinu mbadala (kama vile kondomu) inapendekezwa kwa siku 7 baada ya kuanza kutumia njia ya kupanga uzazi ya homoni.

Kipimo cha ujauzito hufanywa wiki 2 hadi 3 baada ya kutumia kingamimba ya dharura ili kuhakikisha mwanamke hana mimba. Kurejea kwa hedhi na matokeo hasi ya kipimo cha ujauzito kunathibitisha kuwa mwanamke huyo hana mimba.

Jedwali
Jedwali