Kifua Kikuu (TB)

NaEdward A. Nardell, MD, Harvard Medical School
Imekaguliwa naChristina A. Muzny, MD, MSPH, Division of Infectious Diseases, University of Alabama at Birmingham
Imepitiwa/Imerekebishwa Sept 2022 | Imebadilishwa Jan 2024
v785390_sw

Kifua kikuu ni maambukizi sugu yanayosababishwa na bakteria wanaoenezwa hewani Mycobacterium tuberculosis. Kwa kawaida huathiri mapafu, lakini karibu kiungo chochote cha mwili kinaweza kuhusika.

  • Kifua kikuu huenea hasa watu wanapovuta hewa iliyoambukizwa na mtu mwenye ugonjwa unaoathiri mwili.

  • Kikohozi ndicho dalili ya kawaida zaidi, lakini watu pia wanaweza kuwa na homa, kutokwa na jasho usiku, kupungua uzani, kujihisi dhaifu, na dalili nyingine endapo viungo vingine vitaathirika.

  • Utambuzi kwa kawaida huhusisha kipimo cha ngozi cha kifua kikuu au kipimo cha damu, picha za eksirei ya kifua, na uchunguzi na vipimo vya maabara vya sampuli ya makohozi.

  • Viuavijasumu viwili au zaidi hutolewa kila mara ili kupunguza uwezekano wa ukinzani wa bakteria.

  • Utambuzi wa mapema na matibabu pamoja na kuwatenga watu wenye ugonjwa unaoathiri mwili hadi watakapoitikia matibabu husaidia kuzuia kuenea kwa kifua kikuu.

(Tazama pia Kifua Kikuu kwa Watoto Waliozaliwa Karibuni.)

Kifua kikuu kwa kawaida huathiri mapafu, ingawa kinaweza kuathiri karibia kiungo chochote mwilini.

Kifua kikuu husababishwa na bakteria inayoitwa Mycobacterium tuberculosis. Bakteria nyingine zinazohusishwa (zinazoitwa mycobacteria), kama vile Mycobacterium bovis au Mycobacterium africanum, mara kwa mara husababisha ugonjwa kama huo. Bakteria hizi pamoja na Mycobacterium tuberculosis na baadhi ya nyingine huitwa mchanganyiko wa bakteria za mycobacterium tuberculosis.

Bakteria nyingine ya mycobacteria, hasa kundi lililoitwa mchanganyiko wa mycobacteria avium (MAC), pia husababisha magonjwa kwa watu. Magonjwa zinazosababisha ni tofauti na kifua kikuu.

Ukoma husababishwa na bakteria nyingine za mycobacteria.

Kifua kikuu dunia mzima

Kifua kikuu kimekuwa tatizo kubwa la afya ya umma kwa kipindi cha muda mrefu. Katika miaka ya 1800, ugonjwa huu ulisababisha zaidi ya asilimia 30 ya vifo vyote barani Ulaya. Kwa ujio wa viuavijasumu vya kuzuia kifua kikuu mwishoni mwa miaka ya 1940, vita dhidi ya kifua kikuu vilionekana kushindwa. Hata hivyo, kutokana na sababu kama rasilimali duni za afya ya umma, kudhoofika kwa kinga kutokana na VVU/UKIMWI, kuibuka kwa usugu wa dawa, na umaskini uliokithiri katika sehemu nyingi za dunia, kifua kikuu kinaendelea kuwa ugonjwa hatari duniani kote, kama takwimu za mwaka 2020 zinavyoonyesha:

  • Kulikuwa na takribani visa vipya milioni 9.9 vya kifua kikuu chenye dalili na takribani vifo milioni 1.5 vilivyosababishwa na ugonjwa huo.

  • Visa vingi vipya vilitokea Kusini-mashariki mwa Asia (43%), ambayo inajumuisha India na Pakistani, ikifuatiwa na Afrika (25%) na Pasifiki ya Magharibi (18%), ambayo inajumuisha Uchina, Japani, Ufilipino, na Australia.

  • Idadi ya visa vipya hutofautiana sana kulingana na nchi, umri, mbari, jinsia, na hali ya kijamii na kiuchumi. Theluthi mbili ya visa vipya vilitokea katika nchi nane. Visa vingi vipya vilitokea India, ikifuatiwa na Indonesia, Uchina, Ufilipino, Pakistani, Nigeria, Bangladeshi na Afrika Kusini.

Takribani robo ya watu wote duniani wanaaminika kuwa wameambukizwa. Wengi wana maambukizi ya kifua kikuu kisichosababisha athari kwa mwili (yasiyoathiri mwili au fiche). Asilimia ndogo tu ya maambukizi haya huendelea hadi kuwa kifua kikuu kinachoathiri mwili. Wakati wowote, takribani watu milioni 15 duniani kote wana kifua kikuu kianachoathiri mwili.

Duniani kote, kifua kikuu ndicho chanzo kikuu cha vifo. Katika mwaka wa 2020, kifua kikuu kiliwaua takribani watu milioni 1.5 duniani kote, wengi wao wakiwa katika nchi zenye kipato cha chini na cha kati.

Katika maeneo ya dunia ambako maambukizi ya VVU na kifua kikuu hutokea sana, kuwa na maambukizi ya VVU au UKIMWI huongeza sana hatari ya kupata kifua kikuu na kufa. Katika mwaka wa 2020, takribani vifo 214,000 kutokana na kifua kikuu vilitokea kwa watu wenye maambukizi ya VVU.

Je, Ulijua...

  • Kifua kikuu kilisababisha vifo vya takribani milioni 1.5 duniani kote mwaka wa 2020.

Kifua kikuu katika Marekani

Nchini Marekani mwaka wa 2021, visa vipya 7,860 (takribaniu visa 2.4 kwa kila watu 100,000) viliripotiwa. Hata hivyo, matukio hutofautiana kutoka jimbo moja hadi jingine. Kwa mfano, mwaka wa 2020, kulikuwa na visa 6.5 miongoni mwa watu 100,000 huko Hawaii na visa 0.4 miongoni mwa watu 100,000 huko Montana.

Katika mwaka 2020, asilimia 71 ya visa vipya nchini Marekani vilitokea kwa watu waliozaliwa nje ya Marekani katika maeneo ambapo kifua kikuu hotokea sana (kama vile Afrika, Asia, au Amerika Kusini). Hatari ya kuambukizwa huongezeka kwa watu wanaoishi katika makazi ya pamoja kama makazi ya dharura, vituo vya kutoa utunzaji wa muda mrefu, jela au magereza, na kwa wale waliokuwa hawana makazi katika mwaka uliopita. Nchini Marekani, makundi ya wachache huathiriwa kwa kiwango kikubwa zaidi. Kwa mfano, idadi ya kesi kwa kila watu 100,000 ni mara 8 zaidi kwa watu Weusi na hadi mara 33 zaidi kwa watu wa Asia kuliko kwa watu Weupe.

Jinsi Kifua kikuu Kinaendelea

Kwa magonjwa mengi ya kuambukiza (kama maambukizi ya koo au nimonia), watu huugua mara tu baada ya vijidudu kuingia mwilini na huonyesha dalili za kuugua ndani ya kipindi cha wiki 1 au 2. Kifua kikuu hakifuati mtindo huu.

Kifua kikuu hutokea kwa hatua mbalimbali:

  • Maambukizi ya msingi

  • Maambukizi fiche (yasiyoathiri mwili)

  • Ugonjwa ulio hai

Isipokuwa kwa watoto wadogo sana na watu walio na mfumo dhaifu wa kinga, ni idadi ya watu wachache sana ndio wanaougua mara tu bakteria wa kifua kikuu wanapoingia mwilini mwao (hatua hii ya awali inaitwa maambukizi ya kwanza). Katika hali nyingi, bakteria wa kifua kikuu zinazoingia kwenye mapafu huuawa mara moja na kinga ya mwili. Bakteria zinazosalia zikiwa hai humezwa na seli nyeupe za damu zinazoitwa makrofaji. Bakteria iliyomezwa inaweza kusalia ikiwa hai ndani ya seli hizi katika hali ya kutosababisha maambukizi kwa miaka mingi (hatua hii inaitwa maambukizi fiche). Mara nyingi, bakteria hizi hawasababishi matatizo zaidi, lakini kwa asilimia ndogo ya watu walioambukizwa, bakteria hizo hatimaye huanza kuongezeka na kusababisha ugonjwa unaoathiri mwili. Katika awamu hii, watu walioambukizwa huwa wagonjwa na wanaweza kueneza ugonjwa huo.

Maambukizi ya msingi

Katika wiki chache za mwanzo za maambukizi, baadhi ya bakteria zinaweza kusafiri kutoka kwenye mapafu hadi kwenye ntezi za limfu zilizokaribu. Tezi hizi za limfu ziko nje kidogo ya mapafu, ambapo mirija ya bronchi huingia kwenye mapafu. Kwa watu wengi, maambukizi hayaendelei zaidi, na bakteria hubaki katika hali ya kutosababisha maambukizi (haziathiri mwili) na hazisababishi dalili zozote.

Hata hivyo, maambukizi ya kwanza kwa watoto wadogo sana (ambao wana kinga dhaifu dhidi ya maambukizi) na watu wenye mfumo dhaifu wa kinga ya mwili yanaweza kusababisha nimonia na/au kifua kikuu kinachoathiri sehemu nyingine za mwili (kifua kikuu cha nje ya mapafu). Pia, kwa watoto wadogo, tezi za limfu zilizoathiriwa zinaweza kuwa kubwa vya kutosha kubana mirija ya bronchi na kusababisha dalili.

Kwa kawaida, maambukizi hayaambukizi wakati wa maambukizi ya kwanza.

Maambukizi ya kufichika

Wakati wa maambukizi fiche, bakteria husalia zikiwa hai lakini katika hali ya kutosababisha maambukizi ndani ya makrofaji kwa miaka mingi. Mwili huzingira bakteria ndani ya mkusanyiko wa seli, ambazo huunda makovu madogo sana. Bakteria isiyosababisha maambukizi haizai wala kusababisha dalili. Katika hali nyingi, bakteria hizi husalia katika hali ya kutosababisha maambukizi na hawasababishi matatizo yoyote zaidi.

Maambukizi hayo hayaambukizi wakati wa maambukizi fiche.

Ugonjwa ulio hai

Katika asilimia ndogo ya watu walioambukizwa, bakteria ya kifua kikuu ambayo haisababishi maambukizi hatimaye huanza kuongezeka na kusababisha ugonjwa unaathiri mwili. Kubadilika huku kutoka kwenye hali ya kutosababisha maambukizi huitwa kuanza tena kusababisha maambukizi. Katika awamu hii, watu walioambukizwa huwa wagonjwa na wanaweza kueneza ugonjwa huo.

Zaidi ya nusu ya wakati, bakteria zisizosababisha maambukizi huanza kusababisha maambukizi ndani ya kipindi cha miaka 2 ya kwanza baada ya maambukizi ya kwanza, lakini huenda zisisababisha maambukizi kwa muda mrefu sana, hata miongo kadhaa.

Kwa kawaida, madaktari hawajui ni kwa nini bakteria wasiosababisha maambukizi huanza kusababisha maambukizi, lakini kuanza kusababisha maambukizi huku kuna uwezekano mkubwa wa kutokea wakati mfumo wa kinga wa mtu unapodhoofika, hasa kutokana na Maambukizi ya VVU.

Sababu nyingine za hatari zinazoongeza uwezekano wa kuanza tena kusababisha maambukizi ni pamoja na zifuatazo:

  • Kisukari

  • Saratani ya kichwa na shingo

  • Upasuaji wa kuondoa sehemu ya tumbo au tumbo lote

  • Matatizo makali sugu ya figo

  • Matumizi ya tumbaku

  • Kupungua uzani kwa kiasi kikubwa

  • Matumizi ya dawa zinazokandamiza mfumo wa kinga ya mwili (kama vile kotikosteroidi na dawa nyingine kama vile adalimumab, etanercept, na infliximab)

  • Umri mkubwa sana

Kama magonjwa mengi ya kuambukiza, kifua kikuu huenea haraka zaidi na ni hatari zaidi kwa watu ambao wana mfumo dhaifu wa kinga ya mwili. Kwa watu kama hao, kifua kikuu kinaweza kuwa hatarishi kwa maisha.

Upitishaji wa maambukizi

Mycobacterium tuberculosis kinaweza kuishi ndani ya watu pekee. Bakteria hizi kwa kawaida hazienezwi na wanyama, wadudu, udongo, au vitu vingine visivyo hai. Watu huambukizwa kifua kikuu kwa kupumua pekee hewa iliyoambukizwa na mtu mwenye kifua kikuu kinachoathiri mwili. Kumgusa mtu mwenye ugonjwa hakuenezi ugonjwa huo kwa sababu bakteria ya Mycobacterium tuberculosis huenezwa karibu kupitia hewa pekee.

Watu wenye kifua kikuu kinachoathiri mwili kwenye mapafu au kwenye kisanduku cha nyuzi za sauti (zoloto) wanaweza kuambukiza hewa kwa bakteria wanapokohoa, kupiga chafya, au hata kuzungumza au kuimba. Bakteria hawa wanaweza kusalia hewani kwa saa kadhaa. Ikiwa mtu mwingine atavuta pumzi yenye bakteria, mtu huyo anaweza kuambukizwa. Hivyo basi, watu wanaoshirikiana na mtu aliye na kifua kikuu kinachoathiri mwili (kama wanajamii au wahudumu wa afya wanaomtibu mtu huyo) wako kwenye hatari kubwa ya kuambukizwa. Hata hivyo, mara tu watu wanapoanza matibabu yenye ufanisi, hatari ya kueneza maambukizi hupungua haraka, kwa kawaida baada ya takribani kipindi cha wiki 2.

Watu ambao wana maambukizi fiche au kifua kikuu ambacho kiko nje ya mapafu au pua kisanduku cha nyuzi ya sauti hawatoi bakteria hewani na hawawezi kueneza maambukizi.

Ingawa Mycobacterium tuberculosis huishi tu kwa watu, kuna bakteria wanaofanana nao ambao huathiri wanyama. Mycobacterium bovis ni mojawapo ya bakteria hizi zinazohusiana na mycobacteria. Kwa kawaida huambukiza ng'ombe na wakati mwingine huweza kuambukiza watu wanaokunywa maziwa ambayo hayajachemshwa kwenye moto kutoka kwa ng'ombe walioambukizwa. Katika nchi ambapo ng’ombe hufanyiwa vipimo vya kifua kikuu na maziwa huchemshwa kwa moto, maambukizi yanayosababishwa na bakteria hawa mara chache huwa tatizo. Hata hivyo, jibini linayotengenezwa kutokana na maziwa ambayo hayajachemshwa kwa moto kutoka kwa ng'ombe walioambukizwa wakati mwingine huletwa kinyume cha sheria nchini Marekani kutoka nchi nyingine na wakati mwingine husababisha maambukizi. Ikiwa Mycobacterium bovis itaambukiza mapafu, watu wanaweza kueneza bakteria kwa wengine wanapokoroma au kupiga chafya. Watu wanaofanya kazi katika vichinjio vya ng’ombe pia wako hatarini kuambukizwa.

Je, Ulijua...

  • Watu wenye kifua kikuu kinachoathiri mwili mara nyingi huambukiza hewa wanapokohoa, kupiga chafya, au hata kuzungumza au kuimba.

Kuendelea na kuenea kwa maambukizi

Maendeleo ya kifua kikuu kutoka kwenye maambukizi fiche hadi ugonjwa unaoathiri mwili hutofautiana kwa kiasi kikubwa. Maendelea hadi kufikia hatua ya ugonjwa unaoathiri mwili kuna uwezekano mkubwa zaidi na wa haraka zaidi wa kutokea kwa watu walio na maambukizi ya VVU na sababu nyingine za hatari. Ikiwa watu wenye Maambukizi ya VVU wataambukizwa na Mycobacterium tuberculosis na hawapati matibabu sahihi ya VVU, wana uwezekano wa takribani asilimia 10 ya kupata ugonjwa unaoathiri mwili kila mwaka. Kwa upande mwingine, watu ambao wana kifua kikuu kisichoonyesha dalili lakini hawana maambukizi ya VVU wana nafasi ya takribani asilimia 5 hadi 10 ya kupata ugonjwa unaoathiri mwili katika maisha yao.

Kwa watu wenye mfumo wa kinga ya mwili unaofanya kazi kikamilifu, kifua kikuu kinachoathiri mwili kwa kawaida huishia kwenye mapafu (kifua kikuu cha mapafu).

Kifua kikuu cha nje ya mapafu (kifua kikuu cha nje ya mapafu) kwa kawaida hutokana na kifua kikuu cha mapafu ambacho kimeenea kutoka kwenye mapafu kupitia damu na kuathiri sehemu nyingine za mwili. Kama ilivyo kwenye mapafu, maambukizi yanaweza yasilete ugonjwa, lakini bakteria wanaweza kutosababisha maambukizi wakiwa ndani ya kovu dogo sana. Bakteria zisizo sababisha maambukizi ambazo ziko ndani ya makovu haya zinaweza kuanza kusababisha maambukizi tena baadaye maishani, na kusababisha dalili zinazohusiana na viungo vinavyohusika.

Kifua kikuu cha miliari hutokea ikiwa idadi kubwa ya bakteria husafiri kupitia damu na kuenea mwilini kote. Aina hii ya kifua kikuu inaweza kuwa hatari kwa maisha.

Dalili na Matatizo ya Kifua Kikuu

Maambukizi ya msingi

Ni nadra kwa maambukizi ya kwanza kusababisha dalili, lakini dalili zinapotokea, kwa kawaida zinajumuisha uchovu, kikohozi, na homa ya kiwango cha chini. Utando mwembamba, wenye safu mbili unaofunika mapafu unaweza kuvimba na kusababisha maumivu ya kifua.

Maambukizi ya kufichika

Watu wenye maambukizi fiche hawana dalili.

Kifua kikuu cha mapafu amilifu

Baadhi ya watu wenye kifua kikuu cha mapafu kinachoathiri mwili hawana dalili zozote, isipokuwa kutojisikia vizuri, uchovu, kukosa hamu ya kula, na kupungua uzani. Dalili hizi hujitokeza polepole kwa kipindi cha wiki kadhaa. Watu wengine pia hupata dalili zinazoashiria maambukizi ya mapafu, kama vile kikohozi.

Kikohozi ndiyo dalili ya kawaida zaidi ya kifua kikuu cha mapafu. Kwa sababu ugonjwa hukua polepole, watu walioambukizwa mwanzoni wanaweza kudhani kikohozi kinatokana na uvutaji sigara, mafua ya hivi karibuni, mafua ya kawaida, au pumu. Kikohozi kinaweza kutoa kiasi kidogo cha makohozi ya kijani au manjano, hasa watu wanapoamka asubuhi. Hatimaye, makohozi yanaweza kuwa na michirizi ya damu, ingawa damu nyingi hutokea mara chache.

Watu wanaweza kuamka usiku wakiwa wamelowa kwa jasho baridi, wakiwa na homa au bila homa. Wakati mwingine jasho huwa jingi kiasi kwamba watu hulazimika kubadilisha nguo za kulalia au hata mashuka ya kitanda. Hata hivyo, kifua kikuu hakisababishi jasho la usiku kila mara, na magonjwa mengine mengi pia yanaweza kusababisha hali ya kutokwa na jasho la usiku.

Kukosa pumzi kunakoanza ghafla pamoja na maumivu ya kifua yanaweza kuashiria uwepo wa hewa (nimothoraksiau kioevu (mkusanyiko wa majimaji kati ya ukuta wa kifua na mapafu) katika nafasi iliyo kati ya mapafu na ukuta wa kifua. Karibu theluthi moja ya maambukizi ya kifua kikuu hutokea kwanza kama mkusanyiko wa majimaji kati ya ukuta wa kifua na mapafu. Hatimaye, watu wengi wenye kifua kikuu ambacho hakijatibiwa hukumbwa na tatizo la kukosa pumzi huku maambukizi yakienea kwenye mapafu.

Kifua kikuu cha mapafu za ziada

Labda, maeneo yanayoathirika mara nyingi zaidi na ugonjwa wa kifua kikuu unaotokea nje ya mapafu ni

  • Tezi ya limfu

  • Figo

Kifua kikuu kinaweza pia kuathiri mifupa, ubongo, tumbo, utando wenye safu mbili unaozunguka moyo (kifuko cha moyo), viungo (hasa viungo vinavyobeba uzani, kama vile viuno na magoti), na viungo vya uzazi. Kifua kikuu katika maeneo haya kinaweza kuwa kigumu kutambuliwa.

Dalili za kifua kikuu cha nje ya mapafu si dhahiri, na kwa kawaida ni uchovu, kukosa hamu ya kula, homa za mara kwa mara, kutokwa na jasho, na pengine kupungua uzani.

Wakati mwingine maambukizi husababisha maumivu, usumbufu, mkusanyiko wa usaha (jipu), au dalili nyingine, kutegemea na eneo lililoathirika.

  • Tezi ya limfu: Katika maambukizi mapya ya kifua kikuu, bakteria zinaweza kusafiri kutoka kwenye mapafu hadi kwenye tezi za limfu zinazochuja majimaji kutoka mapafuni. Ikiwa kinga ya asili ya mwili inaweza kudhibiti maambukizi, hayaendelei zaidi, na bakteria huacha kusababisha maambukizi. Hata hivyo, watoto wadogo sana wana kinga dhaifu. Ndani yake, nodi za limfu zinazochuja majimaji kutoka mapafuni zinaweza kuvimba kiasi cha kubana mirija ya bronchi, na kusababisha kikohozi cha sauti ya shaba na pengine mapafu kukosa kufanya kazi. Wakati mwingine, bakteria huenea kutoka kwenye mishipa hii ya limfu hadi kwenye tezi za limfu za shingoni. Maambukizi katika tezi za limfu za shingoni yanaweza kupasua ngozi na kutoa usaha. Wakati mwingine bakteria husafiri kupitia damu hadi kwenye tezi za limfu katika sehemu nyingine za mwili.

  • Figo na kibofu cha mkojo: Maambukizi ya figo yanaweza kusababisha homa, maumivu ya mgongo, na usaha na wakati mwingine damu kwenye mkojo. Maambukizi mara nyingi huenea hadi kwenye kibofu cha mkojo, na kumfanya mtu kukojoa mara kwa mara na kukojoa kwa maumivu.

  • Sehemu za siri: Kifua kikuu kinaweza pia kuenea hadi kwenye sehemu za siri. Kwa wanaume, kifua kikuu cha sehemu za siri husababisha korodani kupanuka. Kwa wanawake, husababisha maumivu sugu ya fupanyonga na utasa na huongeza hatari ya kupata mimba katika sehemu isiyo ya kawaida (mimba nje ya mfuko wa uzazi).

  • Ubongo: Kifua kikuu kinachoambukiza tishu zinazofunika ubongo (homa ya uti wa mgongo inayosababishwa na kifua kikuu) ni hatari kwa maisha. Nchini Marekani na nchi nyingine zilizoendelea, homa ya uti wa mgongo inayosababishwa na kifua kikuu hutokea kwa kawaida miongoni mwa wazee au watu walio na mfumo dhaifu wa kinga ya mwili. Katika maeneo ambako kifua kikuu ni cha kawaida miongoni mwa watoto, homa ya uti wa mgongo inayosababishwa na kifua kikuu hutokea zaidi kwa watoto kuanzia kuzaliwa hadi umri wa miaka mitano. Dalili ni pamoja na homa, maumivu ya kichwa yanayoendelea kutokea, kukakamaa kwa shingo, kichefuchefu, kuchanganyikiwa, na kusinzia ambako kunaweza kusababisha hali ya kukosa fahamu. Kifua kikuu kinaweza pia kuambukiza ubongo wenyewe, na kuunda uvimbe unaoitwa tuberculoma. KTuberculoma inaweza kusababisha dalili kama maumivu ya kichwa, kifafa, au udhaifu wa misuli. Tuberculoma pia hupatikana mara nyingi zaidi na husababisha madhara makubwa zaidi kwa watu walio na maambukizi ya VVU.

  • Kifuko cha moyo: Katika ugonjwa wa perikaditisi ya kifua kikuu, kifuko cha moyo (utando wenye safu mbili unaozunguka moyo) hunenepa na wakati mwingine huvuja maji kwenye nafasi iliyo kati ya kifuko cha moyo na moyo. Athari hizi hupunguza uwezo wa moyo kupiga na kusababisha homa, maumivu ya kifua, mishipa ya shingo iliyopanuka, na kupumua kwa shida. Katika sehemu za dunia ambako kifua kikuu ni hutokea sana, perikaditisi ya kifua kikuu ni chanzo cha kawaida cha kushindwa kwa moyo.

  • Utumbo: Kifua kikuu cha matumbo hutokea hasa katika nchi ambazo kifua kikuu kinachoambukiza ng'ombe ni tatizo. Huambukizwa kwa kula au kunywa bidhaa za maziwa ambazo hazijapashwa moto na zimechafuliwa na Mycobacterium bovis. Maambukizi haya yanaweza kusababisha maumivu, kuhara, kuziba kwa utumbo, na kutoka kwenye damu nyekundu kutoka kwenye tundu la haja kubwa. Tishu zilizo tumboni zinaweza kuvimba. Uvimbe huu unaweza kudhaniwa kimakosa kuwa ni saratani.

  • Ngozi: Kifua kikuu kinaweza kuenea kutoka sehemu nyingine, kama tezi za limfu au mifupa, hadi kwenye ngozi (huitwa kifua kikuu cha ngozi). Kinaweza kusababisha kutokea kwa vivimbe vigumu visivyo na maumivu. Hatimaye, vivimbe hivi hupanuka na kuunda vidonda vilivyo wazi. Mifereji inaweza kuunda kati ya eneo lililoambukizwa ndani ya mwili na ngozi, na usaha unaweza kutoka kupitia mifereji hiyo.

Jedwali
Jedwali
Jedwali
Jedwali

Utambuzi wa Kifua Kikuu

  • Eksirei ya kifua

  • Uchunguzi wa hadubini na uundaji wa sampuli ya makohozi

  • Kinapopatikana, kipimo cha ukuzaji wa asidi ya kiini (NAAT)

  • Kipimo cha ngozi cha tuberculin au vipimo vya damu kwa ajili ya kifua kikuu

  • Vipimo vya uchunguzi kwa watu walio katika hatari ya kupata kifua kikuu

Wakati mwingine dalili ya kwanza ya kifua kikuu ni matokeo ya kipimo yanayoonyesha uwepo wa maambukizi. Vipimo vya uchunguzi wa kifua kikuu hufanywa mara kwa mara kwa watu walio katika hatari ya kuambukizwa kifua kikuu.

Madaktari wanaweza kushuku kifua kikuu kulingana na dalili kama homa, kikohozi kinachodumu zaidi ya wiki 2 hadi 3, kutokwa jasho usiku, kupungua uzani, kikohozi kinachotoa damu, maumivu ya kifua na kupumua kwa shida.

Madaktari wanaposhuku kifua kikuu, vipimo vya kwanza vinavyofanywa ni

  • Eksirei ya kifua

  • Uchunguzi wa hadubini na uundaji wa sampuli ya makohozi

  • Rapid NAATs ili kuchunguza nyenzo za kijenetiki (DNA) za Mycobacterium tuberculosis katika sampuli za makohozi

Ikiwa utambuzi huo bado haujulikani, yafuatayo yanaweza kufanywa:

  • Kipimo cha ngozi cha tuberculin

  • Kipimo cha damu kwa ajili ya kifua kikuu

Ikiwa kifua kikuu kitagunduliwa, vipimo vya kuchunguza maambukizi ya VVU (ambayo ni sababu ya hatari ya kuambukizwa kifua kikuu) na homa ya ini B na homa ya ini C vinaweza kufanywa.

Eksirei ya kifua kwa ajili ya kifua kikuu

Kwa watu wenye kifua kikuu, picha ya eksirei ya kifua kwa kawaida huwa si ya kawaida. Hata hivyo, matokeo yasiyo ya kawaida katika kifua kikuu mara nyingi hufanana na yale ya magonjwa mengine, kwa hivyo utambuzi unaweza kutegemea matokeo ya kipimo cha ngozi cha tuberculin na uchunguzi wa makohozi kwa Mycobacterium tuberculosis.

Vipimo vya sputum kwa ajili ya kifua kikuu

Sampuli ya makohozi huchunguzwa kwa hadubini ili kutafuta bakteria ya kifua kikuu na hutumika kukuza bakteria hiyo katika kipimo cha maabara. Uchunguzi wa hadubini hutoa matokeo haraka zaidi kuliko tkipimo cha maabara lakini kina usahihi mdogo. Inagundua takribani nusu tu ya visa vya kifua kikuu vinavyotambuliwa kupitia kipimo cha maabara. Hata hivyo, vipimo vya jadi vya maabara havitoi matokeo kwa wiki nyingi kwa sababu bakteria wa kifua kikuu hukua polepole. Kwa sababu hii, matibabu ya watu wanaoweza kuwa na kifua kikuu huanza mara nyingi wakati madaktari wakisubiri matokeo ya uchunguzi na vipimo vya maabara vya makohozi. Kipimo cha maabara kinachopatikana kwa urahisi kinaweza kutambua ukuaji Mycobacterium tuberculosis kwa kawaida ndani ya siku 21.

Kipimo cha Maabara

Vipimo vinavyoongeza kiasi cha nyenzo za kijenetiki za bakteria (vinavyoitwa vipimo vya ukuzaji wa asidi ya kiini) vinaweza kuthibitisha uwepo wa Mycobacterium tuberculosis ndani ya saa 24 hadi 48. Toleo jipya la kipimo hiki linaweza kutoa matokeo ndani ya saa 2. Sampuli ya makohozi hutumika mara nyingi, lakini sampuli za tishu nyingine kama tezi za limfu zinaweza kutumika inapohitajika.

Vipimo vya kijenetiki vinaweza pia kubaini kwa haraka ikiwa bakteria ya kifua kikuu wana kinzana dhidi ya baadhi ya dawa za kawaida zinazotumika kutibu kifua kikuu, na hivyo kuwasaidia madaktari kuchagua matibabu bora. Vipimo hivi hugundua mabadiliko katika jeni za bakteria ambayo huwawezesha kupinga matibabu kwa kutumia dawa fulani.

Kipimo cha ngozi kwa ajili ya kifua kikuu

Kipimo cha ngozi cha tuberculin (pia huitwa kipimo cha Mantoux) kinachotumia protini iliyotolewa kwa bakteria na kusafishwa (PPD) hufanywa kwa kuingiza kiasi kidogo cha protini iliyotolewa kwa bakteria ya kifua kikuu kati ya safu za ngozi, kwa kawaida kwenye mkono wa mbele. Uvimbe hafifu huonekana mara moja, kisha hutoweka baada ya saa chache. Uvimbe huu humaanisha tu kwamba kipimo kilifanywa kwa usahihi. Takribani siku 2 au 3 baadaye, sehemu ambapo sindano ilidungwa hukaguliwa. Uvimbe unaohisiwa kuwa mgumu wakati wa kugusa na mkubwa zaidi ya ukubwa fulani unaonyesha matokeo uwepo wa maambukizi. Uwekundu karibu na sehemu hiyo bila uvimbe huonyesha kuwa hakuna maambukizi.

Baadhi ya watu ambao wako wagonjwa sana au wenye kinga ya mwili dhaifu (kama wale wenye maambukizi ya VVU) wanaweza wasiitikie kwa kipimo cha ngozi hata kama wameambukizwa na kifua kikuu.

Ingawa kipimo cha ngozi cha tuberculin ni mojawapo ya vipimo muhimu zaidi vya kutambua kifua kikuu, kinaonyesha tu kwamba mtu aliambukizwa na Mycobacterium tuberculosis au bakteria zinazohusiana nayo au alipokea chanjo ya kifua kikuu wakati fulani. Haionyeshi iwapo maambukizi ni kifua kikuu au kwamba maambukizi yanaendelea kwa sasa.

Yaani, matokeo yanaweza kuonyesha kifua kikuu wakati hakipo (matokeo yasiyo sahihi ya uwepo wa maambukizi) kwa sababu watu wana maambukizi yanayohusiana kwa karibu (ambayo kwa kawaida hayana madhara) au wamepata chanjo ya kifua kikuu hivi karibuni.

Matokeo pia yanaweza kuonyesha hakuna maambukizi ya kifua kikuu wakati kipo (matokeo yasiyo sahihi ya kutokuwepo kwa maambukizi). Lakini kwa kawaida, matokeo yasiyo sahihi ya kutokuwepo kwa maambukizi kwa watu pekee ambao

Kipimo cha damu kwa ajili ya kifua kikuu

Kipimo cha interferon-gamma release assay (IGRA) ni kipimo cha damu kinachoweza kugundua kifua kikuu. Kwa kipimo hiki, sampuli ya damu huchanganywa na protini zinazoundwa kwenye maabara zinazofanana na zile zinazozalishwa na bakteria ya kifua kikuu. Ikiwa watu wameambukizwa bakteria ya kifua kikuu, seli zao nyeupe za damu huzalishwa dawa fulani za kulevya (intaferoni) kuitikia protini zinazoundwa kwenye maabara. Kisha damu hiyo huchunguzwa kwa uwepo wa intaferoni ili kubaini kama kuna maambukizi ya kifua kikuu.

Kipimo hiki, tofauti na kipimo cha ngozi cha tuberculin, hakisababishi matokeo yasiyo sahihi ya uwepo wa maambukizi kwa watu ambao wamechanjwa dhidi ya kifua kikuu.

Vipimo vingine

Sampuli ya makohozi kwa kawaida hutosha, lakini mara kwa mara daktari anahitaji kupata sampuli ya kiowevu cha mapafu au tishu ili kufanya utambuzi. Ala inayoitwa bronkoskopu huingizwa kupitia mdomo au puani na kwenye njia za hewa. Inatumika kuchunguza mirija ya mapafu na kupata sampuli ya kioo cha mapafu au tishu. Taratibu hii kawaida hufanywa wakati magonjwa mengine, kama saratani ya mapafu, yanashukiwa.

Wakati dalili zinapendekeza ugonjwa wa homa ya uti wa mgongo inayosababishwa na kifua kikuu, daktari anaweza kuhitaji kufanya kipimo cha kuingiza mrija kwa uti wa mgongo (kudungwa sindano kwenye uti wa mgongo) ili kupata sampuli ya kiowevu cha uti wa mgongo kwa ajili ya uchanganuzi. Kwa sababu bakteria wa kifua kikuu ni vigumu kupata katika kiowevu cha uti wa mgongo na kwa sababu vipimo vya maabara kwa kawaida huchukua wiki, mbinu ya mmenyuko wa mnyororo wa polimerasi (PCR) inaweza kutumika kwenye sampuli. Hutoa aina nyingi za jeni, na kurahisisha utambuzi wa DNA ya bakteria. Ingawa matokeo ya vipimo yanapatikana haraka, madaktari kawaida huanza tiba ya antibiotiki ikiwa wana shaka yoyote ya ugonjwa wa TB wa uti wa mgongo. Matibabu ya mapema yanaweza kuzuia kifo na kupunguza uharibifu wa ubongo.

Vipimo vya Uchunguzi wa Kifua Kikuu

Vipimo fulani hufanywa mara kwa mara kwa watu walio katika hatari ya kuambukizwa kifua kikuu. Vipimo hivyo ni pamoja na kipimo cha ngozi cha tuberculin na kipimo cha damu cha interferon-gamma release assay (IGRA).

Watu walio hatarini kuambukizwa kifua kikuu ni pamoja na wale ambao

  • Wanaoishi au kufanya kazi na watu wenye kifua kikuu kinachoathiri mwili (vipimo hufanywa kila mwaka)

  • Wamebaki tu kutoka maeneo ambapo ugonjwa wa kifua kikuu hutokea sana

  • Wanaanza kutumia dawa ambayo inaweza kudhoofisha mfumo wa kinga na kuanzisha tena kifua kikuu kisichoonyesha dalili ikiwa kipo (kwa mfano, kotikosteroidi na tibakemikali ya saratani)

  • Wanaonyesha dalili za kifua kikuu kinachoweza kutokea kwenye picha ya Eksirei ya kifua kilichofanywa kwa sababu nyingine

  • Wana mfumo dhaifu wa kinga ya mwili (kwa mfano, kwa sababu ya maambukizi ya VVU)

  • Wana baadhi ya magonjwa, kama vile kisukari, ugonjwa wa figo, au saratani ya kichwa au shingo

  • Wana zaidi ya umri wa miaka 70

  • Wanajidunga dawa haramu

Ikiwa matokeo ya kipimo cha ngozi au kipimo cha damu kinichoonyesha uwepo wa maambukizi, watu hufanyiwa tathmini na daktari na picha ya Eksirei ya kifua hupigwa. Ikiwa picha ya eksirei ya kifua ni ya kawaida na watu hawana dalili zinazoashiria kifua kikuu, labda wanaweza kuwa na kifua kikuu kisichoonyesha dalili. Watu wenye kifua kikuu kisichoonyesha dalili hutibiwa kutumia viuavijasumu ( see page Kutibu kifua kikuu mapema). Ikiwa picha ya eksirei ya kifua si ya kawaida, watu hutathminiwa ili kubaini kama wana kifua kikuu kinachoathiri mwili ( see page Utambuzi wa Ugonjwa).

Matibabu ya Kifua Kikuu

  • Kujitenga

  • Dawa za kuua bakteria

  • Wakati mwingine upasuaji au dawa za kotikosteroidi

Watu wengi walioambukizwa hawahitaji kulazwa hospitalini kwa ajili ya kupokea matibabu. Watu hulazwa hospitalini ikiwa

  • Wanaugua sana kifua kikuu

  • Wana ugonjwa mwingine mbaya

  • Wanahitaji kufanyiwa taratibu za utambuzi wa ugonjwa

  • Hawana mahali pazuri pa kwenda (kwa mfano, ikiwa hawana makazi)

  • Wanahitaji kutengwa, kama watu wanaoishi katika mazingira ya kikundi ambapo wanaweza kukutana mara kwa mara na watu ambao hawajawahi kuambukizwa (kama vile nyumba ya kuwatunza wazee)

Kujitenga

Watu wenye kifua kikuu cha mapafu wanaotibiwa hospitalini hutengwa katika chumba kilichoundwa mahususi ili kupunguza hatari ya kueneza maambukizi kupitia hewa. Mlango hubaki kufungwa kadri inavyowezekana, na hewa ndani ya chumba hubadilishwa mara 6 hadi 12 kila saa. Watu waliotengwa hawahitaji kuvaa barakoa ya upasuaji ikiwa wanaweza kufuata maagizo ya jinsi ya kufunika kinywa wanapokohoa. Hata hivyo, watu wanaoingia chumbani ni sharti wavae kifaa cha kupumua (kifaa maalum cha kuchuja hewa, si barakoa ya kawaida ya upasuaji).

Watu wanaweza kuhamia kutoka kwenye kutengwa kwenda chumba cha kawaida cha hospitali wakati wameonyesha wazi kuwa wameitikia matibabu—kwa kawaida, wakati yote yafuatayo yanapotokea:

  • Sampuli zao za makohozi hazijaonyesha dalili zozote (hakuna bakteria ya kifua kikuu iliyoonekana) kwa kipindi muda fulani.

  • Hawana homa tena.

  • Wamepata tena hamu ya kula na hali ya afya njema.

Dawa za kuua bakteria

Idadi kadhaa ya viuavijasumu vinafaa katika kutibu kifua kikuu. Lakini kwa sababu bakteria wa kifua kikuu hukua polepole sana, dawa za antibiotiki lazima zitumiwe kwa muda mrefu—kwa miezi 4 hadi 6 au zaidi. Matibabu lazima yaendelee kwa muda mrefu baada ya watu kujihisi vizuri kabisa. Vinginevyo, kifua kikuu huwa kinajirudia kwa sababu hakikuondolewa kikamilifu. Pia, bakteria wa kifua kikuu wanaweza kuwa sugu dhidi ya dawa za antibiotiki.

Watu wengi hupata shida kukumbuka kutumia dawa zao kila siku kwa muda mrefu kama huo. Watu wengine, kwa sababu mbalimbali, husitisha matibabu mara tu wanapojihisi vizuri. Kwa sababu ya matatizo haya, wataalamu wengi wanapendekeza kwamba watu wenye kifua kikuu wachukue dawa zao kutoka kwa mtoa huduma wa afya, ambaye huwaangalia wakimeza vidonge. Mbinu hii inaitwa tiba inayoangaliwa moja kwa moja (DOT). Kwa sababu DOT inahakikisha kwamba watu wanatumia kila dozi, dawa mara nyingi hutolewa mara 2 au 3 tu kwa wiki baada ya wiki 2 za kwanza.

Antibiotiki mbili au zaidi zinazofanya kazi kwa njia tofauti hutolewa kila wakati kwa sababu matibabu ya dawa moja tu yanaweza kuacha bakteria wachache walio sugu kwa dawa hiyo. Kwa bakteria wengine wengi, bakteria wachache hawatoshi kusababisha kurudi tena kwa ugonjwa, lakini ikiwa kifua kikuu kitatibiwa kwa dawa moja tu, bakteria wa kifua kikuu muda si mrefu watakuwa sugu kwa dawa hiyo.

Hadi hivi karibuni, kulikuwa na awamu mbili za matibabu kwa watu ambao hawajawahi kutibiwa hapo awali:

  • Awamu ya kina: Watu hutumia antibiotiki nne kwa miezi 2.

  • Awamu ya mwendelezo: Watu hutumia antibiotiki mbili pekee kwa miezi 4 hadi 7 zaidi, kulingana na matokeo ya vipimo vya makohozi na eksirei za kifua.

Leo, watu fulani wanaweza kustahili kupata utaratibu wa matibabu unaodumu kwa miezi 4 na unajumuisha dawa mbili pekee.

Antibiotiki zinazotumika sana ni

  • Isoniazid

  • Rifampin

  • Pyrazinamide

  • Ethambutol

Dawa hizi nne zinaweza kutumika pamoja na zinatumika kwanza (zinaitwa dawa za mstari wa kwanza). Dawa hizi zote zina madhara, lakini watu wengi wenye kifua kikuu hupona kwa dawa hizi na hawapati madhara yoyote makubwa.

Kuna michanganyiko mingi tofauti na ratiba za dozi za dawa hizi. Isoniazid, rifampin, na pirazinamide zinaweza kuwa ndani ya kidonge kimoja, na hivyo kupunguza idadi ya vidonge ambavyo watu wanapaswa kutumia kila siku na kupunguza uwezekano wa dawa kuwa na usugu. Tofauti na antibiotiki nyingine, zile zinazotumika kutibu kifua kikuu kwa kawaida hutumika zote kwa wakati mmoja, mara moja kwa siku au mara 2 au 3 kwa wiki.

Dawa za mstari wa pili Kwa kawaida hutumika wakati bakteria wanaosababisha kifua kikuu wameanza kustahimili dawa za mstari wa kwanza au pale ambapo watu hawawezi kuvumilia dawa za mstari wa kwanza. Dawa zingine za antibiotiki hutumika kama dawa za mstari wa pili. Zinajumuisha aminoglycosides(kama vile streptomycin, kanamycin. na amikacin), capreomycin (ambayo ina uhusiano wa karibu na aminoglycosides), na fluoroquinolone (kama vile levofloxacin na moxifloxacin).

Dawa zingine mpya zimetengenezwa ili kusaidia kutibu kifua kikuu ambacho ni sugu kwa dawa za kawaida. Dawa hizi ni pamoja na bedaquiline, delamanid, na pretomanid.

Jedwali
Jedwali

Je, Ulijua...

  • Matibabu ya kifua kikuu lazima yaendelee kwa muda mrefu baada ya watu kujisikia vizuri.

Upinzani wa dawa

Bakteria ya kifua kikuu inaweza kuwa sugu kwa antibiotiki kwa urahisi, hasa wakati watu hawatumii dawa hizo mara kwa mara au kwa muda mrefu kama inavyotakiwa.

Bakteria wanaostahimili matibabu kwa kutumia antibiotiki wanasababisha visa vingi zaidi vya kifua kikuu (kinachoitwa kifua kikuu kinachostahimili dawa).

Usugu wa dawa ni tatizo kubwa kwa sababu kifua kikuu kilicho sugu kwa dawa lazima kitibiwe kwa muda mrefu sana. Kwa kawaida watu lazima watumie dawa nne au tano kwa miezi 18 hadi 24. Dawa zinazotumika kutibu kifua kikuu kilicho sugu kwa dawa mara nyingi huwa na ufanisi mdogo, zenye sumu zaidi, na ghali zaidi.

Bakteria wa kifua kikuu ambao ni sugu kwa antibiotiki huainishwa kulingana na usugu wake kwa dawa husika. Uainishaji wa Shirika la Afya Duniani (WHO) ni

  • Kifua kikuu sugu kwa dawa nyingi (MDR-TB): Sugu kwa angalau isoniazidi na rifampin

  • Kifua kikuu ambacho hakijawa sugu kwa dawa nyingi (kabla ya XDR-TB): Usugu kwa isoniazid na rifampin na pia fluoroquinolone yoyote

  • Kifua kikuu sugu sana kwa dawa (XDR-TB): Ni sugu kwa isoniazid, rifampin, fluoroquinolone yoyote, na angalau moja ya dawa zifuatazo: levofloxacin, moxifloxacin, bedaquiline, au linezolid

Dawa mpya za kifua kikuu bedaquiline, delamanid, na pretomanid na fluoroquinolone moxifloxacin zinafanya kazi dhidi ya aina sugu za bakteria wa kifua kikuu na zinaweza kusaidia kudhibiti janga la usugu dhidi ya dawa.

Matibabu mengine

Upasuaji wa kuondoa sehemu ya mapafu ni mara chache sana unahitajika ikiwa watu hufuata mpango wa matibabu ya dawa kwa uaminifu. Hata hivyo, upasuaji wakati mwingine unahitajika ili kutibu watu wenye hali zifuatazo:

  • Maambukizi yaliyo sugu sana kwa dawa

  • Kikohozi kinachoendelea kutoa damu

  • Njia za hewa zilizoziba

  • Usaha uliojikusanya (ili kuukausha)

Wakati perikaditisi ya kifua kikuu inasababisha kizuizi kikubwa cha mwendo wa moyo, pericardium inaweza kuhitaji kuondolewa kupitia upasuaji. Tuberculoma (uvimbe unaotokea kwa sababu ya kifua kikuu) kwenye ubongo inaweza kuhitaji kuondolewa kwa upasuaji.

Wakati mwingine madaktari hutoa kotikosteroidi (kama vile dexamethasone) wakati ambapo kifua kikuu kinasababisha uvimbe mwingi, hasa kwa watu wenye ugonjwa wa homa ya uti wa mgongo, pericarditis, au uvimbe wa mapafu.

Kinga ya Kifua Kikuu

Kinga ya kifua kikuu ina vipengele vitatu:

  • Kuzuia enezaji wa maambukizi

  • Kutibu maambukizi mapema kadiri iwezekanavyo kabla hayajawa ugonjwa unaoendelea

  • Wakati mwingine chanjo

Kukomesha kuenea kwa kifua kikuu

Kwa sababu bakteria wa kifua kikuu wapo kwenye hewa, uingizaji hewa mzuri kwa kutumia hewa safi hupunguza mkusanyiko wa bakteria na kupunguza kuenea kwao. Pia, taa za miale ya urujuanimno zinaweza kutumika kuua bakteria wa kifua kikuu wanaoenezwa kwa njia ya hewa katika majengo ambapo watu walio hatarini wamekusanyika, kama vile makazi ya watu wasio na makazi, magereza, na maeneo ya kusubiri hospitalini na idara ya dharura. Endapo watoa huduma wa afya hushughulikia sampuli za tishu au majimaji yaliyoambukizwa au kuingiliana na watu ambao wanaweza kuwa wameambukizwa, huvaa barakoa zilizowekwa maalum zinazoitwa vipumuliaji, ambavyo huchuja hewa, ili kuwasaidia kuwalinda.

Hakuna tahadhari zinazohitajika ikiwa watu hawana dalili hata kama kipimo chao cha ngozi au damu cha kifua kikuu kinaonyesha kuwa wana maambukizi.

Watu wengi wenye kifua kikuu amilifu hawahitaji kulazwa hospitalini. Hata hivyo, ili kusaidia kuzuia kuenea kwa ugonjwa huo, wanapaswa kufanya yafuatayo:

  • Kukaa nyumbani

  • Kuepuka wageni (hawahitaji kuepuka wanafamilia ambao tayari wapo kwenye mazingira hayo)

  • Kufunika mdomo kwa kitambaa au kiwiko wanapokohoa

Watu wanapaswa kuzingatia tahadhari hizi hadi watakaponekana kupona na hawakohoi tena. Baada ya wiki moja au mbili tu za matibabu kwa kutumia antibiotiki sahihi, watu wana uwezekano mdogo wa kueneza ugonjwa huo. Hata hivyo, ikiwa wanaishi au wanafanya kazi na watu walio katika hatari kubwa (kama vile watoto wadogo au watu wenye UKIMWI), uchambuzi wa kurudiwa wa sampuli za makohozi unaweza kuhitajika ili kubaini wakati ambapo hatari ya kueneza maambukizi imepita. Pia, watu wanaoendelea kukohoa wakati wa matibabu, hawatumii dawa zao kama ilivyoelekezwa, au wana kifua kikuu sugu sana dhidi ya dawa wanaweza kuhitaji kufuata tahadhari hizi kwa muda mrefu ili wasieneze ugonjwa huo.

Matibabu ya kusimamiwa moja kwa moja (DOT) pia yanaweza kusaidia kuzuia kuenea kwa maambukizi. Kuhakikisha kwamba watu walioambukizwa wanahutumia dawa walizoandikiwa kama ilivyoelekezwa huongeza uwezekano wa bakteria kutokomezwa.

Wafanyakazi wa afya ya umma hujaribu kubaini ni nani aliyeambukizwa na mtu mwenye kifua kikuu na kupendekeza kwamba watu hawa wapimwe kifua kikuu.

Kutibu kifua kikuu mapema

Kwa sababu kifua kikuu huenezwa tu na watu wenye ugonjwa amilifu, matibabu ya ugonjwa tuli na utambuzi wa mapema na matibabu ya ugonjwa amilifu ni miongoni mwa njia bora za kuzuia kuenea kwake.

Watu wengi ambao wana ngozi inayoonyesha kifua kikuu au wamepimwa damu hutibiwa hata kama bado hawajaugua.

Antibiotiki ya isoniazid ina ufanisi mkubwa katika kuzuia maambukizi kabla hayajawa ugonjwa amilifu. Inatolewa kila siku kwa miezi 9. Kwa baadhi ya watu, rifampin pekee inaweza kutolewa kila siku kwa miezi 4. Katika baadhi ya nchi, isoniazid na rifapentine hutumiwa pamoja mara moja kwa wiki kwa miezi 3 kama matibabu yanayosimamiwa moja kwa moja.

Tiba ya kinga kwa hakika huwanufaisha vijana ambao wamepimwa ngozi na kuonesha wana tuberculin. Pia ina uwezekano wa kuwasaidia wazee waliopimwa ngozi na kuonesha wana tuberculin ikiwa wako katika hatari kubwa ya kupata kifua kikuu—kwa mfano, ikiwa yoyote kati ya yafuatayo yanatumika:

  • Kipimo chao cha ngozi au damu kilibadilika hivi karibuni kutoka hasi na kuwa chanya.

  • Wamekuwa katika mazingira ya ugonjwa hivi karibuni.

  • Wana mfumo dhaifu wa kinga.

Kwa wazee walio na maambukizi tuli ya muda mrefu, hatari ya usumu kutokana na antibiotiki inaweza kuwa kubwa kuliko hatari ya kupata kifua kikuu. Katika hali kama hizo, mara nyingi madaktari huwasiliana na mtaalamu wa masuala hayo kabla ya kuamua kama watatumia tiba ya kuzuia.

Ikiwa watu wamepimwa ngozi au damu na kuonekana wana ugonjwa, hatari ya kupata maambukizi ni kubwa katika hali zifuatazo:

  • Ikiwa wataambukizwa VVU

  • Ikiwa watatumia dawa za kotikosteroidi au dawa zingine zinazokandamiza mfumo wa kinga (ikiwa ni pamoja na baadhi ya dawa mpya za kuzuia mwako)

Watu kama hao kwa kawaida wanahitaji matibabu ya maambukizi ya kifua kikuu tuli.

Chanjo kwa ajili ya kifua kikuu

Katika maeneo ya dunia ambapo kifua kikuu kimeenea, chanjo inayoitwa bacille Calmette-Guérin (BCG) hutumika kufanya yafuatayo:

  • Kuzuia kuongezeka kwa matatizo makubwa, kama vile meningitis

  • Husaidia kuzuia maambukizi kwa watu walio katika hatari kubwa ya kuambukizwa Kifua kikuu cha Mycobacterium, hasa watoto

Kwa kawaida madaktari hawapendekezi chanjo ya BCG kwa watu wanaoishi Marekani. Hata hivyo, chanjo inaweza kuwa na jukumu katika kuwalinda wafanyakazi wa huduma ya afya na wengine (hasa watoto) walio katika hatari ya kupata kifua kikuu ambacho ni sugu dhidi ya dawa mbili au zaidi.

Utafiti unaendelea kufanya ili kutengeneza chanjo yenye ufanisi zaidi.

Watu waliopokea BCG wakati wa kuzaliwa wanaweza kuonyesha wana ugonjwa kupitia kipimo cha ngozi cha tuberculin miaka mingi baadaye, hata kama hawajaambukizwa bakteria wa kifua kikuu. Athari ya chanjo ya BCG kwenye matokeo ya vipimo vya ngozi kwa kawaida huwa ndogo kuliko ile ya kifua kikuu, na hupungua kadri muda unavyopita. Takriban miaka 15 baada ya chanjo ya BCG, matokeo chanya ya kipimo yana uwezekano mkubwa wa kusababishwa na kifua kikuu kuliko chanjo ya BCG. Hata hivyo, watu waliochanjwa wakati wa kuzaliwa mara nyingi, badaye maishani mwao, wanahusisha kimakosa kipimo cha ngozi kinachoonyesha kuwa na ugonjwa na chanjo ya BCG. Katika nchi nyingi, kifua kikuu hunyanyapaliwa, na watu wengi wanasita kuamini kwamba wana maambukizi tuli, na ugonjwa ulio amilifu kidogo. Kwa kawaida, ikiwa watoto waliochanjwa wafanya kipimo cha ngozi cha tuberculin, madaktari hudhani ni kutokana na kifua kikuu na hutibu ipasavyo. Maambukizi tuli yasiyotibiwa yanaweza kusababisha matatizo makubwa, hasa kwa watoto.

Hata hivyo, ikiwezekana, watu waliopewa chanjo ya BCG wanapaswa kupimwa kwa kutumia kipimo cha kutolewa kwa interferon-gamma (IGRA) kwa sababu IGRA haisababishi matokeo ya kipimo chanya cha uwongo kwa watu waliopokea chanjo ya BCG. Kipimo hiki kinaweza pia kubaini endapo mwitikio chanya wa kipimo cha ngozi unatokana na maambukizi ya Kifua kikuu cha Mycobacterium.