Clostridioides (zamani Clostridium) difficile–Colitis Iliyoambukizwa

(Kolaitisi ya Pseudomembranous; C. diff)

NaLarry M. Bush, MD, FACP, Charles E. Schmidt College of Medicine, Florida Atlantic University;
Maria T. Vazquez-Pertejo, MD, FACP, Wellington Regional Medical Center
Imekaguliwa naBrenda L. Tesini, MD, University of Rochester School of Medicine and Dentistry
Imepitiwa/Imerekebishwa Imebadilishwa Jun 2023
v39247319_sw

Clostridioides difficile (C. difficile-colitis) ni uvimbe wa utumbo mpana (koloni) unaosababisha kuhara. Uvimbe husababishwa na sumu inayozalishwa na bakteria wa C. difficile na kwa kawaida hujitokeza baada ya watu kutumia viuavijasumu vinavyowezesha bakteria hawa.

  • C. difficile-colitis kwa kawaida hutokea baada ya kutumia viuavijasumu.

  • Dalili za kawaida huanzia kinyesi kilicholegea kidogo hadi kuhara damu, maumivu ya tumbo, na homa.

  • Madaktari hupima kinyesi na wakati mwingine hutumia mrija wa kutazama ili kuchunguza utumbo mkubwa wa watu wenye dalili za C. difficile-colitis.

  • Watu wengi wenye C. Difficile-colitis hupona baada ya kiuavijasumu kilichochea colitis kusitishwa na kiuavijasumu kingine kuanza kutumiwa.

Clostridioides difficile (C. difficile, C. difficile) hazihitaji oksijeni ili kuishi. Yaani, hivyo ni anaerobi.

Je, Ulijua...

  • Baadhi ya watu wenye afya njema wana bakteria wa C. difficile wanaoishi kwenye utumbo wao.

(Angalia pia Muhtasari wa Maambukizi ya Clostridial.)

Sababu za C. diff Colitis

Katika C. difficile-colitis, bakteria huzalisha sumu zinazosababisha uvimbe wa utumbo mpana (colitis), kwa kawaida baada ya viuavijasumu kutumiwa kutibu maambukizi. Viuavijasumu vingi hubadilisha uwiano wa aina na wingi wa bakteria wanaoishi kwenye utumbo. Hivyo, bakteria fulani zinazosababisha magonjwa, kama vile C. difficile, wanaweza kukua na kuchukua nafasi ya bakteria wasio na madhara ambao kwa kawaida huishi kwenye utumbo. C. difficile ndiyo sababu ya kawaida ya ugonjwa wa colitis unaotokea baada ya matumizi ya viuavijasumu.

Wakati bakteria wa C. difficile wanapozidi kukua, hutoa sumu zinazosababisha kuhara, colitis, na kutengenezwa kwa utando usio wa kawaida (pseudomembrani) kwenye utumbo mpana.

Aina hatari zaidi ya C. difficile imetambuliwa katika baadhi ya milipuko ya magonjwa hospitalini. Aina hii hutoa sumu zaidi, husababisha ugonjwa mbaya zaidi na uwezekano mkubwa wa kurudia tena, ni rahisi kuambukizwa, na haijibu vizuri matibabu ya viuavijasumu.

Karibu kiuakijasumu chochote kinaweza kusababisha tatizo hili, lakini clindamycin, penicillin (kama vile ampicillin na amoxicillin), cephalosporin (kama vile ceftriaxone), na fluoroquinolone (kama vile levofloxacin na ciprofloxacin) ndizo zinazohusishwa mara nyingi zaidi. C. difficile-colitis inaweza kutokea hata baada ya matumizi ya muda mfupi sana ya kiuavijasumu. C. difficile-colitis pia inaweza kutokea baada ya matumizi ya baadhi ya dawa za tibakemikali ya saratani.

Maambukizi ya C. difficile hutokea sana wakati dawa ya kiuavijasumu inapomezwa kwa mdomo, lakini pia hutokea wakati dawa za viuavijasumu zinapodungwa kwenye misuli au kutolewa kwa mshipa (kwa njia ya mishipa).

Madhara ya kupata C. difficile-colitis na hatari yake huongezeka kadiri umri unavyoongezeka. Hali nyingine za hatari zinajumuisha

  • Kuwa na ugonjwa mmoja au zaidi mkali

  • Kukaa hospitalini kwa muda mrefu

  • Kuishi katika makazi ya huduma za uuguzi

  • Kufanyiwa upasuaji wa mfumo wa mmeng’enyo wa chakula

  • Kuwa na tatizo au kutumia dawa inayopunguza asidi tumboni

Dawa zinazopunguza asidi ya tumbo ni pamoja na vizuizi vya vimeng’enya vya kutoa protoni na vizuizi vya histamine-2 (H2), ambavyo hutumika kutibu ugonjwa wa kurudi kwa asidi kwenye umio na ugonjwa wa kidonda cha tumbo.

Wakati mwingine chanzo cha bakteria ni utumbo wa mtu mwenyewe. C. Difficile kwa kawaida hupatikana kwenye utumbo wa watoto wachanga, watu wazima wenye afya njema, na watu wazima waliolazwa hospitalini. Katika watu hawa, C. difficile kwa kawaida hazisababishi magonjwa isipokuwa zikikua sana. Hata hivyo, watu hawa wanaweza kueneza clostridia kwa watu walio katika hatari. Kuenea kwa maambukizi kutoka kwa mtu hadi mwingine kunaweza kuzuiwa kwa kuosha mikono kwa kina zaidi.

Watu pia wanaweza kupata bakteria kutoka kwa wanyama vipenzi au kutoka kwenye mazingira.

Ugonjwa wa colitis unaosababishwa na maambukizi ya C. difficile hutokea mara chache isipokuwa watu wawe wametumia viuavijasumu hivi majuzi. Hata hivyo, matukio yanayosababisha mfadhaiko wa mwili, kama vile upasuaji (hasa unaohusisha tumbo au utumbo), yanaweza kusababisha pia usumbufu wa uwiano wa aina na wingi wa bakteria kwenye utumbo au kuathiri mifumo ya asili ya ulinzi wa utumbo, jambo ambalo, kwa upande wake, huruhusu maamukizi ya C. difficile na ugonjwa wa colitis kutokea.

Dalili za C. diff Colitis

Dalili za maambukizi ya C. difficile kwa kawaida huanza siku 5 hadi 10 baada ya kuanza kutumia viuavijasumu lakini yanaweza kutokea siku ya kwanza au hadi miezi 2 baadaye.

Dalili hutofautiana kulingana na kiwango cha uvimbe unaosababishwa na bakteria, kuanzia kinyesi kilicholegea kidogo hadi kuhara damu, maumivu ya tumbo na mkakamao wa misuli ya tumbo, na homa. Kichefuchefu na kutapika hutokea mara chache.

Visa vilivyo kali zaidi(fulminant colitis) vinaweza kuhusisha hali inayotishia maisha za upungufu wa maji mwilini, mapigo ya moyo ya juu shinikizo la chini la damu na kutoboka kwa utumbo mpana.

Utambuzi wa C. diff Colitis

  • Vipimo vya kinyesi

  • Wakati mwingine kipimo cha sigmoidoskopia au kolonoskopia

Madaktari wanashuku C. difficile-colitis kwa mtu yeyote anayepata kuhara ndani ya miezi 2 baada ya kutumia dawa ya kiuavijasumu au ndani ya saa 72 baada ya kulazwa hospitalini.

Utambuzi unathibitishwa kwa kutumia vipimo vya kinyesi. Madaktari hufanya vipimo ili kugundua sumu zinazozalishwa na C. difficile pamoja na kimeng'enya fulani kinachotolewa na bakteria. Madaktari pia hufanya vipimo kama vile mwitikio wa mnyororo wa polymerase (PCR) ili kugundua uwepo wa nyenzo za kijeni (DNA) za bakteria.

Daktari anaweza pia kutambua C. difficile-colitis kwa kukagua sehemu ya chini ya utumbo mpana uliovimba (koloni ya sigmoid), kwa kawaida kupitia sigmoidoskopia (mrija wa kutazama unaonyumbulika). Iwapo wataona aina maalum ya uvimbe inayoitwa pseudomembranous colitis, C. difficile–colitis hutambuliwa. Kolonoskopia (mrija mrefu unaonyumbulika la kuangalia ndani) hutumiwa kuchunguza utumbo mpana wote endapo sehemu iliyoathirika ya utumbo iko juu zaidi kuliko uwezo wa kufikiwa na sigmoidoskopia. Hata hivyo, taratibu hizi kwa kawaida hazihitajiki.

Madaktari wanaweza kufanya vipimo vya upigaji picha, kama vile eksirei au tomografia iliyokokotolewa (CT) ya tumbo, ikiwa wanashuku tatizo kubwa, kama vile kutoboka kwa utumbo mpana, ugonjwa wa fulminant colitis au megacoloni.

Matibabu ya C. diff Colitis

  • Kusitisha matumizi ya viuavijasumu vinavyosababisha ugonjwa wa colitis

  • Viuavijasumu vyenye ufanisi dhidi ya C. difficile

  • Kwa ajili ya kujirudia, viuavijasumu

  • Kwa kujirudia mara kwa mara, wakati mwingine upandikizaji wa haja kubwa (kinyesi)

Ikiwa mtu mwenye C. difficile–colitis anapata kuhara akiwa anatumia kiuavijasumu, kiuavijasumu hicho husitishwa mara moja isipokuwa ikiwa ni cha lazima sana kuendelea kukitumia. Baada ya kusitisha kiuavijasumu, dalili kwa kawaida hupotea ndani ya siku 10 hadi 12. Ikiwa dalili ni kali au zinaendelea, watu kwa kawaida hupewa antibiotiki ambayo hufanya kazi dhidi ya C. difficile.

Visa vingi vya C. difficile-colitis hutibiwa kwa kutumia kiuavijasumu cha vancomycin au fidaxomicin, zinazotolewa kwa mdomo. Fidaxomicin husababisha kujirudia kwa dalili mara chache.

Dawa (kama vile loperamide) ambazo watu wakati mwingine hutumia kupunguza mwendo wa utumbo na kutibu kuhara hazipaswi kutumiwa. Dawa hizo zinaweza kurefusha au kuzidisha ugonjwa kwa kuweka sumu inayosababisha ugonjwa ikigusa utumbo mpana kwa muda mrefu zaidi.

Mara kwa mara, C. difficile-colitis ni mbaya sana kiasi kwamba mtu lazima alazwe hospitalini ili apate maji ya mshipa, elektroliti (kama vile sodiamu, magnesiamu, kalsiamu na potasiamu), na kuongezewa damu.

Mara chache, upasuaji unahitajika. Kwa mfano, upasuaji wa kuondoa utumbo mpana (colectomy) unaweza kuhitajika katika visa vikali kama hatua ya kuokoa maisha.

Matibabu ya kurudia

Dalili hurudi kwa asilimia 15 hadi 20 ya watu wenye ugonjwa huu, kwa kawaida ndani ya wiki chache baada ya kuacha matibabu. Mara ya kwanza kuhara kunaporudi, watu hupewa dawa zingine za kiuavijasumu sawa. Ikiwa kuhara kunaendelea kurudi, hupewa vancomycin au fidaxomicin, yoyote ambayo hawajapewa bado, kwa wiki kadhaa.

Kupandikiza kinyesi (haja kubwa) ni chaguo kwa baadhi ya watu ambao ugonjwa hujirudia mara kwa mara. Katika utaratibu huu, takriban kikombe (karibu mililita 200 hadi 300) cha kinyesi kutoka kwa mtoaji mwenye afya njema huwekwa kwenye utumbo mpana wa mtu. Kinyesi cha mchangiaji hupimwa kwanza ili kubaini vijidudu vinavyoweza kusababisha ugonjwa. Upandikizaji wa kinyesi unaweza kutolewa kama enema, kupitia mrija unaoingizwa kupitia pua hadi kwenye njia ya kumeng'enya chakula, au kupitia kolonoskopia. Madaktari wanafikiri kwamba kinyesi kutoka kwa mchangiaji hurejesha usawa wa kawaida wa bakteria kwenye utumbo wa mtu aliye na C. difficile-colitis. Baada ya matibabu haya kutumika, kuna uwezekano mdogo wa dalili kurudi tena. Tembe iliyo na kinyesi chenye afya cha mchangiaji pia ni tiba bora.

Bezlotoxumab ni dawa ya kingamwili ya monokloni ambayo hutolewa na mshipa. Hujifunga kwenye mojawapo ya sumu zinazozalishwa na C. difficile. Kutoa bezlotoxumab pamoja na matibabu ya kawaida ya kiuavijasumu kunaweza kupunguza uwezekano wa kuhara kurudia.