Utunzaji wa Kwanza wa Mtoto Aliyezaliwa Karibuni

NaDeborah M. Consolini, MD, Thomas Jefferson University Hospital
Imekaguliwa naAlicia R. Pekarsky, MD, State University of New York Upstate Medical University, Upstate Golisano Children's Hospital
Imepitiwa/Imerekebishwa Sept 2023 | Imebadilishwa Mar 2024
v813458_sw

Watoto wachanga wenye afya (kutoka kuzaliwa hadi mwezi 1) na watoto wachanga (kutoka mwezi 1 hadi mwaka 1) wanahitaji aina mbalimbali za huduma ili kuhakikisha ukuaji wa kawaida na afya njema.

Wakati wa kujifungua, kijusi ambacho huwa ndani ya maji ya amnioni na hutegemea kondo la nyuma kwa lishe na oksijeni hubadilika kwa kiasi kikubwa na kuwa mtoto mchanga anayepumua hewa na kula kwa mdomo. Mara tu baada ya mtoto kuzaliwa, daktari, mkunga, au muuguzi huondoa ute na mabaki mengine kutoka mdomoni, puani, na kooni kwa kutumia kifaa cha kufyonza. Baada ya hapo, mtoto mchanga huanza kupumua na hahitaji tena oksijeni kupitia kitovu. Vibanio viwili huwekwa kwenye kamba ya kitovu, kisha kamba hukatwa kati ya vibanio hivyo.

Baada ya kujifungua kwa njia ya uke, mtoto mchanga anaweza kulazwa kwa uangalifu juu ya tumbo la mama ili kugusana ngozi kwa ngozi au kufunikwa kwa blanketi ili mama amshike. Baada ya kujifungua kwa upasuaji, ikiwa mzazi mwingine au mtu mwingine anayemsaidia yupo, mtoto mchanga anaweza kupewa mtu huyo amshike. Mama anaweza kumuona mtoto mchanga na baadaye kumbeba mara baada ya upasuaji kukamilika.

Si kila utaratibu wa kujifungua hufuata mpangilio wa kawaida. Kwa mfano, baadhi ya wanawake hupata matatizo ya uchungu na kujifungua. Katika baadhi ya hali, mtoto mchanga huhitaji uangalizi maalum wa kitabibu baada ya kuzaliwa.

Kukata Kiunga Mwana

Muda mfupi baada ya kuzaliwa, vibanio viwili huwekwa kwenye kamba ya kitovu, kisha hukatwa kati yake. Kibano kilicho kwenye kisiki cha kamba kinaweza kuondolewa baada ya kamba kukauka kabisa. Kisiki kinapaswa kuwekwa safi na kikavu. Kisiki huanguka chenyewe baada ya wiki moja au mbili.

Daktari au mkunga humchunguza mtoto mchanga ili kubaini kasoro zozote zilizo wazi au dalili za shida. Uchunguzi kamili wa kimwili hufanyika baadaye, kwa kawaida ndani ya saa 24 baada ya kuzaliwa. Hali ya mtoto mchanga mara tu baada ya kuzaliwa hupimwa dakika ya 1 na dakika ya 5 kwa kutumia . Alama ya Apgar hutumika kupatiana pointi kwa mapigo ya moyo, juhudi za kupumua, toni ya misuli, hisia, na rangi. Alama ya 7 hadi 10 huchukuliwa kuwa ya kawaida, 4 hadi 6 ni ya kati, na 0 hadi 3 ni ya chini. Alama ya chini ya Apgar ni ishara kwamba mtoto aliyezaliwa karibuni ana shida na anaweza kuhitaji usaidizi wa ziada katika kupumua au mzunguko wa damu. Alama ya Apgar haitabiri chochote kuhusu afya ya mtoto baada ya dakika chache za kwanza za maisha.

Jedwali

Mara tu mtoto mchanga anapokuwa imara, wauguzi hupima mduara wa kichwa, uzito na urefu (tazama pia Ukuaji wa Kimwili wa Watoto Wachanga na Watoto).

Kumweka mtoto mchanga katika hali ya joto ni muhimu sana. Haraka iwezekanavyo, mtoto mchanga hufungwa kwa nguo nyepesi na kichwa hufunikwa ili kupunguza upotevu wa joto la mwili.

Mara tu baada ya kuzaliwa, wazazi huhimizwa kumbeba mtoto wao mchanga. Baadhi ya wataalamu wanaamini kuwa mgusano wa mapema wa kimwili husaidia kuanzisha uhusiano wa karibu kati ya mzazi na mtoto. Hata hivyo, wakati mwingine mtoto mchanga huhitaji huduma ya kitabibu au huenda kukawa na sababu nyingine inayochelewesha mgusano na wazazi. Wazazi bado wanaweza kujenga uhusiano mzuri na mtoto hata wasipotangamana saa za kwanza.

Mama na mtoto mchanga kwa kawaida hupumzika pamoja katika chumba cha kujifungulia. Akina mama ambao wananyonyesha humlaza mtoto wao mchanga kwenye titi ndani ya dakika 30 za kwanza baada ya kujifungua. Kunyonyesha huchochea oksitosini, homoni inayosaidia mfuko wa uzazi kupona na kuimarisha uzalishaji wa maziwa. Iwapo mtoto anatunzwa kwenye wodi ya watoto, huwekwa chali kwenye kitanda kidogo na kuwekwa katika hali ya joto.

Baada ya kuzaliwa, daktari au muuguzi hufanya vipimo na kutoa matibabu fulani kwa mtoto ili kugundua na kuzuia magonjwa fulani, ikiwa ni pamoja na yafuatayo:

  • Vipimo vya kawaida vya uchunguzi wa watoto wachanga hufanywa.

  • Kiasi kidogo cha antibiotiki, kama erythromycin, tetracycline, nitrati ya fedha, au katika baadhi ya nchi iodini ya povidone, huwekwa machoni ili kuzuia maambukizi kutokana na vijidudu vyovyote hatari ambavyo huenda mtoto amegusana navyo wakati wa kujifungua.

  • Chanjo ya homa ya ini B ni mojawapo ya chanjo za kawaida zinazopendekezwa kwa watoto wote. Watoto wote wachanga wanapaswa kupewa dozi ya kwanza ya chanjo ya homa ya ini B kabla ya kuruhusiwa kutoka hospitalini.

  • Kwa kuwa watoto huzaliwa na viwango vya chini vya vitamini K, sindano ya vitamini K hutolewa kuzuia kutokwa damu (ugonjwa wa watoto wachanga kutokwa na damu).

Takribani saa 6 au zaidi baada ya kuzaliwa, mtoto mchanga huoshwa. Muuguzi huepuka kuondoa sehemu nyeupe yenye mafuta (vernix caseosa) inayofunikaa ngozi ya mtoto kwa sababu husaidia kulinda dhidi ya maambukizi.