Attention-Deficit/Hyperactivity Disorder (ADHD)

NaStephen Brian Sulkes, MD, Golisano Children’s Hospital at Strong, University of Rochester School of Medicine and Dentistry
Imekaguliwa naAlicia R. Pekarsky, MD, State University of New York Upstate Medical University, Upstate Golisano Children's Hospital
Imepitiwa/Imerekebishwa Apr 2024 | Imebadilishwa Nov 2025
v824905_sw

Ugonjwa wa upungufu wa usikivu/kuongezeka kwa shughuli (ADHD) ni usikivu duni au kwa muda mfupi na/au shughuli nyingi na msukumo usiofaa kwa umri wa mtoto ambao huingilia utendaji au ukuaji.

  • ADHD ni ugonjwa wa ubongo unaotokea tangu kuzaliwa au unaotokea muda mfupi baada ya kuzaliwa.

  • Baadhi ya watoto wana shida kubwa ya kudumisha usikivu, kumakinika, na uwezo wa kukamilisha kazi; baadhi ya watoto huwa na shughuli nyingi kupita kiasi na wana msukumo; na wengine yote mawili.

  • Madaktari hutumia dodoso zilizojazwa na wazazi na walimu pamoja na uchunguzi wa mtoto ili kufanya utambuzi.

  • Dawa za kuchangamsha neva au dawa nyingine pamoja na mazingira yaliyopangwa, utaratibu, mpango wa kuingilia kati shuleni, na mbinu za malezi zilizorekebishwa mara nyingi zinahitajika.

Ugonjwa wa upungufu wa usikivu/kuongezeka kwa shughuli (ADHD) ni aina moja ya ugonjwa wa ukuaji wa neva.

Ingawa kuna utata mkubwa kuhusu idadi ya watoto walioathiriwa, inakadiriwa kuwa ADHD huathiri asilimia 5 hadi 15 ya watoto na ni mara mbili zaidi ya kawaida miongoni mwa wavulana.

Sifa nyingi za ADHD mara nyingi huonekana kabla ya umri wa miaka 4 na mara nyingi kabla ya umri wa miaka 12, lakini huenda zisiathiri pakubwa utendaji wa kitaaluma na utendaji wa kijamii hadi miaka ya shule ya kati.

Hapo awali ADHD iliitwa tatizo la upungufu wa usikivu tu (ADD). Hata hivyo, tukio la kawaida la shughuli nyingi kupita kiasi kwa watoto walioathiriwa—ambalo kwa kweli ni ongezeko la upungufu wa usikivu na msukumo—lilisababisha mabadiliko ya istilahi ya sasa.

ADHD ina aina 3

  • Kutokuwa msikivu

  • Mwenye shughuli nyingi/mwenye msukumo mkubwa

  • Yote mawili

Dalili za ADHD huanzia ndogo hadi kali na zinaweza kuzidishwa au kuwa tatizo katika mazingira fulani, kama vile nyumbani au shuleni. Vikwazo vya shule na mitindo ya maisha iliyopangwa hufanya usimamizi unaofaa wa ADHD kuwa muhimu zaidi. Ingawa baadhi ya dalili za ADHD zinaweza pia kutokea kwa watoto wasio na ADHD, ni za mara kwa mara na kali zaidi kwa watoto walio na ADHD.

Je, Ulijua...

  • Kuongezeka kwa shughuli katika ADHD ni ongezeko la kimwili la upungufu wa usikivu na msukumo.

ADHD kwa watu wazima

Ingawa ADHD inachukuliwa kuwa ugonjwa wa watoto na huanza kipindi cha utotoni, huenda isitambulike hadi kipindi cha ujana au utu uzima. Tofauti za neva huendelea kutokea hadi kipindi cha utu uzima, na takribanii nusu ya watu huendelea kuwa na dalili za tabia katika kipindi cha utu uzima.

Kwa watu wazima, dalili hujumuisha

  • Kushindwa kumakinika

  • Kutatizika kukamilisha kazi (ujuzi duni wa utendaji)

  • Kutokuwa na utulivu

  • Mihemko ya hisia

  • Kutokuwa mvumilivu

  • Kutatizika kudumisha mahusiano

Inaweza ikawa vigumu zaidi kuitambua ADHD wakati wa utu uzima. Dalili zinaweza kufanana na zile za magonjwa ya akili, ikijumuisha matatizo ya hisia na matatizo ya wasiwasi. Watu wazima wanaotumia pombe na dawa za kulevya vibaya wanaweza pia kuwa na dalili zinazofanana. Madaktari huwaomba watu wazima kujaza dodoso ili kugundua ugonjwa wa ADHD, lakini wanaweza pia kuhitaji kukagua rekodi kutoka shuleni ili kuthibitisha mtindo wa kukosa usikivu au msukumo wa ghafla.

Watu wazima walio na ADHD wanaweza kunufaika kwa kutumia aina zilezile za dawa za kusisimua kama watoto walioathiriwa. Wanaweza pia kuhitaji ushauri nasaha ili kuwasaidia kuboresha ujuzi wao wa usimamizi wa muda na kukuza ujuzi mwingine wa kukabiliana na changamoto.

Sababu za ADHD

ADHD haina chanzo kimoja mahususi kinachojulikana, lakini mara nyingi sababu za kijenetiki (vya kurithi) huwa zipo. Utafiti unaonyesha kuwa ADHD huenda inahusisha kasoro katika nyurotransmita (vitu vinavyosambaza ishara za neva ndani ya ubongo). Baadhi ya sababu nyingine za hatari ni pamoja na uzani mdogo wakati wa kuzaliwa (chini ya pauni 3 [gramu 1500]), jeraha la kichwa, maambukizi ya ubongo, upungufu wa madini ya chuma, tatizo la kushindwa kupumua ninapolala na kuathiriwa na madini ya risasi, pamoja na kuathiriwa na pombe, tumbaku, au pengine kokeini kabla ya kujifungua. ADHD pia inahusishwa na matukio ya kiwewe wakati wa utotoni, kwa mfano, vurugu, unyanyasaji, au kutelekezwa.

Baadhi ya watu wameibua wasiwasi kuhusu iwapo viambato vya chakula na sukari vinaweza kusababisha ADHD. Ingawa baadhi ya watoto huonekana kuwa wachangamfu kupita kiasi au kuwa na msukumo wa ghafla baada ya kula vyakula vyenye sukari, tafiti zimethibitisha kwamba tofauti za ubongo zinazosababisha ADHD huwa zipo wakati wa kuzaliwa na kwamba vyakula na sababu za kimazingira hazisababishi ugonjwa huo.

Dalili za ADHD

ADHD kimsingi ni tatizo la kudumisha usikivu, umakinifu, na kuendelea kufanya kazi (uwezo wa kumaliza kazi). Watoto walioathiriwa wanaweza pia kuwa na utendaji wa kupita kiasi na wenye msukumo wa ghafla. Watoto wa chekechea wenye ADHD wanaweza kuwa na matatizo ya mawasiliano na kuonekana kuwa na changamoto za mtagusano wa kijamii. Watoto wanapofikia umri wa kwenda shule, wanaweza kuonekana kama wasiomakinika. Wanaweza kuchezesha miili yao na kujigeuza geuza kwa kukosa utulivu Wanaweza kuwa na msukumo wa ghafla na kuzungumza bila kusubiri zamu yao. Katika kipindi cha baadaye cha utotoni, watoto kama hao wanaweza kusogeza miguu yao bila kutulia, kusogeza na kuchezesha mikono yao, kuzungumza kwa msukumo wa ghafla, na kusahau kwa urahisi, na wanaweza kuwa na mpangilio mbaya. Kwa ujumla si wachokozi.

Dalili zote hazihitaji kuwepo ili kugundua ugonjwa wa upungufu wa makini na utendaji wa kupita kiasi (ADHD). Hata hivyo, dalili 6 au zaidi za kukosa usikivu au za utendaji wa kupita kiasi na msukumo wa ghafla sharti ziwepo kila wakati ili kutambua ugonjwa huu (au 6 kutoka kila kundi ili kutambua aina ya jumla ya ADHD). Dalili ni sharti ziwepo katika mazingira mawili au zaidi (kwa mfano, nyumbani na shuleni) na sharti ziathiri utendaji wa kijamii au kitaaluma.

Dalili za kukosa usikivu:

  • Mara nyingi hukosa kuzingatia kwa makini maelezo madogo.

  • Anatatizika kudumisha usikivu katika kazi na michezo

  • Haonekani kusikiliza anapozungumzwa moja kwa moja

  • Mara nyingi hafuati maagizo na hukosa kumaliza kazi

  • Mara nyingi hutatizika kupanga kazi na shughuli

  • Mara nyingi huepuka, hapendi, au husita kufanya kazi zinazohitaji juhudi endelevu za kiakili

  • Mara nyingi hupoteza vitu

  • Hukengeushwa kwa urahisi na vichocheo vyingine visivyo muhimu

  • Huwa msahaulifu

Dalili za utendaji wa kupita kiasi na msukumo wa ghafla:

  • Mara nyingi huchezesha mikono au miguu au hujigeuzageuza kwa kukosa utulivu

  • Mara nyingi huondoka kwenye kiti darasani na sehemu nyingine

  • Mara nyingi hukimbia au kukwea juu ya vitu kupita kiasi

  • Anatatizika kucheza au kushiriki katika shughuli za burudani kwa utulivu

  • Mara nyingi huwa anatembeatembea au kama “anaendeshwa na injini”

  • Mara nyingi huzungumza kupita kiasi

  • Mara nyingi hujibu maswali kwa ghafla kabla maswali hayajakamilika

  • Mara nyingi hutatizika kusubiri zamu yake

  • Mara nyingi hukatiza au kuingilia shughuli za wengine

Takribani asilimia 20 hadi 60 ya watoto wenye ADHD wana ulemavu wa kujifunza unaoathiri stadi ya kusoma, hisabati, au lugha ya maandishi na wengi wana matatizo ya kitaaluma kama vile alama duni kutokana na kukosa mpangilio au kutokamilisha kazi za ziada (ujuzi wa utendaji). Kazi inaweza kuwa isiyo na mpangilio, ikiwa na makosa ya kizembe na ukosefu wa mawazo ya kina. Watoto walioathiriwa mara nyingi hutenda kana kwamba akili zao zipo mahali pengine na hawasikilizi. Mara nyingi hawatekelezi maombi au kukamilisha kazi za shule, kazi za ziada, au majukumu mengine. Kunaweza kuwa na mabadiliko ya mara kwa mara kutoka kazi moja ambayo haijakamilika hadi nyingine.

Watoto walioathiriwa wanaweza kuwa na matatizo ya kujithamini, unyogovu, wasiwasi, au upingaji wa mamlaka kufikia wakati wa kipindi cha ujana. Takribani asilimia 60 ya watoto wadogo wana matatizo kama vile tatizo la hasira kali, na watoto wakubwa wengi wana uvumilivu mdogo kwa hali za kukatisha tamaa.

Utambuzi wa ADHD

  • Tathmini ya daktari

Utambuzi wa ADHD hutegemea idadi, mara zinapotokea, na ukali wa dalili. Watoto ni sharti wawe na dalili 6 au zaidi za kukosa usikivu au za utendaji wa kupita kiasi na msukumo wa ghafla (au 6 kutoka kila kundi ili kutambua aina ya jumla ya ADHD; tazama Dalili za ADHD). Dalili ni sharti ziwepo katika angalau mazingira mawili tofauti (kwa kawaida, nyumbani na shuleni) ili mwitikio wa mtoto kwa matatizo maalum katika hali moja yasidhaniwe kimakosa kuwa ADHD. Kutokea kwa dalili nyumbani au shuleni pekee na mahali pengine popote hakustahili kuitwa ADHD kwa sababu dalili hizo zinaweza kusababishwa na hali maalum ya mazingira hayo. Dalili sharti pia ziwe dhahiri zaidi kuliko inavyotarajiwa kwa kiwango cha ukuaji wa mtoto na sharti ziwepo kwa kipindi cha miezi 6 au zaidi. Mara nyingi, utambuzi huwa mgumu kwa sababu unategemea uamuzi wa mtu anayemchunguza mtoto. Pia, watoto ambao kimsingi tatizo lao kuu ni kukosa usikivuwanaweza kutoonekana kuwa na tatizo hadi utendaji wao wa masomo uanze kuathirika vibaya.

Hakuna kipimo cha maabara cha kutambua ADHD. Madodoso kuhusu vipengele mbalimbali vya tabia na ukuaji yanaweza kuwasaidia madaktari na wanasaikolojia kufanya utambuzi. Kwa sababu matatizo ya kujifunza ni ya kawaida, watoto wengi hufanyiwa vipimo vya kisaikolojia ili kusaidia kubaini kama ADHD ipo na kugundua uwepo wa tatizo mahususi la kujifunza, iwe kama chanzo cha kukosa usikivu au kama tatizo linaloambatana nayo.

Uchunguzi wa mwili na wakati mwingine vipimo mbalimbali vya damu na vingine ili kuondoa uwezekano wa magonjwa mengine pia hufanywa.

Idadi inayoongezeka ya watoto wanatambuliwa kuwa na tatizo la upungufu wa usikivu/utendaji kupita kiasi (ADHD). Hata hivyo, kuna wasiwasi miongoni mwa madaktari na wazazi kwamba watoto wengi wanatambuliwa kimakosa kuwa na ugonjwa huo. Kiwango cha juu cha shughuli kinaweza kuwa cha kawaida kabisa na ni kuzidisha tu tabia ya kawaida ya kipindi cha utotoni. Vinginevyo, inaweza kuwa na sababu mbalimbali, ikiwa ni pamoja na matatizo ya kihisia au matatizo ya utendaji wa ubongo, kama vile ADHD.

Kwa ujumla, watoto wa miaka 2 wana shughuli nyingi na mara chache hukaa kimya. Kiwango cha juu cha shughuli na kelele ni cha kawaida hadi kufikia umri wa miaka 4. Katika makundi haya ya umri, na kwa watoto wanaokua kimaendeleo kulingana na umri huu, tabia hiyo ni ya kawaida. Tabia ya kuwa na utendaji wa shughuli nyingi inaweza kusababisha migogoro kati ya wazazi na mtoto na inaweza kuwatia wasiwasi wazazi. Pia inaweza kusababisha matatizo kwa wengine wanaowasimamia watoto kama hao, wakiwemo walimu.

Kubaini kama kiwango cha utendaji wa shughuli wa mtoto ni cha juu isivyo kawaida hakupaswi kutegemea tu uvumilivu wa mtu aliyekasirika. Hata hivyo, ni dhahiri kuwa baadhi ya watoto wana utendaji wa shughuli nyingi zaidi kuliko kiwango cha wastani. Ikiwa kiwango cha juu cha utendaji wa shughuli kinajumuishwa pamoja na tatizo la usikivu kwa kipindi cha muda mfupi na msukumo wa ghafla, kinaweza kufafanuliwa kama utendaji wa kupita kiasi na kuchukuliwa kuwa sehemu ya ADHD.

Kuwakemea na kuwaadhibu watoto kwa kuwa na utendaji wa kiwango cha juu wa shughuli kwa kawaida huleta matokeo yasiyotarajiwa, na kuongeza kiwango cha utendaji wa shughuli wa mtoto. Kuepuka hali ambazo mtoto analazimika kuketi bila kusonga kwa muda mrefu au kumpata mwalimu mwenye ujuzi wa kushughulikia watoto kama hao kunaweza kusaidia. Ikiwa hatua rahisi hazisaidii, tathmini ya kitabibu au kisaikolojia inaweza kuwa muhimu ili kuondoa tatizo la msingi kama vile ADHD.

Matibabu ya ADHD

  • Dawa za kusisimua ubongo

  • Marekebisho ya tabia

Mapendekezo ya matibabu kwa watoto wenye ADHD hutofautiana kulingana na umri:

  • Watoto wa umri wa shule ya chekechea: Matibabu ya awali ni tiba ya tabia. Dawa zinaweza kuzingatiwa ikiwa mwitikio wa mikakati ya kitabia haitoshi au ikiwa dalili ni za wastani hadi kali.

  • Watoto wa umri wa kwenda shule: Matibabu ya awali ni tiba ya kitabia pamoja na dawa.

Sheria ya Elimu ya Watu Wenye Ulemavu ya Serikali Kuu (IDEA) inahitaji shule za umma kutoa elimu bila malipo na inayofaa kwa watoto na vijana wenye ADHD. Elimu ni sharti itolewe katika mazingira yasiyo na vikwazo vingi na yaliyo jumuishi zaidi—yaani, mazingira ambayo watoto wanapata fursa zote za kushirikiana na wenzao wasio na ulemavu na wana ufikiaji sawa wa rasilimali za jamii. Sheria ya Wamarekani Wenye Ulemavu na Kifungu cha 504 cha Sheria ya Urekebishaji pia huhakikisha kuwa wanajumuishwa katika shule na maeneo mengine ya umma.

Tiba ya dawa

Dawa za kusisimua ubongo ndizo tiba ya dawa yenye ufanisi zaidi. Methylphenidate na dawa nyingine zinazofanana na amphetamine ndizo dawa za kusisimua ubongo zinazoagizwa na daktari mara nyingi zaidi. Zina ufanisi sawa na zina madhara yanayofanana. Dawa kadhaa zinazotoa dawa polepole (zinazofanya kazi kwa muda mrefu) zinapatikana pamoja na aina za kawaida, na huruhusu matumizi ya dozi mara moja kwa siku na zinaweza kusaidia kuzuia matumizi yasiyofaa.

Madhara ya dawa za kusisimua ubongo yanaweza kujumuisha

  • Matatizo ya kulala (kama vile kukosa usingizi)

  • Kupungua kwa hamu ya kula

  • Maumivu ya kichwa

  • Maumivu ya tumbo

  • Kuongezeka kwa mapigo ya moyo na shinikizo la damu

  • Unyogovu, huzuni, au wasiwasi

Watoto wengi hawana madhara yoyote isipokuwa labda kupungua kwa hamu ya kula. Madhara yote hutoweka wakati mtu anaacha kutumia dawa. Hata hivyo, zinapotumiwa kwa dozi kubwa kwa kipindi cha muda mrefu, dawa za kusisimua zinaweza kupunguza ukuaji wa watoto, na ukuaji huu uliopungua unaweza kuendelea hadi kipindi cha utu uzima, kwa hivyo madaktari hufuatilia uzani na kimo. Ikiwa watoto wanakua polepole au wana madhara mengine makubwa, madaktari wanaweza kushauri "kuacha kutumia dawa kwa kipindi cha muda fulani." Kuacha kutumia dawa kwa kipindi cha muda fulani ni kusitisha utumiaji wa dawa za kusisimua wakati ambapo watoto hawahitaji kuwa makini sana, kwa mfano wikendi au wakati wa likizo za shule. Hata hivyo, baadhi ya watoto hutatizika sana kufanya kazi hata nje ya mazingira ya shule na huenda wasiweze kuvumilia kuacha kutumia dawa kwa kipindi cha muda fulani.

Dawa nyingine kadhaa zinaweza tatizo la kukosa usikivu na dalili za kitabia. Dawa hizi zinajumuisha

  • Atomoxetine (dawa ya ADHD isiyo ya kusisimua)

  • Baadhi ya dawa ambazo kwa kawaida hutumika kutibu shinikizo la juu la damu kama vile clonidine na guanfacine

  • Dawa za kuzuia msongo wa mawazo

  • Dawa za kupunguza wasiwasi

Wakati mwingine, mchanganyiko wa dawa hutumika.

Udhibiti wa tabia

Ili kupunguza athari za ADHD, majengo, ratiba, mpango wa mikakati ya shule, na mbinu za malezi zilizorekebishwa mara nyingi huhitajika. Watoto wasio na changamoto kubwa za tabia wanaweza kunufaika kutokana na matibabu ya dawa pekee. Hata hivyo, dawa za kusisimua hazifanyi kazi muda wote, hivyo basi marekebisho yanaweza kuhitajika ili kusaidia katika ujuzi wa kupanga mambo na ujuzi mwingine. Tiba ya kitabia inayotolewa na mwanasaikolojia wa watoto wakati mwingine hujumuishwa na matibabu ya dawa.

Ubashiri wa ADHD

Muhimu zaidi, idadi kubwa ya watoto wenye ADHD hukua na kuwa watu wazima wabunifu na wenye tija, na watu walio na ADHD wanaweza kuzoea mazingira ya kazi vizuri zaidi kuliko mazingira ya shule. Hata hivyo, ikiwa ugonjwa huo hautatibiwa utotoni, hatari ya matumizi mabaya ya pombe au dawa za kulevya au kujiua inaweza kuongezeka.

Watoto wenye ADHD kwa ujumla hawaachi kuwa na tatizo la kukosa usikivu kadri anavyokua kiumri, ingawa watoto wenye utendaji wa kupita kiasi huwa wanapunguza kwa kiasi msukumo wa ghafla na utendaji wa kupita kiasi kadri wanavyokua. Hata hivyo, vijana na watu wazima wengi hujifunza kuzoea tatizo lao la kukosa usikivu. Takribani theluthi moja ya watu hugundua kuwa wanaendelea kunufaika kutokana na matumizi ya dawa za kusisimua.

Matatizo mengine ambayo yanaweza kujitokeza au kuendelea kutokea katika kipindi cha ujana na utu uzima ni pamoja na matokeo duni shuleni, ukosefu wa ajira, matumizi mabaya ya dawa za kulevya, ajali za magari, mahusiano yasiyo imara, kutokuwa na mpangilio (inayojulikana kama ujuzi duni wa utendaji), kutojithamini, wasiwasi, unyogovu na kutatizika kujifunza tabia zinazofaa kijamii.

Taarifa Zaidi

Nyenzo zifuatazo za lugha ya Kiingereza zinaweza kuwa muhimu. Tafadhali kumbuka kuwa MWONGOZO hauwajibiki kwa maudhui ya nyenzo hizi.

  1. Shirika Linaloshughulikia Tatizo la Upungufu wa Usikivu (ADDA): Shirika linalotoa rasilimali kwa watu wazima wenye ADHD

  2. Watoto na Watu Wazima Wenye Tatizo la Upungufu wa Usikivu/Utendaji wa Kupita Kiasi (CHADD): Shirika linalotoa rasilimali za kielimu, msaada, na matibabu kwa watu wote wenye ADHD

  3. Shirika Linalotoa Msaada kwa Walemavu wa Kujifunza Nchini Amerika (LDA): Shirika linalotoa rasilimali za kielimu, usaidizi, na utetezi kwa watu wenye ulemavu wa kujifunza

  4. Sheria ya Elimu ya Watu Wenye Ulemavu (IDEA): Sheria ya Marekani inayotoa elimu ya umma mwafaka bila malipo kwa watoto wenye ulemavu wanaostahiki na kuhakikisha elimu maalum na huduma zinazohusiana kwa watoto hao

  5. Sheria ya Wamarekani wenye Ulemavu: Sheria ya Marekani inayokataza ubaguzi unaotokana na ulemavu

  6. Kifungu cha 504 cha Sheria ya Urekebishaji: Sheria ya Marekani inayohakikisha haki fulani kwa watu walio na ulemavu