Watoto wachanga wenye afya njema wanapaswa kuonwa na daktari wao mara kwa mara katika mwaka wa kwanza wa maisha. Ziara za huduma ya kinga ya afya (pia huitwa ziara za ustawi wa mtoto) kwa kawaida hufanyika ndani ya siku chache baada ya kuzaliwa au umri wa wiki 2 na akiwa na umri wa miezi 1, 2, 4, 6, na 9. Wakati wa ziara hizi, daktari hutumia miongozo mahususi ya umri ili kufuatilia ukuaji na maendeleo ya mtoto na kuwauliza wazazi maswali kuhusu hatua mbalimbali za ukuaji (tazama jedwali ). Vipimo wakati mwingine hufanywa, na katika ziara nyingi, daktari humpatia mtoto chanjo dhidi ya magonjwa mbalimbali (tazama Ratiba ya Chanjo za Utotoni).
Ziara za huduma ya afya pia humruhusu daktari kuwaelimisha wazazi kuhusu kula, kulala, tabia, usalama wa mtoto, lishe, mazoezi, na tabia njema za kiafya. Zaidi ya hayo, daktari huwaeleza wazazi mabadiliko ya ukuaji wa mtoto wao yanayotarajiwa kufikia ziara inayofuata.
Uchunguzi
Urefu na kimo cha mtoto, uzito, na mzingo wa kichwa vitapimwa katika kila ziara. Daktari anamchunguza mtoto mchanga kwa kasoro mbalimbali, ikiwa ni pamoja na dalili za matatizo ya kurithi au kasoro za kuzaliwa.
Macho huchunguzwa, na uoni hupimwa. Watoto wachanga waliozaliwa kabla ya wakati (kabla ya kukamilika kwa wiki 32 za ukuaji ndani ya uterasi) kwa kawaida wanahitaji uchunguzi wa macho wa mara kwa mara na mtaalamu wa macho ili kuangalia retina isiyokomaa iitwayo retinopathy of prematurity, ambayo ni ugonjwa wa macho unaotokea pale watoto wachanga wanapozaliwa kabla ya mishipa ya damu machoni mwao kukua kikamilifu na inaweza kusababisha upofu, na kwa ajili ya utokeaji wa hitilafu za kuakisi mwanga, ambazo husababisha kufifia kwa uwezo wa kuona. Matatizo haya ni ya kawaida zaidi miongoni mwa watoto wachanga waliozaliwa kabla ya wakati.
Daktari hukagua nyonga za mtoto mchanga kwa ajili ya dalili kama viungo vya nyonga vimelegea au vimeteguka (displasia ya ukuaji wa nyonga). Daktari hukagua meno ya mtoto, ikiwa yapo, kwa ajili ya mashimo na kinywa kwa ajili ya ukungu, ambayo ni maambukizi ya kawaida ya chachu (fangasi) miongoni mwa watoto wachanga.
Daktari pia huchunguza moyo, mapafu, tumbo, mikono na miguu, na sehemu za siri.
Uchunguzi
Vipimo vya uchunguzi hufanywa ili kutathmini kama watoto wachanga wako katika hatari ya kupata matatizo fulani.
Vipimo vya damu hufanywa ili kugundua anemia, ugonjwa wa selimundu, na kuwepo kwa madini ya risasi.
Vipimo vya uwezo wa kusikia hufanywa muda mfupi baada ya kuzaliwa ili kubaini kama mtoto mchanga ana tatizo la kusikia au kupoteza uwezo wa kusikia (tazama Vipimo vya Uchunguzi wa Watoto Wachanga) na hurudiwa baadaye ikiwa wasiwasi mpya utatokea kuhusu usikivu wa mtoto mchanga (tazama pia Usikivu Hafifu kwa Watoto).
Watoto wachanga huchunguzwa vigeozo hatarishi vya kifua kikuu (TB) kwa kutumia dodoso katika ziara zote za ustawi wa mtoto, kwa kawaida kuanzia utotoni. Vigezo hatarishi ni pamoja na mazingira ya kuambukizwa TB, kuzaliwa au kusafiri katika maeneo ya dunia ambayo TB imeenea (nchi zingine tofauti na Marekani, Kanada, Australia, na New Zealand na nchi za Magharibi na Kaskazini mwa Ulaya), kuwa na mwanafamilia mwenye TB, na kuwa na wazazi au watu wa karibu ambao ni wahamiaji wa hivi karibuni kutoka maeneo ambayo TB imeenea au ndugu ambaye alikuwa gerezani hivi karibuni. Wale walio na vigezo hatarishi kwa kawaida hufanyiwa vipimo vya uchunguzi wa kifua kikuu.
Usalama
Katika ziara hizi, daktari huwapa wazazi miongozo ya usalama inayolingana na umri.
Miongozo ya usalama ifuatayo inatumika kwa watoto wachanga kuanzia kuzaliwa hadi umri wa miezi 12:
Tumia kiti cha gari kinachotazama nyuma na ukiweke kwenye kiti cha nyuma cha gari.
Seti hita ya maji ya moto katika nyuzi joto 120 Farenhaiti au chini ya hapo.
Zuia uangukaji kutokana na kubadilisha meza na karibu na ngazi.
Laza watoto wachanga chali kwenye godoro imara na tambarare kwa kila walalapo usingizi, usishiriki nao kitanda kimoja, na usiweke mito, magodoro ya pembezoni mwa kitanda, mashuka yasiyotoshea, midoli ya wanyama au vitu vya kuchezea, mashuka yenye matabaka, vifariji, au blanketi zenye uzito au zilizolegea kwenye kitanda cha mtoto. (Tazama pia upau wa pembeni Salama kwa Kulala: Kupunguza Hatari ya Kifo cha Ghafla kwa Mtoto (SIDS).)
Usiwape watoto wachanga vyakula na vitu vinavyoweza kusababisha kukosa pumzi au kuvivuta kwa pumzi hadi kwenye mapafu.
Usitumie vifaa vya kutembelea watoto.
Weka komeo za usalama kwenye makabati na funika soketi za umeme.
Kuwa macho unapowaangalia watoto wachanga kwenye beseni la maji au karibu na bwawa la kuogelea au maji yoyote na pale wanapojifunza kutembea.
Image courtesy of the Centers for Disease Control and Prevention (CDC), National Center for Injury Prevention and Control (Transportation Safety Resources). This guidance from the CDC is for the United States, and regulations may differ in other countries.
Image courtesy of the Centers for Disease Control and Prevention (CDC), National Center for Injury Prevention and Control (Transportation Safety Resources). This guidance from the CDC is for the United States, and regulations may differ in other countries.
Image courtesy of the Centers for Disease Control and Prevention (CDC), National Center for Injury Prevention and Control (Transportation Safety Resources). This guidance from the CDC is for the United States, and regulations may differ in other countries.
Image courtesy of the Centers for Disease Control and Prevention (CDC), National Center for Injury Prevention and Control (Transportation Safety Resources). This guidance from the CDC is for the United States, and regulations may differ in other countries.
Lishe na mazoezi
Kwa watoto wachanga, mapendekezo ya lishe yanategemeana na umri. Daktari anaweza kuwasaidia wazazi kupima faida za kunyonyesha dhidi ya kumpa maziwa ya fomula na kutoa mwongozo kuhusu vyakula vigumu.
Wazazi wanapaswa kuwapa watoto wachanga mazingira salama ambayo wanaweza kuzurura na kuchunguza. Michezo ya nje inapaswa kupewa nafasi tangu utotoni.
Muda wa kutazama skrini (kwa mfano, televisheni, michezo ya video, simu za mkononi na vifaa vingine vya mkononi, na muda usio wa kielimu wa kompyuta) unaweza kusababisha kutoshughulisha mwili na unene kupita kiasi. Udhibiti wa muda ambao mtoto hutumia vifaa vya skrini unapaswa kuanzia wakati wa kuzaliwa na kudumishwa katika ujana wake wote.