Ziara zilizopangwa za kuonana na daktari (pia huitwa ziara za ustawi wa mtoto) huwapa wazazi taarifa kuhusu ukuaji na maendeleo ya mtoto wao. Ziara kama hizo pia huwapa wazazi fursa ya kuuliza maswali na kuomba ushauri, kwa mfano, kuhusu mafunzo ya kutumia choo.
Chuo cha Marekani cha Matibabu ya Watoto kinapendekeza kwamba baada ya mwaka wa kwanza wa maisha watoto wanapaswa kumuona daktari wao kwa ziara za huduma ya kinga ya afya wakiwa na umri wa miezi 12, 15, 18, 24, na 30 na kisha kila mwaka hadi umri wa miaka 10. Ziara zinaweza kufanywa mara nyingi zaidi kulingana na ushauri wa daktari au mahitaji ya familia.
Uchunguzi
Katika kila ziara, vipimo kadhaa huchukuliwa, taratibu za uchunguzi hufanywa, na chanjo hutolewa kulingana na ratiba.
Urefu na uzito hupimwa, na mzingo wa kichwa hupimwa hadi mtoto atakapofikisha miezi 36. Ukuaji mzuri ni kiashiria kimoja kwamba mtoto kwa ujumla ana afya njema. Ukubwa halisi wa umbo la mtoto si muhimu zaidi ya vile mtoto anabakia katika asilimia au karibu na asilimia sawa na kwenye chati ya urefu na uzito katika kila ziara. Mtoto ambaye kila wakati huwa katika asilimia ya 10 anaweza kuwa sawa (ingawa ni mdogo kuliko watoto wengi wa umri huo), ilhali mtoto anayeporomoka kutoka asilimia ya 35 hadi ya 10 anaweza kuwa na tatizo la kiafya.
Kuanzia umri wa miaka 3, shinikizo la damu litapimwa katika kila ziara.
Daktari pia hufuatilia jinsi mtoto alivyoendelea kiukuaji (tazama Ukuaji wa Mtoto) tangu ziara ya mwisho. Kwa mfano, daktari anaweza kutaka kujua kama mtoto wa miezi 18 ameanza kuzungumza au kama mtoto wa miaka 6 ameanza kusoma maneno machache (tazama jedwali ). Vivyo hivyo, madaktari mara nyingi huuliza maswali yanayolingana na umri kuhusu tabia ya mtoto. Je, mtoto wa miezi 18 ana hasira kali? Je, mtoto wa miaka 2 analala usiku kucha? Je, mtoto wa miaka 6 anakojoa kitandani usiku? Wazazi na madaktari wanaweza kujadili aina hizi za masuala ya kitabia na ukuaji wakati wa ziara za huduma ya kinga ya afya na kwa pamoja kubuni mbinu za kushughulikia masuala yoyote.
Hatimaye, daktari hufanya uchunguzi kamili wa mwili. Mbali na kumchunguza mtoto kuanzia kichwani hadi kwenye vidole vya miguu, ikiwa ni pamoja na moyo, mapafu, tumbo, sehemu za siri, uti wa mgongo, mikono, miguu, kichwa, shingo, macho, masikio, pua, mdomo, na meno, daktari anaweza kutaka mtoto afanye kazi zinazolingana na umri wake. Ili kuangalia ujuzi wa jumla wa misuli (kama vile kutembea na kukimbia), daktari anaweza kumwambia mtoto wa miaka 4 aruke kwa mguu mmoja. Ili kuangalia ujuzi mzuri wa misuli (kuchezesha vitu vidogo kwa mikono), mtoto anaweza kuulizwa achore picha au kunakili maumbo fulani.
Uchunguzi
Ziara za kinga zinapaswa kujumuisha ukaguzi wa uoni na usikivu. Uchunguzi wa uoni unaweza kuanza akiwa na umri wa miaka 3, ikiwa watoto wanaweza kutoa ushirikiano, lakini inashauriwa akiwa na umri wa miaka 4 na 5. Wazazi wanapaswa kumjulisha daktari kabla ya umri huo ikiwa wana wasiwasi wowote kuhusu uwezo wa kuona wa mtoto wao. Katika umri huu, vipimo vya uoni vinajumuisha matumizi ya chati na mashine za kupimia.
Vipimo vya uwezo wa kusikia, baada ya upimaji wa mtoto mchanga, kwa kawaida huanza akiwa na umri wa miaka 4, lakini wazazi wanapaswa kumjulisha daktari kabla ya hapo ikiwa wana wasiwasi wowote kuhusu usikivu wa mtoto wao.
Baadhi ya watoto wanaweza kuhitaji kuchunguzwa damu yao dhidi ya anemia au kiwango kilichoongezeka cha risasi.
Watoto walio katika hatari ya kuwa na kiasi cha juu cha lehemu wanapaswa kufanya kipimo cha damu kati ya umri wa miaka 2 na 10. Watoto walio katika hatari ni pamoja na wale ambao wana historia ya familia yenye viwango vya juu vya lehemu, mshtuko wa moyo, au kiharusi au wana sababu za hatari za ugonjwa wa moyo (kwa mfano, kisukari, unene kupita kiasi, au shinikizo la damu). Watoto wote wanapaswa kufanya kipimo cha lehemu wakiwa na umri wa miaka 9 hadi 11 na tena wakiwa na umri wa miaka 17 hadi 21.
Watoto huchunguzwa vigezo hatarishi vya kifua kikuu (TB) kwa kutumia dodoso katika ziara zote za ustawi wa mtoto. Vigezo hatarishi ni pamoja na mazingira ya kuambukizwa TB, kuzaliwa au kusafiri katika maeneo ya dunia ambayo TB imeenea (nchi zingine tofauti na Marekani, Kanada, Australia, na New Zealand na nchi za Magharibi na Kaskazini mwa Ulaya), kuwa na mwanafamilia mwenye TB, na kuwa na wazazi au watu wa karibu ambao ni wahamiaji wa hivi karibuni kutoka maeneo ambayo TB imeenea au ndugu ambaye alikuwa gerezani hivi karibuni. Wale walio na vigezo hatarishi kwa kawaida hufanyiwa vipimo vya uchunguzi wa kifua kikuu.
Umri wa mtoto na mambo mengine mbalimbali yataamua kama vipimo vingine vitafanywa.
Usalama
Usalama wa mtoto hujadiliwa wakati wa ziara za kinga. Masuala mahususi ya usalama yanategemea umri wa mtoto. Kwa mfano, majadiliano yanaweza kulenga usalama wa baiskeli kwa mtoto wa miaka 6. Mifano ifuatayo ya kuzuia kuumia inatumika kwa watoto wenye umri wa miezi 12 hadi miaka 4:
Tumia kiti cha gari kinacholingana na umri na uzito. (Watoto wachanga na watoto wadogo wanapaswa kusafiri wakiwa wamekaa kwa kutazama nyuma hadi watakapokua zaidi ya uzito au urefu wa kukaa kutazama nyuma wa kiti cha gari kinachoweza kugeuzwa. Viti vya gari vinavyoweza kugeuzwa vina kikomo ambacho kitawaruhusu watoto wengi kusafiri wakiwa wametazama nyuma hadi umri wa miaka 2. Mara tu wanapofikisha umri wa miaka 2 au, bila kujali umri, wamepita ukubwa wa kiti chao cha gari kinachotazama nyuma, watoto wadogo wanapaswa kukaa katika kiti cha gari kinachotazama mbele wakiwa na mikanda kwa muda mrefu iwezekanavyo kulingana na kikomo cha uzito na urefu.)
Weka viti vya gari kwenye kiti cha nyuma cha gari.
Pitia usalama wa gari kama abiria na kama mtembea kwa miguu.
Funga kamba za dirisha ili kuepuka kunyonga shingo.
Tumia vifuniko va usalama na komeo.
Zuia kuanguka.
Ondoa bunduki nyumbani.
Wasimamie watoto kwa karibu ukiwa ndani ya maji au karibu na maji yoyote (kwa mfano, beseni la maji au bafu, mabwawa, spa, mabwawa ya kucheza watoto, madimbwi, mitaro ya umwagiliaji, au maji mengine yoyote yaliyotuama). Watoto wenye umri wa mwaka 1 na zaidi wanapaswa kuwa na masomo ya kuogelea na wanapaswa kuvaa koti la kuokoa maisha wakati wa kuogelea na wakati wote wakiwa ndani ya boti.
Image courtesy of the Centers for Disease Control and Prevention (CDC), National Center for Injury Prevention and Control (Transportation Safety Resources). This guidance from the CDC is for the United States, and regulations may differ in other countries.
Image courtesy of the Centers for Disease Control and Prevention (CDC), National Center for Injury Prevention and Control (Transportation Safety Resources). This guidance from the CDC is for the United States, and regulations may differ in other countries.
Image courtesy of the Centers for Disease Control and Prevention (CDC), National Center for Injury Prevention and Control (Transportation Safety Resources). This guidance from the CDC is for the United States, and regulations may differ in other countries.
Image courtesy of the Centers for Disease Control and Prevention (CDC), National Center for Injury Prevention and Control (Transportation Safety Resources). This guidance from the CDC is for the United States, and regulations may differ in other countries.
Mbali na zile zilizoorodheshwa hapo juu, mifano ifuatayo ya kuzuia majeraha inatumika kwa watoto wa miaka 5 na zaidi:
Tumia kiti cha gari kinachotazama mbele chenye mkanda kwa muda mrefu iwezekanavyo (mpaka watoto wapite uzito au urefu wa kiti cha gari) na kisha tumia kiti cha busta ya kuweka mkanda hadi mkanda wa kiti cha gari utoshee vizuri (kawaida watoto wanapokuwa wamefikia urefu wa futi 4 na inchi 9 na wana umri wa kati ya miaka 8 na 12).
Watoto walio chini ya umri wa miaka 13 wakae kiti cha nyuma cha gari wakiwa wamefunga mkanda.
Ikiwa gari halina kiti cha nyuma, zima mfuko wa hewa kwenye kiti cha mbele cha abiria.
Watoto wavae kofia ya baiskeli na vifaa vya michezo vya kujikinga.
Waelekeze watoto kuhusu njia salama za kuvuka barabara.
Wasimamie kwa karibu wakiwa wanaogelea na wakati mwingine watoto wavae koti la kuokoa maisha wakati wa kuogelea na kila wakati wakiwa ndani ya boti.
Daktari anaweza pia kusisitiza mada zingine za usalama, kama vile umuhimu wa kufunga na kutunza kengele za moshi na kuweka vitu vinavyoweza kuwa sumu (kama vile visafishaji na dawa) na silaha za moto (bunduki) mbali na watoto. Wazazi wanapaswa kutumia fursa hiyo kuibua mada zinazohusiana zaidi na hali/mazingira ya kipekee ya familia yao. Kadiri watoto wanavyokua, wanaweza kuwa washiriki hai katika mijadala hii.
Lishe na mazoezi
Wazazi wanaweza kusaidia kuzuia unene kupita kiasi na kisukari aina ya 2 kwa kuanzisha mifumo bora ya ulaji na kukuza tabia ya mazoezi ya mara kwa mara. Wazazi wanapaswa kuwapa watoto vyakula mbalimbali vyenye afya, ikiwa ni pamoja na matunda na mboga-mboga pamoja na vyanzo vya protini. Milo ya kawaida na vitafunio vidogo vyenye lishe huchochea ulaji mzuri hata kwa mtoto wa shule ya awali mwenye kuchagua vyakula. Ingawa watoto wanaweza kukwepa baadhi ya vyakula vyenye afya, kama vile brokoli au maharagwe, kwa muda fulani, ni muhimu kuendelea kuwapa vyakula vyenye afya. Zaidi ya hayo, wazazi wanapaswa kupunguza juisi za matunda kwa mtoto, ambazo, licha ya asili yake kuonekana kuwa na afya njema, kimsingi ni maji ya sukari. Baadhi ya watoto hupoteza hamu yao ya kula wakati wa chakula ikiwa wanakunywa juisi nyingi ya matunda. Wazazi wanapaswa kuwaongoza watoto kuepuka kula vitafunwa mara kwa mara na vyakula vyenye kalori nyingi, chumvi, na sukari.
Kufanya mazoezi na kudumisha afya njema ya mwili na hisia ni muhimu sana kwa watoto. Kucheza nje na familia au kushiriki katika timu ya riadha ni njia nzuri ya kuwajenga watoto kufanya mazoezi na kuzuia unene kupita kiasi.
Muda wa kutazama skrini (kwa mfano, televisheni, michezo ya video, simu za mkononi na vifaa vingine vya mkononi, na muda usio wa kielimu wa kompyuta) unaweza kusababisha kutoshughulisha mwili na unene kupita kiasi. Udhibiti wa muda ambao mtoto hutumia vifaa vya skrini unapaswa kuanzia wakati wa kuzaliwa na kudumishwa katika ujana wake wote.