Uchunguzi wa Fupanyonga

NaShubhangi Kesavan, MD, Cleveland Clinic Learner College of Medicine, Case Western Reserve University
Imekaguliwa naOluwatosin Goje, MD, MSCR, Cleveland Clinic, Lerner College of Medicine of Case Western Reserve University
Imepitiwa/Imerekebishwa Apr 2024 | Imebadilishwa Jun 2024
v8497025_sw

Lengo la uchunguzi wa fupanyonga ni kuchunguza sehemu zote za anatomia ya uzazi ya mwanamke. Ikiwa mwanamke atafanyiwa uchunguzi wa fupanyonga au la, uamuzi wa pamoja unapaswa kufanywa kati ya mwanamke na daktari wake au mtaalamu mwingine wa afya. (Angalia pia Chuo cha Madaktari wa Uzazi na Wanajinakolojia wa Marekani (ACOG): Vipimo vya Fupanyonga—Maswali Yanayoulizwa Sana.)

Ikiwa mwanamke ana maswali au wasiwasi wowote kuhusu uchunguzi wa fupanyonga, anapaswa kuzungumza na daktari wake. Wanawake ambao hawajawahi kufanyiwa uchunguzi wa fupanyonga wanapaswa kumuuliza daktari amuelezee kinachoendelea wakati wa uchunguzi huo. Ikiwa sehemu yoyote ya uchunguzi husababisha maumivu, mwanamke anapaswa kuhimizwa kumfahamisha daktari wakati wa uchunguzi.

Uchunguzi wa fupanyonga hufanywa

Wanawake wanapaswa kuzungumza na mtaalamu wao wa afya kuhusu kama na mara ngapi uchunguzi wa fupanyonga unahitaji kufanywa. Mwanamke hahitaji uchunguzi wa fupanyonga kabla ya kuanza kutumia njia mpya ya upangaji wa uzazi, isipokuwa kifaa cha kuingizwa kwenye uterasi. Uchunguzi wa fupanyonga si njia ya kuaminika kila mara kama njia ya kugundua kansa ya ovari.

Katika umri wa miaka 21 hadi 25, wanawake wengi wanapaswa kuanza kufanyiwa vipimo vya uchunguzi wa saratani ya mlango wa kizazi, kama vile kipimo cha Papanicolaou (Pap) na/au kipimo cha virusi vya papiloma vya binadamu (HPV). Kwa kawaida vipimo vya uchunguzi hufanywa kila baada ya miaka 3 hadi 5, kulingana na umri wa mtu, aina ya kipimo, vipengele vya hatari ya saratani ya mlango wa kizazi na matokeo ya vipimo vya awali.

Uchunguzi wa fupanyonga unajumuisha yafuatayo:

Anatomia ya Uzazi wa Mwanamke wa Nje

Anatomia ya Ndani ya Uzazi ya Mwanamke

Mwanamke anapaswa kukojoa kabla ya uchunguzi wa fupanyonga na anaweza kuombwa kuchukua sampuli ya mkojo ili itumiwe katika uchambuzi. Kwa kawaida, gauni au shuka hutolewa, na msaidizi huwepo ili kumchunga na wakati mwingine kusaidia katika uchunguzi. Ikiwa mwanamke anataka kuangalia wakati uchunguzi wa fupanyonga unaendelea, anapaswa kumwambia daktari, ambaye anaweza kumpa kioo. Daktari anaweza kuelezea uchunguzi au kupitia matokeo kabla, wakati au baada ya uchunguzi.

Wakati wa uchunguzi wa fupanyonga, mwanamke hulala chali huku nyonga na magoti yake yamepinda na matako yake yakiwa pembeni mwa meza ya uchunguzi. Mkao huu husaidia kufungua fupanyonga ili daktari aweze kuchunguza anatomia ya ndani ya uzazi. Meza maalum za uchunguzi wa fupanyonga zina vikuku vya visigino ili kumsaidia mwanamke kudumisha mkao huu. Kabla ya uchunguzi wa fupanyonga kuanza, daktari humwomba mwanamke alegeze miguu na nyonga zake.

Kwa uchunguzi, daktari kwanza hukagua eneo la nje la viungo vya uzazi na kubaini kasoro zozote, kubadilika rangi, kutokwa na uchafu au uvimbe. Uchunguzi huu unaweza kubaini kasoro zozote au unaweza kuonyesha dalili za matatizo ya homoni, kansa, maambukizi, jeraha au unyanyasaji wa kingono.

Daktari hutawanya tishu katika mlango wa uke (inayoitwa kuma au midomo ya kuma) na kuchunguza mlango huo wa uke. Kwa kutumia spekalamu (kifaa cha chuma au plastiki kinachoshikilia kuta za uke), daktari huchunguza uke na mlango wa kizazi (sehemu ya chini ya uterasi).

Uke huchunguzwa ili kubaini iwapo kuna matatizo (kama vile uvimbe uliojaa maji) na kutokwa na uchafu. Mlango wa kizazi huchunguzwa kwa makini ili kuangalia ikiwa kuna dalili za uvimbe, kasoro au saratani ya mlango wa kizazi. Daktari anaweza kutumia brashi ndogo ya plastiki kuchukua sampuli ili atumie kupima, kwa kawaida kipimo cha Papanicolaou (Pap) na/au kipimo cha HPV (ili kupima saratani ya mlango wa kizazi). Sampuli inaweza kuchukuliwa kutoka ukeni au shingo wa uzazi ili ipimwe ili kufahamu vyanzo vya uke kuwa chungu, kama vile maambukizi ya kuvu ukeni, maambukizi ya chachu ukeni au maambukizi ya zinaa.

Daktari anamwomba mwanamke akohoe au ajilaze chini ili aangalie ikiwa kuna kupungua kwa viungo vya fupanyonga , ambayo ni kutokeza kwa kibofu cha mkojo, rektamu au chango ndani ya uke.

Kipimo cha Pap

Madaktari hutumia spekulamu (kifaa cha chuma au plastiki) kushikilia kuta za uke. Kisha huingiza brashi ndogo ya plastiki ili kutoa sampuli kutoka kwenye mlango wa kizazi (sehemu ya chini ya uterasi) ili ipimwe.

Baada ya kuondoa spekulamu ukeni, daktari huingiza vidole vya shahada na kati vya mkono mmoja akiwa amevaa glavu ndani ya uke na kugusa kuta za uke ili kukagua wapo kuna kasoro zozote au maeneo yenye uchungu. Daktari pia hugusa mlango wa kizazi ili kuangalia ikiwa kuna kasoro au uchungu wowote ambao haukuweza kugunduliwa wakati wa uchunguzi wa spekulamu.

Vidole vikiwa ukeni, daktari kisha huweka vidole vya mkono mwingine kwenye sehemu ya chini ya fumbatio juu ya mfupa wa kinena (huu unaitwa uchunguzi kwa mikono miwili). Uchunguzi huu hufanywa ili kugusa uterasi na ovari na uvimbe wa nyama au uchungu wowote usio wa kawaida kwenye mfumo wa uzazi wa mwanamke. Kati ya mikono miwili, kwa kawaida uterasi huhisiwa kama muundo imara, laini na wenye umbo la pea, na nafasi yake, ukubwa, uthabiti, uhamaji na kiwango cha uchungu (ikiwa upo) vinaweza kubainishwa.

Kisha daktari hujaribu kuhisi ovari na nyenzo nyingine inayozunguka uterasi (kama vile mirija ya ova iliyovimba) kwa kusogeza mkono kwenye fumbatio zaidi upande mmoja na kuweka shinikizo zaidi kiasi. Shinikizo zaidi linahitajika kwa sababu ovari ni ndogo na ni ngumu zaidi kuhisiwa kuliko uterasi. Baada ya ukomo wa hedhi, ovari huwa ndogo (kwa sababu ya kupungua kwa utendaji kazi wa homoni) na kwa kawaida daktari hawezi kuzihisi wakati wa uchunguzi wa fupanyonga. Mwanamke anaweza kuona sehemu hii ya uchunguzi kuwa isiyofurahisha kidogo, lakini haipaswi kuwa chungu. Daktari hubaini iwapo kuna kasoro zozote kwenye ovari na ikiwa kuna uchungu katika ovari au nyenzo nyingine.

Uchunguzi wa rektamu na uke

Mchanganyiko wa uchunguzi wa rektamu na uke unaweza kufanywa. Wakati mwingine uvimbe au kasoro katika sehemu ya nyuma ya fupanyonga (sehemu inayoelekea uti wa mgongo) au kwenye tishu kati ya uke na rektamu zinaweza kugunduliwa tu kwa kutumia aina hii ya uchunguzi. Daktari huingiza kidole cha shahada kwenye uke na kidole cha kati katika rektamu.

Zaidi ya hayo, daktari anaweza kuchunguza rektamu ili kubaini iwapo kuna bawasiri, nyufa, polipu na uvimbe. Sampuli ndogo ya kinyesi inaweza kuchukuliwa kwa kidole kilichovishwa glavu na kupimwa ili kubaini iwapo kuna damu isiyoonekana. Mwanamke anaweza kupewa kifaa cha kupeleka nyumbani ili kupima damu isiyoonekana kwenye kinyesi.