Sepsisi ni mwitikio mkubwa wa mwili kwa bakteremia au maambukizi mengine pamoja na kasoro au kutofanya kazi kwa mfumo muhimu katika mwili. Mshtuko wa septiki ni shinikizo la damu la chini ambalo ni hatari kwa maisha ya binadamu (mshtuko) na kutofanya kazi kwa viungo kutokana na sepsisi.
Kwa kawaida, sepsisi inatokana na maambukizi fulani ya bakteria, wakati mwingine hupatikana hospitalini.
Kuwa na hali fulani (kama vile mfumo wa kinga ulio dhaifu), magonjwa fulani ya muda mrefu, pamoja na kiungo cha kuwekwa au valvu ya moyo na kasoro fulani za valvu ya moyo huongeza hatari.
Kwanza, watu huwa na joto la mwili la juu (au wakati mwingine la chini), wakati mwingine wakitetemeka kutokana na kuhisi baridi na udhaifu.
Kadri sepsisi inavyokua mbaya, moyo huanza kupiga kwa haraka, kupumua kunakuwa kwa kasi, watu huanza kuchanganyikiwa na shinikizo la damu linapungua.
Madaktari hushuku utambuzi kulingana na dalili na kuthibitisha kwa kugundua bakteria katika sampuli ya damu, mkojo, au nyenzo nyingine.
Dawa za kuua bakteria hutolewa mara moja, pamoja na oksijeni na vioevu kwa kupitia mshipa na wakati mwingine dawa za kuongeza shinikizo la damu.
(Tazama pia Utangulizi wa Bakteremia, Sepsisi na Mshtuko wa Sepsisi.)
Kwa kawaida, mwitikio wa mwili kwa maambukizi unahusishwa na eneo maalum lililoathirika, kwa mfano dalili za maambukizi ya njia ya mkojo mara nyingi zinahusishwa na kibofu cha mkojo. Lakini katika sepsisi, mwitikio wa maambukizi hufanyika katika mwili mzima—unaitwa mwitikio wa mfumo mzima.
Mwitikio huu kwa kawaida unajumuisha joto la juu lisilo la kawaida (homa) au joto la chini (kushuka kwa joto la mwili) pamoja na mojawapo au zaidi ya dalili zifuatazo:
Mapigo ya moyo ya haraka
Kupumua kwa haraka
Ingawa maambukizi mengi husababisha dalili kama hizo katika mwili mzima, katika sepsisi viungo huanza kutofanya kazi inavyofaa na mtiririko wa damu unakuwa hafifu kwa sehemu za mwili.
Mshtuko wa Sepsisi ni sepsisi inayosababisha shinikizo la damu kuwa chini sana (mshtuko). Kama matokeo yake, viungo vya ndani kama vile mapafu, figo, moyo na ubongo, kwa kawaida hupokea damu ndogo sana na kusababisha kutofanya kazi inavyofaa. Mshtuko wa Sepsisi hugunduliwa wakati shinikizo la damu linabaki chini licha ya matibabu ya kuingiza maji mwilini kupitia mishipa. Mshtuko wa sepsisi ni hatari kwa maisha.
Sababu za Sepsisi na Septic Shock
Sepsisi hutokea wakati sumu zinazozalishwa na bakteria fulani zinasababisha seli katika mwili kutoa vitu vinavyosababisha uvimbe (saitokini). Ingawa saitokini husaidia mfumo wa kinga kupambana na maambukizi, zinaweza kuwa na athari mbaya:
Zinaweza kusababisha mishipa ya damu kupanuka (kuongezeka) na hivyo kupunguza shinikizo la damu.
Zinaweza kusababisha damu kuganda katika mishipa midogo ya damu ndani ya sehemu za mwili.
Mara nyingi, sepsisi husababishwa na maambukizi ya aina fulani za bakteria. Kwa nadra, fangasi, kama Candida, husababisha sepsisi. Maambukizi yanayoweza kusababisha sepsisi huanza mara nyingi katika mapafu, tumbo, au njia ya mkojo. Kwa watu wengi, maambukizi haya hayasababisha sepsisi. Hata hivyo, wakati mwingine bakteria huenea kwenye mtiririko wa damu (hali inayoitwa bakteremia). Sepsisi inaweza kisha kutokea. Wakati mwingine maambukizi yanaweza kutoka kwenye majipu ya ngozi. Wakati mwingine, kama katika ugonjwa wa mshtuko wenye sumu, sepsisi husababishwa na sumu zinazotolewa na bakteria ambazo hazijaenea kwenye mtiririko wa damu.
Matatizo ya Sepsisi na Septic Shock
Kupungua kwa shinikizo la damu na vipande vidogo vya damu iliyoganda husababisha mfululizo wa matatizo mabaya:
Mzunguko wa damu hupungua kwa viungo muhimu (kama figo, mapafu, moyo na ubongo).
Moyo hujaribu kufidia kwa kufanya kazi kwa bidii hivyo kuongeza mapigo ya moyo na kiasi cha damu inayopigwa. Hatimaye, sumu za bakteria na kuongezeka kwa kazi ya kupiga damu hufanya moyo kuwa dhaifu. Kama matokeo yake, moyo hupiga damu ndogo na viungo muhimu vinapata damu kidogo zaidi.
Wakati tishu hazipati damu ya kutosha, zinatoa asidi ya lactic (bidhaa ya taka) kupita kiasi kwenye mtiririko wa damu na kufanya damu kuwa na asidi zaidi (Asidosisi).
Madhara haya yote husababisha mzunguko mbaya wa kutofanya kazi inavyofaa kwa sehemu za mwili:
Figo hutoa mkojo kidogo au hazitoi kamwe na bidhaa za taka (kama urea nitrojeni) kutoka kwenye shughuli za kemikali mwilini hujikusanya kwenye damu.
Kuta za mishipa ya damu zinaweza kuvuja, kuruhusu vioevu kutoka kwenye mtiririko wa damu na kusababisha uvimbe.
Ufanisi wa mapafu hupungua kwa sababu mishipa ya damu katika mapafu inavuja, vopevu hivo hukusanyika na kufanya kupumua kuwa ngumu.
Kadri vipande vidogo sana vya damu iliyoganda vinavyoendelea kujitokeza, vinatumia protini iliyo kwenye damu zinazosababisha damu kuganda. Kisha, kutokwa na damu kupita kiasi (ugandikaji wa damu uliosambaa mwilini) unaweza kutokea.
Viashiria vya Hatari vya Sepsisi na Septic Shock
Hatari ya sepsisi inaongezeka kwa watu wenye hali zinazopunguza uwezo wao wa kupambana na maambukizi makali. Hali hizi ni pamoja na zifuatazo:
Kuwa mtoto mchanga (angalia Sepsisi kwa Watoto Wachanga)
Kuwa mtu mzima mzee
Kuwa mjamzito
Kuwa na magonjwa fulani ya muda mrefu kama kisukari au sirosisi
Kuwa na mfumo wa kinga ulio dhaifu kutokana na matumizi ya dawa zinazoshinikiza mfumo wa kinga (kama dawa za tibakemikali au kotikosteroidi) au kutokana na magonjwa fulani (kama saratani, maambukizi ya VVU na magonjwa ya mfumo wa kinga)
Kuwa umetibiwa hivi karibuni kwa kutumia dawa za kuua bakteria au kotikosteroidi
Kuwa umelazwa hospitalini hivi karibuni (hasa katika kitengo cha wagonjwa mahututi)
Hatari pia huongezeka kwa watu ambao wana uwezekano mkubwa wa bakteria kuingia kwenye mzunguko wao wa damu. Watu kama hao ni pamoja na wale ambao wana kifaa cha matibabu kilichoingizwa ndani ya mwili (kama katheta iliyoingizwa kwenye mshipa au njia ya mkojo, mirija ya kutoa maji mwilini, au mirija ya kupumua). Wakati vifaa vya matibabu vinapoingizwa ndani ya mwili, vinaweza kuingiza bakteria ndani ya mwili. Bakteria pia zinaweza kukusanyika kwenye vifaa kama hivyo na kuongeza uwezekano wa maambukizi na sepsisi. Kadri kifaa kinavyobaki mahali, ndivyo hatari inavyoongezeka.
Hali nyingine pia zinaongeza hatari ya sepsisi:
Kujidunga dawa za kulevya: Dawa na sindano zinazotumika mara nyingi si safi. Kila sindano inaweza kusababisha bakteremia kwa viwango tofauti. Watu wanaotumia dawa hizi pia wako katika hatari ya magonjwa ambayo yanaweza kudhoofisha mfumo wa kinga (kama maambukizi ya VVU).
Kuwa na kiungo cha kuwekwa au valvu ya moyo au kasoro fulani za valvu ya moyo: Bakteria hujikusanya na kukusanyika kwenye sehemu hizi. Bakteria zinaweza kuachiliwa mara kwa mara au kwa muda mrefu kwenye mzunguko wa damu.
Kuwa na maambukizi yanayoendelea licha ya matibabu kwa kutumia dawa za kuua bakteria: Bakteria nyingine zinazosababisha maambukizi na sepsisi ni sugu kwa dawa za kuua bakteria. Dawa za kuua bakteria haziondoi bakteria sugu. Hivyo, maambukizi yakiendelea kwa watu wanaotumia dawa za kuua bakteria, kuna uwezekano mkubwa kuwa yamesababishwa na bakteria sugu kwa dawa za kuua bakteria na zinaweza kusababisha sepsisi.
Dalili za Sepsisi na Septic Shock
Watu wengi hupata homa, lakini wengine hupata joto chini la mwili. Watu wanaweza kutetemeka kutokana na kuhisi baridi na kuhisi mwili ukiwa dhaifu. Dalili nyingine zinaweza pia kuwepo kulingana na aina na eneo la maambukizi ya awali (kwa mfano, watu wenye nimonia wanaweza kuwa na kikohozi, maumivu ya kifua na shida ya kupumua). Kupumua, mapigo ya moyo, au zote mbili zinaweza kuwa za kasi.
Kadri sepsisi inavyozidi kuwa mbaya, watu huanza kuchanganyikiwa na kuwa na tahadhari ndogo. Ngozi inakuwa na joto na rangi inabadilika kuwa nyekundu. Mapigo ya moyo ni ya haraka na yenye nguvu na watu hupumua kwa kasi. Watu hukojoa mara chache na kwa kiasi kidogo na shinikizo la damu hupungua. Baadaye, joto la mwili mara nyingi hushuka chini ya kiwango cha kawaida na inakuwa vigumu sana kupumua. Ngozi inaweza kuwa baridi na kupoteza rangi na yenye madoa, au kuwa buluu kwa sababu mtiririko wa damu umepungua. Kupungua kwa mtiririko wa damu kunaweza kusababisha tishu, ikiwa ni pamoja na tishu katika sehemu muhimu (kama vile utumbo), kufa na kusababisha kifo cha tishu.
Wakati mshtuko wa sepsisi unapotokea, shinikizo la damu huwa chini licha ya matibabu. Septic shock inaweza kuwa ya kufisha.
Utambuzi wa Sepsisi na Septic Shock
Ukuzaji wa bakteria katika maabara
Majaribio ya kutafuta chanzo cha maambukizi (uchunguzi kwa kawaida unajumuisha picha za eksirei za kifua na uchunguzi mwingine wa picha na ukuzaji wa bakteria kutoka kwenye sampuli za maji au tishu)
Madaktari kwa kawaida wanashuku sepsisi wakati mtu mwenye maambukizi anapojitokeza ghafla na kuwa na joto la juu au la chini, mapigo ya moyo kiwango cha kupumua cha haraka, au shinikizo la chini la damu.
Ili kuthibitisha uchunguzi, madaktari hutafuta bakteria katika mzunguko wa damu (bakteremia), ushahidi wa maambukizi mengine ambayo yanaweza kusababisha sepsisi na idadi isiyo ya kawaida ya seli nyeupe za damu katika sampuli ya damu.
Sampuli za damu zinachukuliwa ili kujaribu kukuza (ukuzaji wa bakteria) bakteria katika maabara (kwa kawaida ni mchakato wa siku 1 hadi 3). Hata hivyo, ikiwa mtu amekuwa akitumia dawa za kuua bakteria kwa ajili ya maambukizi yao ya awali, bakteria zinaweza kuwa lakini huenda zisikue. Wakati mwingine katheta huondolewa mwilini na sehemu za mwisho hukatwa na kutumwa kwenye maabara. Kugundua bakteria katika katheta ambayo ilikuwa na mgusano na damu kunaonyesha kwamba bakteria huenda ziko katika mzunguko wa damu.
Ili kuchunguza maambukizi mengine ambayo yanaweza kusababisha sepsisi, madaktari huchukua sampuli za maji au tishu, kama vile mkojo, maji ya uti wa mgongo wa ubongo, tishu kutoka kwenye vidonda, kikohozi kilichotolewa kutoka mapafuni. Sampuli hizi hukuzwa na kuangaliwa kama zina bakteria.
Eksirei za kifua na uchunguzi mwingine wa picha, kama vile ultrasonografia, tomografia ya kompyuta (CT), na upigaji picha kwa mwanga wa sumaku (MRI), pia zinaweza kufanywa kutafuta chanzo cha maambukizi.
Uchunguzi mwingine hufanywa ili kutafuta dalili za sehemu za mwili kutofanya kazi inavyofaa na matatizo mengine ya sepsisi. Uchunguzi huo unaweza kujumuisha:
Uchunguzi wa damu kupima viwango vya asidi ya maziwa na bidhaa nyingine za taka za kimetaboli, ambazo zinaweza kuwa juu na idadi ya chembe sahani (seli zinazosaidia damu kuganda), ambazo zinaweza kuwa chache
Uchunguzi wa damu au sensa iliyowekwa kwenye kidole kupima viwango vya oksijeni katika damu na hivyo kutathmini jinsi mapafu na mishipa ya damu inavyofanya kazi
Elektrokadiografia (ECG) kuangalia kasoro katika mpigo wa moyo na hivyo kubaini ikiwa usambazaji wa damu kwa moyo unakutosha
Uchunguzi mwngine wa kubaini kama mshtuko unatokana na sepsisi au tatizo jingine
Matibabu ya Sepsisi na Septic Shock
Dawa za kuua bakteria
Maji ya ndani ya mishipa.
Oksijeni
Kuondoa chanzo cha maambukizi
Wakati mwingine dawa za kuongeza shinikizo la damu
Madaktari mara moja hutibu sepsisi na mshtuko wa sepsisi kwa kutumia dawa za kuua bakteria. Madaktari hawangoji matokeo ya kuthibitisha uchunguzi kwa sababu kuchelewesha matibabu ya dawa za kuua bakteria kunapunguza sana nafasi za kuishi. Matibabu hufanyika hospitalini.
Watu wenye mshtuko wa sepsisi au ambao ni wagonjwa sana huchukuliwa mara moja katika kitengo cha wagonjwa mahututi kwa ajili ya matibabu.
Dawa za kuua bakteria
Wakati wa kuchagua dawa za kuua bakteria za awali, madaktari huzingatia ni bakteria gani zinaweza kuwepo, hali ambayo hutegemea mahali ambapo maambukizi yalianzia. Kwa mfano, bakteria zinazosababisha maambukizi ya njia ya mkojo kwa kawaida ni tofauti na bakteria zinazosababisha maambukizi ya ngozi. Pia, madaktari huzingatia ni bakteria gani zinazoongoza katika maambukizi katika jamii ya mtu na katika hospitali yao maalum. Mara nyingi, dawa 2 au 3 za kuua bakteria hutolewa pamoja ili kuongeza nafasi za kuua bakteria, hasa wakati chanzo cha bakteria hakijulikani. Baadaye, matokeo ya uchunguzi yanapopatikana, madaktari wanaweza kubadilisha dawa ya kuua bakteria ambayo ni bora dhidi ya bakteria maalum zinazosababisha maambukizi.
Maji ya ndani ya mishipa.
Watu wenye mshtuko wa sepsisi pia hupatiwa kiasi kikubwa cha maji kupitia mshipa ili kuongeza kiasi cha maji katika mzunguko wa damu na hivyo kuongeza shinikizo la damu. Kuwapa maji kidogo hakuna ufanisi lakini kuwapa maji mengi sana kunaweza kusababisha kujaa kwa mapafu (maji kukusanyika ndani ya mapafu).
Oksijeni
Oksijeni hutolewa kupitia barakoa, kifaa cha kutoa oksijeni, au kupitia mrija la kupumua ikiwa umewekwa. Ikiwa inahitajika, mashine ya kusaidia katika kupumua (kifaa kinachosaidia hewa kuingia na kutoka kwenye mapafu) hutumiwa kusaidia katika kupumua.
Kuondoa chanzo cha maambukizi
Ikiwa majipu yapo, usaha hutolewa. Katheta, mirija, au vifaa vingine vya matibabu ambavyo vinaweza kuwa vimeanzisha maambukizi hutolewa au kubadilishwa. Upasuaji unaweza kufanywa ili kuondoa tishu zilizoambukizwa au kufa.
Matibabu mengine
Ikiwa maji yaliyowekwa kupitia mshipa hayaongezi shinikizo la damu, madaktari wakati mwingine hutoa dawa zinazofanya mishipa ya damu kuwa nyembamba (kama vile norepinephrine). Dawa hizi huongeza shinikizo la damu na kuongeza mtiririko wa damu kwenye ubongo, moyo na sehemu nyingine. Hata hivyo, kwa sababu dawa hizi zinaweza kufanya mishipa ya damu kuwa nyembamba ndani ya sehemu za mwili, wakati mwingine hupunguza kiasi cha mtiririko wa damu katika sehemu hizo.
Wakati mwingine watu wenye mshtuko wa sepsisi hupata kiwango cha juu cha sukari ya damu (glukosi). Kwa sababu sukari ya damu ya juu hukwamisha jinsi mfumo wa kinga unavyoitikia maambukizi, madaktari hutoa insulini kupitia mshipa kwa watu ili kupunguza kiwango cha glukosi katika damu.
Kotikosteroidi (kama haidrokotisoni) zinaweza kuwekwa kupitia mshipa kwa watu ambao shinikizo lao la damu linaendelea kuwa chini licha ya kupokea maji na dawa za kutosha kwa ajili ya kuongeza shinikizo la damu na licha ya kutibiwa chanzo cha maambukizi yao.
Ubashiri wa Sepsisi na Septic Shock
Bila matibabu, mshtuko wa sepsisi ni hatari kwa maisha katika watu wengi. Hata na matibabu, kuna hatari kubwa ya kifo. Kwa wastani, ni hatari kwa maisha katika takriban 30 hadi 40% ya watu. Hata hivyo, hatari ya kifo inatofautiana sana kulingana na mambo mengi, ikiwa ni pamoja na jinsi watu wanavyotibiwa haraka, aina ya bakteria zinazohusika (hasa ikiwa bakteria hizo ni zimekuwa sugu kwa dawa za kuua bakteria) na hali ya afya ya mtu.