Magonjwa na Kifo kwa Watoto Wachanga

NaSteven D. Blatt, MD, State University of New York, Upstate Medical University
Imekaguliwa naAlicia R. Pekarsky, MD, State University of New York Upstate Medical University, Upstate Golisano Children's Hospital
Imepitiwa/Imerekebishwa Imebadilishwa Jul 2025
v823979_sw

Watoto wachanga wanaougua au waliozaliwa kabla ya wakati mara nyingi hupokea huduma ya matibabu katika kitengo cha huduma maalum ya utunzaji au kitengo cha wagonjwa wachanga mahututi (NICU). Fursa ya wazazi kuingiliana na mtoto wao mchanga wakati huu mgumu inaweza kupunguzwa na mahitaji ya kimatibabu ya mtoto huyo mchanga. Hata hivyo, hospitali nyingi hujaribu kuwapa wazazi fursa nyingi iwezekanavyo za kuingiliana na mtoto wao mchanga, na hakuna mtoto mchanga, hata anayetumia mashine ya kupumulia, ambaye ni mgonjwa sana kuonwa na kuguswa na wazazi. Aidha, wazazi kwa kawaida hufadhaika kihisia kutokana na hali ya mtoto wao mchanga na wanaweza kuhisi wanyonge wakati ambapo wanahitajika zaidi. Hii inaweza kuongeza hisia za kutoweza au hatia, hasa kwa wazazi ambao watoto wao wachanga wanaogua sana au waliozaliwa kabla ya wakati wamelazwa hospitalini kwa muda mrefu.

Katika tukio mbaya la mtoto kufariki, hasara hii huwa ya kuhuzunisha kihisia kwa wazazi.

(Angalia pia Kifo na Kufa kwa Watoto na uangalie Utangulizi wa Kifo na Kufa.)

Je, Ulijua...

  • Ugonjwa au kifo cha mtoto mchanga au mtoto mara nyingi huwafanya wazazi wajisikie kuwa na hatia, hata kama hawana kosa.

Magonjwa kwa Watoto Wachanga

Wazazi wanapaswa kumwona, kumshika na kuingiliana na mtoto wao haraka iwezekanavyo na kadri iwezekanavyo. Hata kwa watoto wachanga wanaougua sana au waliozaliwa kabla ya wakati, mara nyingi wazazi wanaweza kusaidia kulisha, kuogesha na kubadilisha nguo. Kwa kawaida wazazi huhimizwa kutoa utunzaji wa moja kwa moja kwa mtoto wao mchanga kama njia ya kumjua mtoto wao mchanga na kujiandaa kumpeleka mtoto wao nyumbani.

Mgusano wa ngozi kwa ngozi kati ya wazazi na watoto wachanga (wakati mwingine huitwa utunzaji wa kangaruu) unahimizwa kwa sababu una faida nyingi kwa wazazi na watoto wachanga. Katika utunzaji wa kangaruu, mtoto mchanga kwa kawaida huvaa nepi pekee na hushikiliwa kifuani mwa mzazi akiwa uchi. Watoto wachanga wanaogusana ngozi kwa ngozi na wazazi wanaweza kuongeza uzito, kuchangamka, kulala vizuri, na kuwa na nafasi nzuri ya kunyonya (kunyonya titi) haraka kuliko wale ambao hawafanyi hivyo. Wazazi wanaogusana ngozi kwa ngozi huwa na mfadhaiko mdogo na hujenga uhusiano wa karibu na watoto wao wachanga, na mama wanaweza kutoa maziwa zaidi. Kunyonyesha kunawezekana wakati mtoto mchanga yuko katika kitengo cha huduma maalum ya uuguzi au NICU, hata kama mtoto mchanga lazima alishwe kupitia mrija mwanzoni. Vitengo vingi vya uuguzi wa watoto wachanga husaidia familia kuhifadhi na kutumia maziwa ya mama kwa manufaa ya watoto wao.

Hospitali nyingi huwahimiza wazazi kukaa kando ya kitanda cha mtoto wao mchanga mchana na usiku na hata kushiriki katika zamu za hospitali zinazolenga familia ambapo wanaweza kuingiliana na madaktari, wauguzi, na wahudumu wengine na kujadili mipango ya matibabu. Hospitali nyingi huruhusu wazazi kutembelea saa yoyote, na zingine zina maeneo ambako wazazi wanaweza kukaa kwa muda mrefu ili kuwa karibu na watoto wao wachanga.

Ikiwa mtoto mchanga ana kasoro ya kuzaliwa (pia huitwa tatizo la kuzaliwa nalo), wazazi wanaweza kuhisi hatia, huzuni, hasira au hisia nyingine. Wengi huhisi hatia zaidi kwa sababu ya kupata hisia kama hizo. Kumwona na kumgusa mtoto haraka iwezekanavyo baada ya kuzaliwa kunaweza kuwasaidia wazazi kuzoeana na mtoto kama vile wangefanya na mtoto mwingine yeyote. Vipindi vya ushauri nasaha na usaidizi kuhusu kasoro ya kuzaliwa, matibabu yanayowezekana, na ubashiri wa ugonjwa wa mtoto mchanga vinaweza kuwasaidia wazazi kuelewa hali ya mtoto wao mchanga, kujiandaa kumtunza mtoto wao nyumbani, kupanga huduma bora ya kimatibabu, na kutunza afya yake ya akili. Kuwasiliana na familia zilizo na mtoto mwenye kasoro kama hiyo ya kuzaliwa au kuwasiliana na vikundi vya usaidizi pia kunaweza kusaidia.

Kupoteza Mtoto Aliyezaliwa Karibuni (Kifo Mchanga)

Ikiwa mtoto mchanga atakufa kabla ya kuonwa au kuguswa na wazazi, baadhi ya wazazi wanaweza kuhisi kana kwamba hawakuwahi kupata mtoto. Ingawa inaumiza, kumbeba au kumwona mtoto baada ya kifariki kunaweza kuwasaidia wazazi kuanza mchakato wa kuomboleza. Wazazi wa mtoto mchanga aliyezaliwa mfu wakati mwingine hupata faraja katika kumvisha mtoto mchanga au kumfunika mtoto mchanga kwenye blanketi na kupiga picha, kuchukua nyayo, au vitu vingine vya kukumbukwa wanavyoweza kuhifadhi ili kumkumbuka mtoto wao. Desturi hii humfanya mtoto mchanga kuchukuliwa kama mtu wa kawaida na kusisitiza kwamba mtoto mchanga alikuwa sehemu halisi ya familia yao.

Je, Ulijua...

  • Kuona na kugusa mtoto mchanga aliyefariki mara nyingi huwasaidia wazazi kuanza kuomboleza.

Kuhisi utupu, matumaini na ndoto zilizopotea, na hofu zinaweza kuwalemea wazazi, ambao wanaweza kuwa wenye huzuni. Wazazi huwa na tabia ya kuhisi hatia, kujilaumu hata kama hawahusiki na kifo hicho. Huzuni na hatia inayofuata inaweza kuathiri uhusiano kati ya wazazi. Utaratibu wa kuomboleza unaweza pia kumaanisha kwamba wazazi hawawezi kuhudumia mahitaji ya wanafamilia wengine, wakiwemo watoto wengine.

Familia nyingi ambazo watoto wao wachanga wanaugua sana, waliozaliwa kabla ya wakati, au waliofariki zinaweza kufaidika na ushauri nasaha kutoka kwa wahudumu wa kisaikolojia au wa kidini. Vikundi vya usaidizi vya wazazi na familia pia vinaweza kusaidia.

Taarifa Zaidi

Nyenzo zifuatazo za lugha ya Kiingereza zinaweza kuwa muhimu. Tafadhali kumbuka kuwa Mwongozo hauwajibiki kwa maudhui ya nyenzo hizi.

  1. March of Dimes: Kukabiliana na Huzuni Baada ya Kifo cha Mtoto Wako

  2. Caring Community

  3. The Compassionate Friends