Rubela

(Surua ya Ujerumani; Surua ya Siku 3)

NaBrenda L. Tesini, MD, University of Rochester School of Medicine and Dentistry
Imekaguliwa naBrenda L. Tesini, MD, University of Rochester School of Medicine and Dentistry
Imepitiwa/Imerekebishwa Jun 2023 | Imebadilishwa Nov 2025
v819386_sw

Rubela ni maambukizi ya virusi yanayoambukiza ambayo kwa kawaida husababisha dalili zisizo kali kwa watoto, kama vile maumivu ya viungo na upele. Rubela inaweza kusababisha kifo cha kijusi au kasoro kali za kuzaliwa nazo iwapo mama ataambukizwa wakati wa ujauzito wa mapema.

  • Rubela inasababishwa na virusi.

  • Dalili za kawaida ni pamoja na nodi za limfu ambazo zimevimba, madoa yenye rangi ya waridi kwenye paa la mdomo, na upele maalum.

  • Utambuzi unategemea dalili.

  • Matibabu ya rubella yanalenga kupunguza dalili.

  • Chanjo ya kawaida inaweza kuzuia rubela.

(Tazama pia Rubela kwa Watoto Wachanga.)

Rubella kwa kawaida ni maambukizi madogo ambayo hutokea utotoni. Hata hivyo, rubela huenda ikawa na madhara makubwa kwa watoto wachanga ambao waliambukizwa kabla ya kuzaliwa. Mwanamke ambaye ameambukizwa wakati wa wiki 16 za kwanza (hasa wiki 8 hadi 10 za kwanza) za ujauzito mara nyingi hupitisha maambukizi kwenye kijusi. Maambukizi haya ya fetasi husababisha kuharibika kwa mimba, kuzaliwa mfu, au kasoro nyingi kali anazozaliwa nazo mtoto mchanga (zinazojulikana kama ugonjwa wa kuzaliwa wa rubela).

Rubela hapo awali ilijulikana kama "Surua ya Kijerumani" au "Surua ya siku 3" kwa sababu husababisha upele sawa na upele unaosababishwa na surua. Hata hivyo, husababishwa na virusi tofauti.

Rubella huenezwa hasa kwa kuvuta hewa yenye matone madogo yenye unyevunyevu yaliyo na virusi ambayo yamekoholewa hewani na mtu aliyeambukizwa. Kutangamana kwa karibu na mtu aliyeambukizwa pia kunaweza kueneza maambukizi. Watu ambao wamewahi kuambukizwa rubela huambukiza zaidi kuanzia wiki 1 kabla hadi wiki 1 baada ya upele kutokeaa, na maambukizi kwa kawaida huenea wakati upele upo. Hata hivyo, watu ambao hawana upele au dalili zozote bado wanaweza kueneza virusi kwa watu wengine. Mtoto mchanga aliyeambukizwa kabla ya kuzaliwa anaweza kueneza maambukizi kwa miezi mingi baada ya kuzaliwa.

Mtu ambaye amewahi kuambukizwa rubela hupata kinga na kwa kawaida hawezi kuambukizwa tena.

Rubela hapo awali ilikuwa kawaida wakati wa majira ya kuchipua, huku milipuko mikubwa ikiambukiza mamilioni ya watu kila baada ya miaka 6 hadi 9. Maambukizi hayo sasa ni nadra nchini Marekani kwa sababu ya chanjo iliyoenea. Hata hivyo, baadhi ya wanawake vijana waliokomaa hawajawahi kupata rubela au chanjo ya rubela na hivyo wako katika hatari ya kupata watoto wenye kasoro kubwa za kuzaliwa nazo iwapo wataambukizwa wakati wa ujauzito wa mapema.

Tangu mwaka wa 2004 nchini Marekani visa vyote vya rubella vimeletwa na watu wanaosafiri kutoka maeneo ambapo rubela inapatikana sana na kupata rubela wakiwa nje ya nchi kabla ya kurudi nchini Marekani.

Je, Ulijua...

  • Chanjo ya kawaida inaweza kuzuia rubela na maambukizi mengi ya virusi.

Dalili za Rubela

Dalili za Rubela hutofautiana kidogo kati ya watoto na watu wazima. Visa vingi huwa na athari ndogo.

Dalili za rubela huanza takriban siku 14 hadi 21 baada ya kuambukizwa.

Kwa watoto, rubela kwa kawaida husababisha dalili ndogo au zisizoonekana kabisa.

Dalili ndogo huenda zikatokea kwa watoto siku 1 hadi 5 kabla ya upele kutokea:

  • Homa ya chini (chini ya 102° F [39° C])

  • Usumbufu wa jumla

  • Jicho la waridi

  • Nodi za limfu ambazo zimevimba shingoni na nyuma ya kichwa

  • Koo jekundu au linalowasha

  • Maumivu ya viungo

Upele unaosababishwa na rubella ni sawa na ule unaosababishwa na surua lakini si mwekundu kupita kiasi na hauungani na kuunda maeneo makubwa mekundu. Upele huo huanzia kwenye uso na shingo na kuenea haraka kwenye pingiti, mikono na miguu. Vipele vinapoonekana, ngozi hugeuka kuwa nyekundu kidogo (kuiva), hasa kwenye uso. Madoa mekundu yasiyo na maumivu yanaweza kuonekana nyuma ya paa la mdomo na koo (madoa ya Forchheimer). Upele huo kwa kawaida hudumu kwa takriban siku 3 lakini unaweza kudumu kwa siku kadhaa zaidi.

Katika matukio machache, watu hupata maambukizi ya sikio la kati (otitis media) au kiwango cha chini cha chembe chembe za kugandisha damu (thrombocytopenia).

Maambukizi ya ubongo (encephalitis) ni tatizo nadra sana, lakini wakati mwingine huleta kifo.

Upele wa Rubela
Ficha Maelezo

This photo shows the rash caused by rubella. The rash caused by rubella is similar to the rash caused by measles but is not as intensely red and does not merge to form large red areas.

Image courtesy of the Public Health Image Library of the Centers for Disease Control and Prevention.

Utambuzi wa Rubela

  • Tathmini ya daktari

  • Vipimo vya kupima kiasi cha kingamwili kwa watu walio katika hatari kubwa

Madaktari hushuku ugonjwa wa rubela kwa watu walio na tezi za limfu (lymph nodes) zilizovimba nyuma ya kichwa na upele wa kipekee.

Utambuzi wa uhakika wa rubela ni muhimu kwa wanawake wajawazito, watu walio na kichwa kuvimba (encephalitis), na watoto wachanga. Utambuzi unaweza kuthibitishwa kwa kupima kiasi cha kingamwili dhidi ya virusi vya rubela kwenye damu au kwa kupima sampuli kutoka kwenye koo, pua, au mkojo.

Kabla ya mtoto kuzaliwa, utambuzi unaweza kufanywa kwa kijusi kwa kupima maji ya chupa (amniotic fluid) au damu ya kijusi chenyewe. Wanawake wajawazito hufanyiwa uchunguzi wa damu wa mara kwa mara mapema wakati wa ujauzito ili kuthibitisha ikiwa wana kinga dhidi ya rubela.

Matibabu ya Rubela

  • Asetaminofeni au ibuprofen kwa ajili ya homa na maumivu ili kumfanya mgonjwa ajisikie nafuu

Hakuna matibabu ya kuponya maambukizi ya rubela. Watu wengi hupona kabisa bila kuhitaji matibabu. Acetaminophen au dawa ya kupunguza uvimbe isiyo na asteroidi (NSAIDs), kama vile ibuprofen, zinaweza kutolewa kwa homa na maumivu.

Hakuna matibabu ya ugonjwa wa kuvimba ubongo (encephalitis), ambao lazima upite wenyewe huku mgonjwa akipewa huduma ya kumtuliza maumivu.

Kinga ya Rubela

  • Chanjo ya MMR

Hakuna tena chanjo ya pekee kwa ajili ya rubela peke yake. Chanjo ya surua-matumbwitumbwi-rubella (MMR) ni chanjo ya muunganisho ambayo ina surua hai lakini waliodhoofika, matumbwitumbwi ba vurusi vya rubela. Chanjo ya MMR ni mojawapo ya chanjo za kawaida za utotoni na hutolewa kwa watoto katika mataifa mengi ambayo yana mfumo imara wa huduma za afya. Chanjo ya MMR na chanjo ya varisela (tetekuwanga) zinapatikana pia kama chanjo iliyounganishwa (chanjo ya MMRV).

Dozi mbili za chanjo ya MMR hupendekezwa mara kwa mara. Dozi ya kwanza hutolewa kati ya umri wa miezi 12 na 15, lakini inaweza kutolewa kwa watoto wenye umri mdogo wa kuanzia miezi 6 wakati wa mlipuko wa surua au kabla ya kusafiri nje ya nchi. Dozi ya pili hutolewa kati ya umri wa miaka 4 na 6.

Watoto ambao walikuwa chini ya umri wa mwaka 1 walipochanjwa bado wanahitaji dozi 2 zaidi baada ya siku yao ya kwanza ya kuzaliwa.

Kwa baadhi ya watoto, chanjo husababisha homa kidogo na upele, lakini watu hawaambukizi.

Chanjo ya MMR kwa kawaida hutoa kinga ya kudumu.

MMR ni chanjo hai na haitolewi wakati wa ujauzito.

Wanawake wajawazito ambao hawana kinga wanapaswa kuepuka kukutana na mtu yeyote mwenye rubela. Ingawa chanjo ya MMR haiwezi kutolewa wakati wa ujauzito, inaweza kutolewa mara tu baada ya kujifungua kwa watu ambao hawana kinga ili wawe salama wakati wa mimba za baadaye.

Watu waliochanjwa utotoni ambao wanapanga kupata ujauzito wanaweza kupimwa damu ili kuthibitisha kinga yao, kwa sababu baadhi ya watu hawapati kinga ya kudumu baada ya chanjo hiyo ya kwanza. Mara tu kinga inapothibitishwa, watu hawahitaji kupimwa tena kabla ya mimba zinazofuata.

Ili kuzuia kukiambukiza kijusi, watu ambao hawajachanjwa na wanaoweza kupata ujauzito wanapaswa kupata dozi moja ya chanjo ya MMR kisha wasubiri wiki 4 kabla ya kujaribu kushika mimba.

Kwa maelezo zaidi kuhusu nani anapaswa na nani asipewe chanjo ya MMR, tazama Utoaji wa Chanjo ya MMR. Tazama pia Madhara ya Chanjo ya MMR.