Wanawake wanaweza kuwa na ugumba ikiwa idadi ya mayai kwenye ovari zao ni ndogo na/au mayai hayako sawa.
Idadi na ubora wa mayai Katika ovari, zinaweza kuanza kupungua zikiwa na umri wa miaka 30 au hata mapema zaid, na hupungua kwa haraka baada ya umri wa miaka 40.
Madaktari hufanya vipimo vya damu ili kupima viwango vya homoni zinazohusika katika kutolewa kwa mayai na/au ultrasonografia ya ovari ili kuona na kuhesabu idadi ya vinyweleo (vifuko vidogo vilivyojaa kiowevu ambavyo vina mayai).
Matibabu hutegemea hali na umri wa mwanamke na inaweza kujumuisha kutumia mayai kutoka kwa mwanamke mwingine, hasa ikiwa mwanamke ana umri wa zaidi ya miaka 42.
(Angalia pia Muhtasari wa Ugumba.)
Ovari zina mayai, na mayai yote ambayo mwanamke atakuwa nayo yapo kwenye ovari anapozaliwa. Hakuna mayai mapya yanayozalishwa baadaye maishani. Idadi na ubora wa mayai (hifadhi ya ovari) inaweza kuanza kupungua katika umri wa miaka 30 au hata mapema zaidi. Hupungua kwa haraka baada ya umri wa miaka 40. Lakini umri si sababu pekee inayosababisha idadi na ubora wa mayai kupungua. Matatizo katika ovari pia yanaweza kusababisha kupungua huko.
Katika upungufu wa ovari wa msingi (wakati mwingine huitwa ukomo wa hedhi mapema), idadi ya mayai kwenye ovari hupungua katika umri mdogo. Kwa wanawake wachache, upungufu wa ovari ndiyo sababu ya kupata hedhi isiyo ya kawaida au kutopata hedhi kabisa.
Utambuzi wa Matatizo Kwa Mayai
Vipimo vya damu ili kupima viwango vya homoni fulani
Atrasonografia
Madaktari wanaweza kuwapima wanawake wafuatao ili kubaini iwapo wana matatizo ya mayai:
Wale walio na umri wa miaka 35 au zaidi
Wale ambao wamefanyiwa upasuaji wa ovari
Wale ambao hawajaitikia vyema dawa za uzazi (kama vile gonadotropini) ambazo huchochea mayai kadhaa kukomaa na kutolewa
Madaktari wanaweza kupima viwango vya homoni ya kuchochea foliko na estrojeni katika damu kwa wakati fulani wakati wa mzunguko wa hedhi. (Homoni ya kuchochea foliko huchochea kutolewa kwa mayai.) Kuongezeka kwa viwango vya homoni ya kuchochea foliko na kupungua kwa viwango vya estrojeni mwanzoni mwa mzunguko wa hedhi huonyesha tatizo la mayai.
Vipimo vya kuaminika zaidi vya kugundua matatizo ya mayai ni
Vipimo vya damu ili kupima viwango vya homoni ya antimullerian (AMH), ambayo huzalishwa na vinyweleo (vifuko vilivyojaa kiowevu kwenye ovari ambayo ina yai)
Ultrasonografia kwa kutumia kifaa cha kipimo cha picha kinachotumia mawimbi ya sauti ambacho huwekwa ndani ya uke (ultrasonografia ya uke) kuangalia na kuhesabu idadi ya vinyweleo
Kiwango cha chini cha homoni ya antimullerian kinaonyesha kuwa idadi ya vinyweleo ni ndogo. Idadi ndogo ya folikoli (zinazozingatiwa na kuhesabiwa wakati wa kipimo cha picha kinachotumia mawimbi ya sauti) inamaanisha kuwa ujauzito baada ya utungishaji mimba kwenye maabara una uwezekano mdogo lakini bado unawezekana.
Hata hivyo, mimba inaweza kutokea hata ikiwa matokeo ya vipimo si ya kawaida.
Matibabu ya Matatizo Kwa Mayai
Matibabu kulingana na hali na umri wa mwanamke
Kwa sababu mimba inaweza kutokea, madaktari wanapendekeza matibabu tofauti kwa kila mwanamke kulingana na hali na umri wake. Matibabu kama hayo yanaweza kujumuisha yale yanayotumika kutibu matatizo ya utoaji wa mayai, kama vile clomiphene, letrozole na gonadotropini za binadamu.
Ikiwa wanawake wana umri wa zaidi ya miaka 42 au ikiwa idadi au ubora wa mayai umepungua, kutumia mayai kutoka kwa mwanamke mwingine (mtoaji), ikiwa yanapatikana, inaweza kuwa chaguo.