Saratani ya Ovari, Saratani ya Mrija wa Uzazi, na Saratani ya Kitambi cha tumbo

NaPedro T. Ramirez, MD, Houston Methodist Hospital;
Gloria Salvo, MD, MD Anderson Cancer Center
Imekaguliwa naOluwatosin Goje, MD, MSCR, Cleveland Clinic, Lerner College of Medicine of Case Western Reserve University
Imepitiwa/Imerekebishwa Oct 2023 | Imebadilishwa Aug 2025
v806269_sw

Saratani ya ovarini saratani inayotokea kwenye ovari. Inahusiana na saratani ya mirija ya fallopia, ambayo hukua kwenye mirija inayotoka ovari hadi kwenye uterasi, na saratani ya utando wa tumbo, ambayo ni saratani ya tishu zilizo kwenye utando wa tumbo. Saratani hizi kwa kawaida hugunduliwa katika hatua iliyoendelea.

  • Saratani ya ovari huenda isisababishe dalili hadi itakapoenea.

  • Ikiwa madaktari wanashuku saratani ya ovari, vipimo vya damu, ultrasonografia na picha ya mwangwi wa sumaku au tomografia ya kompyuta hufanywa.

  • Kwa kawaida, ovari zote, mirija yote ya fallopia na uterasi huondolewa.

  • Tibakemikali mara nyingi inahitajika baada ya upasuaji.

(Angalia pia Muhtasari wa Saratani za Mfumo wa Uzazi wa Kike.)

Saratani ya ovari (kasinoma ya ovari) hutokea mara nyingi zaidi kwa wanawake wenye umri wa miaka 50 hadi 70. Nchini Marekani, saratani ya ovari ndiyo saratani ya pili kwa ukawaida katika wanawake, inayojitokeza kwa takriban mwanamke 1 kati ya 70. Ni chanzo cha tano cha vifo vya saratani kwa wanawake na, nchini Marekani, itasababisha takriban visa vipya 19,710 na vifo 13,270 mwaka wa 2023.

Kwa sababu saratani ya ovari na mirija ya fallopia ina sifa nyingi (dalili, utambuzi, na matibabu), kwa kawaida huzingatiwa pamoja. Saratani inayoanzia kwenye mirija ya fallopia ni nadra.

Anatomia ya Ndani ya Uzazi ya Mwanamke

Kuna aina nyingi za saratani ya ovari. Hukua kutoka kwa aina nyingi tofauti za seli kwenye ovari. Saratani zinazoanzia sehemu ya juu ya ovari (kasinoma za epithelial) huchangia zaidi ya 90%. Saratani zingine nyingi za ovari huanza kutoka kwa seli zinazozalisha mayai (zinazoitwa uvimbe wa seli zazi) au kwenye tishu zinazounganisha (zinazoitwa uvimbe wa seli za stroma). Uvimbe wa seli zazi kwa kawaida hutokea kwa wanawake walio chini ya umri wa miaka 30.

Wakati mwingine saratani kutoka sehemu zingine za mwili huenea hadi kwenye ovari.

Saratani ya ovari inaweza kuenea kama ifuatavyo:

  • Moja kwa moja hadi eneo la karibu

  • Kupitia kuenea kwa seli za saratani kutoka sehemu nyingine hadi kwenye tumbo

  • Kupitia mfumo wa limfu hadi sehemu zingine za fupanyonga na tumbo

  • Mara chache sana, hupitia kwenye damu, hatimaye huonekana katika sehemu za mbali za mwili, hasa ini na mapafu

Viashiria vya Hatari vya Saratani ya Ovari

Mambo yanayoongeza hatari ya kupata saratani ya ovari ni pamoja na yafuatayo:

  • Kuwa mzee (muhimu zaidi)

  • Kuwa na jamaa wa karibu (mama, dada, au binti) ambaye amewahi kuwa na saratani ya ovari

  • Kutozaa watoto wowote

  • Kupata mtoto wa kwanza ukiwa mzee

  • Kuanza kutokwa na hedhi mapema

  • Kuchelewa kwa ukomo hedhi

  • Kuwa na saratani ya uterasi, matiti, au utumbo mpana (koloni) au kuwa na mwanafamilia ambaye amewahi kuwa na moja ya saratani hizi

Matumizi ya dawa zinazomezwa za kuzuia mimba hupunguza hatari kwa kiasi kikubwa.

Takriban 15% ya visa vya saratani ya ovari vinahusiana na mabadiliko ya jeni za BRCA1 na BRCA2, ambazo pia zinahusika katika baadhi ya saratani ya matiti. Wakati mabadiliko ya jeni hizi au mabadiliko mengine adimu ya jeni yanapohusika, saratani ya ovari na matiti hutokea katika familia. Saratani kama hizo wakati mwingine huitwa magonjwa ya kurithi ya saratani ya matiti na ovari. Kwa wanawake ambao wana mabadiliko ya jeni ya BRCA1, hatari ya kupata saratani ya ovari katika maisha yote ni 20 hadi 40%. Hatari huongezeka kidogo kwa wanawake wenye mabadiliko ya jeni ya BRCA2. Mabadiliko ya jeni ya BRCA1 na BRCA2 ni ya kawaida zaidi miongoni mwa wanawake Wayahudi wa Ashkenazi kuliko idadi ya watu kwa ujumla.

Dalili za Saratani ya Ovari

Saratani ya ovari husababisha ovari iliyoathiriwa kuongezeka ukubwa. Kwa wanawake vijana, kuongezeka ukubwa kwa ovari kunaweza kusababishwa na mfuko usio na saratani uliojaa majimaji (uvimbe wa ovari). Hata hivyo, baada ya kukoma hedhi, ovari iliyoongezeka ukubwa inaweza kuwa ishara ya saratani ya ovari.

Wanawake wengi hawaonyeshi dalili hadi pale saratani itakapofikia hatua za juu. Dalili zinapoonekana, huwa za jumla. Hizi ni pamoja na usumbufu wa tumbo, kuvimbiwa, kupoteza hamu ya kula, hisia ya kushiba mapema, mabadiliko ya mazoea ya kwenda haja kubwa, na kukojoa mara kwa mara.

Hatimaye, tumbo linaweza kuvimba kwa sababu ovari huongeza ukubwa au majimaji hujikusanya kwenye tumbo (inayoitwa ascites). Katika hatua hii, maumivu katika eneo la fupanyonga, anemia, na kupunguza uzani ni jambo la kawaida.

Mara chache, uvimbe wa seli zazi au seli za stroma hutoa estrojeni, ambayo inaweza kusababisha tishu kwenye utando wa uterasi kukua kupita kiasi na matiti kuomgeza ukubwa. Au uvimbe huu unaweza kutoa homoni za kiume (androjeni), ambazo zinaweza kusababisha nywele za mwili kukua kupita kiasi, au homoni zinazofanana na homoni za tezi, ambazo zinaweza kusababisha dalili za tezi ya dundumio inayofanya kazi kupita kiasi (homoni nyingi kupita kiasi kwenye dundumio (hyperthyroidism)).

Utambuzi wa Saratani ya Ovari

  • Atrasonografia

  • Wakati mwingine tomografia ya kompyuta au upigaji picha wa mwangwi wa sumaku

  • Vipimo vya damu

Kutambua saratani ya ovari katika hatua zake za mwanzo ni vigumu kwa sababu dalili kwa kawaida hazionekani hadi saratani iwe kubwa sana au imeenea nje ya ovari na kwa sababu magonjwa mengi yasiyo makubwa sana husababisha dalili zinazofanana.

Ikiwa madaktari watagundua ovari iliyoongezeka ukubwa wakati wa uchunguzi wa kimwili au wanashuku saratani ya ovari mapema kulingana na dalili, uchunguzi wa kipimo cha ultrasonografia hufanywa kwanza. Wakati mwingine tomografia ya kompyuta (CT) au upigaji picha kwa mwangwi wa sumaku (MRI) hutumiwa kusaidia kutofautisha uvimbe wa ovari kutoka kwa uvimbe mgumu wa saratani. Ikiwa saratani iliyoendelea inashukiwa, CT au tomografia ya utoaji wa positron (PET) kwa kawaida hufanywa kabla ya upasuaji ili kubaini kiwango cha saratani.

Ikiwa saratani inaonekana haipo, madaktari humchunguza mwanamke huyo mara kwa mara.

Ikiwa madaktari wanashuku saratani au matokeo ya vipimo hayako wazi, vipimo vya damu kwa kawaida hufanywa ili kupima viwango vya dutu vinavyoweza kuashiria uwepo wa saratani (alama za uvimbe), kama vile antijeni ya saratani 125 (CA 125). Viwango visivyo vya kawaida vya alama za uvimbe pekee havithibitishi utambuzi wa saratani, lakini vinapojumuishwa na taarifa nyingine, vinaweza kusaidia katika utambuzi.

Uchunguzi wa biopsi hufanywa ili kuthibitisha utambuzi wa saratani ya ovari na, ikiwa utambuzi umethibitishwa, ili kubaini aina ya saratani. Madaktari huchunguza ovari na viungo vingine kwenye tumbo na fupanyonga (ili kuangalia ueneaji). Utaratibu huu unafanywa kupitia mojawapo ya njia mbili:

  • Laparoskopia: Madaktari kwa kawaida hutumia mrija mwembamba na unaonyumbulika wa kutazama (laparoskopu) unaoingizwa kupitia mkato mdogo chini ya kitovu, hasa ikiwa wanafikiri saratani haijaendelea. Wanatumia vifaa vilivyounganishwa kupitia laparoskopu, wakati mwingine kwa usaidizi wa roboti, kuchukua sampuli kutoka kwa tishu zingine mbalimbali na kuchunguza ovari na viungo vingine. Taarifa zinazopatikana zinaweza kuwasaidia madaktari kubaini kama saratani imeenea na kwa kiwango gani (hatua yake). Ovari zinaweza pia kuondolewa ili kutibu saratani ya ovari kwa kutumia laparoskopi.

  • Upasuaji wazi: Ikiwa madaktari wanafikiri saratani inaweza kuwa imefika hatua ya juu, wanafanya mkato tumboni na kutazama moja kwa moja uterasi na tishu zinazoizunguka. Wanabaini hatua ya saratani na kuondoa saratani nyingi kadri iwezekanavyo.

Madaktari huzingatia kupendekeza upimaji wa jeni kwa mwanamke yeyote anayetambuliwa kuwa na saratani ya ovari (au mirija ya fallopia). Madaktari pia huuliza kuhusu saratani ambazo wanafamilia wowote wamewahi kuwa nazo. Taarifa hii inaweza kuwasaidia madaktari kutambua wanawake ambao wana uwezekano mkubwa wa kuwa na aina ya saratani ya kurithi, kama ile inayosababishwa na mabadiliko ya jeni katika jeni ya BRCA.

Kuweka daraja saratani ya ovari, mrija wa uzazi na peritoneal

Upasuaji wa kuondoa saratani ya ovari na falopia unajumuisha kuondolewa kwa uterasi, ovari, na mirija ya falopia.

Hutua hutegemea kiwango cha kuenea kwa saratani. Awamu zipo kati ya I (ya mapema zaidi) hadi IV (iliyoendelea):

  • Awamu ya I: Saratani hutokea tu katika ovari moja au zote mbili au mirija ya falopia.

  • Awamu ya II: Saratani imeenea hadi kwenye uterasi au tishu zilizo karibu ndani ya fupanyonga (ambayo ina viungo vya ndani vya uzazi, kibofu cha mkojo, na rektamu) au hutokea tu kwenye utando wa viungo vya tumbo.

  • Awamu ya III: Saratani imeenea nje ya fupanyonga hadi kwenye nodi za limfu na/au hadi sehemu zingine za tumbo (kama vile sehemu ya juu ya ini au wengu).

  • Awamu ya IV: Saratani imeenea hadi maeneo ya mbali (kwa mfano, hadi kwenye mapafu).

Matibabu ya Saratani ya Ovari

  • Kwa kawaida kuondolewa kwa ovari, mirija ya fallopia na uterasi

  • Kuondolewa kwa tishu zote zinazoonekana kuathiriwa (upasuaji wa kupunguza ukubwa)

  • Kwa kawaida tibakemikali

Kiwango cha upasuaji hutegemea aina ya saratani ya ovari na mirija ya falopia na hatua yake.

Saratani ya ovari na mirija ya falopia inapotambuliwa kwa mara ya kwanza, kwa kawaida huenea kwenye tumbo lote, kwa hivyo matibabu kwa kawaida huhusisha mojawapo ya yafuatayo:

  • Upasuaji ili kuondoa uvimbe mwingi kadri iwezekanavyo, ikifuatiwa na tibakemikali

  • Tibakemikali, ikifuatiwa na upasuaji na tibakemikali zaidi

Kwa saratani nyingi za ovari na mirija ya falopia, matibabu huhusisha kuondoa ovari na mirija ya falopia (salpingo-oophorectomy) na kuondoa uterasi (hysterectomy). Upasuaji wa laparoskopi au upasuaji wa laparoskopi unaofanywa kwa kutumia roboti unaweza kufanywa kwanza ili kubaini kama upasuaji mkubwa zaidi ni chaguo linalofaa. Ikiwa sivyo, tibakemikali huanzishwa.

Wakati saratani imeenea nje ya ovari, nodi za limfu zilizo karibu na sehemu zilizo karibu ambapo saratani huenea pia huondolewa. Mbinu hii inalenga kuondoa saratani yote inayoonekana.

Ikiwa mwanamke ana saratani ya hatua ya kwanza inayoathiri ovari moja tu na anataka kupata mimba, madaktari wanaweza kuondoa ovari na mirija ya falopia iliyoathiriwa pekee.

Kwa saratani zilizofika hatua ya juu zaidi ambazo zimeenea kwenye sehemu zingine za mwili, madaktari kwa kawaida huondoa saratani nyingi iwezekanavyo ili kuongeza muda wa kuishi. Aina hii ya upasuaji huitwa upasuaji wa kupunguza ukubwa. Hata hivyo, kulingana na mahali ambapo saratani imeenea na kiasi cha saratani kilichopo, wanawake wanaweza kutibiwa kwa tibakemikali badala ya au kabla na baada ya upasuaji.

Baada ya upasuaji, wanawake wengi wenye kasinoma ya epithelia ya hatua ya I isiyo kali sana hawahitaji matibabu zaidi. Kwa saratani zingine za hatua ya I au kwa saratani zilizoendelea zaidi, tibakemikali inaweza kutumika kuharibu maeneo yoyote madogo ya saratani ambayo yanaweza kubaki.

Wanawake wengi wenye uvimbe wa seli zazi wanaweza kuponywa kwa kuondolewa kwa ovari moja iliyoathiriwa na mirija ya falopia pamoja na mchanganyiko wa dawa mbili au zaidi za tibakemikali. Tiba ya mionzi haitumiki sana.

Saratani ya ovari iliyofika hatua ya juu kwa kawaida hurjirudia. Kwa hivyo baada ya tibakemikali, madaktari kwa kawaida hupima viwango vya alama za saratani (kama vile CA 125). Viwango vya alama za saratani vinavyobaki juu kwa kawaida humaanisha kwamba baadhi ya uvimbe upo.

Ikiwa saratani inarejea baada ya tibakemikali kuonekana kuwa na ufanisi, tibakemikali hurudiwa. Dawa nyingi tofauti za tibakemikali au mchanganyiko wa dawa zinaweza kutumika.

Ubashiri wa Saratani ya Ovari

Ubashiri wa saratani ya ovari kwa wanawake unategemea hatua.

Ubashiri huwa mbaya zaidi saratani inapokuwa kali zaidi au upasuaji unaposhindwa kuondoa tishu zote zenye kasoro. Saratani hurejea kwa takriban 70% ya wanawake ambao wamewahi kuwa na saratani ya hatua ya III au IV.

Kinga ya Saratani ya Ovari

Hakuna kipimo cha uchunguzi wa saratani ya ovari au mirija ya falopia. Hata hivyo, baadhi ya wataalamu wanaamini kwamba ikiwa saratani ya ovari au ya matiti hutokea katika familia, wanawake wanapaswa kupimwa kwa kasoro za kijenetiki. Ikiwa jamaa wa karibu au familia pana wana saratani kama hiyo, haswa miongoni mwa familia za Wayahudi wa Ashkenazi, wanawake wanapaswa kujadili upimaji wa jeni kwa kasoro za BRCA na madaktari wao.

Wanawake wenye mabadiliko fulani ya jeni ya BRCA wanaweza kupewa chaguo la kuondoa ovari na mirija ya falopia, hata wakati hakuna saratani iliyopo. Mbinu hii huondoa hatari ya saratani ya ovari na hupunguza hatari ya saratani ya matiti.

Je, Ulijua...

  • Ikiwa wanawake wana jamaa wa karibu au familia pana wenye saratani ya ovari au matiti, wanapaswa kumuuliza daktari wao kuhusu upimaji wa jeni kwa kasoro za BRCA.

Taarifa Zaidi

Nyenzo zifuatazo za lugha ya Kiingereza zinaweza kuwa muhimu. Tafadhali kumbuka kuwa MWONGOZO hauwajibiki kwa maudhui ya nyenzo hizi.

  1. Taasisi ya Saratani ya Wanawake: Tovuti hii inatoa viungo vya taarifa kuhusu saratani ya wanawake, majaribio ya kimatibabu (ikiwa ni pamoja na kutafuta jaribio la kushiriki), na utafiti. Pia hutoa kozi kuhusu masuala ya saratani na hushiriki hadithi za binafsi za mapambano ya wanawake na saratani.

  2. Taasisi ya Kitaifa ya Saratani: Saratani: Ovari, Mrija wa Fallopia, na Saratani ya Msingi ya Utando wa Tumbo: Tovuti hii inatoa viungo vya taarifa za jumla kuhusu saratani ya ovari, mirija ya falopia, na saratani ya msingi ya utando wa tumbo, pamoja na viungo vya taarifa kuhusu sababu, uzuiaji, uchunguzi, matibabu, na utafiti na kuhusu kukabiliana na saratani.

  3. Taasisi ya Kitaifa ya Saratani: BRCA1 na BRCA2: Hatari ya Saratani na Upimaji wa Jeni: Tovuti hii inatoa taarifa kuhusu jeni za BRCA, manufaa na madhara yanayoweza kutokea katika upimaji wa jeni, na matokeo ya kuwa na mabadiliko ya kijeni ya BRCA.