Maambukizi ya Meningokokali

NaLarry M. Bush, MD, FACP, Charles E. Schmidt College of Medicine, Florida Atlantic University;
Maria T. Vazquez-Pertejo, MD, FACP, Wellington Regional Medical Center
Imekaguliwa naBrenda L. Tesini, MD, University of Rochester School of Medicine and Dentistry
Imepitiwa/Imerekebishwa Jul 2024 | Imebadilishwa Jul 2025
v38987305_sw

Maambukizi ya meningokokali husababishwa na bakteria Neisseria meningitidis (meningokosi) na hujumuisha homa ya uti wa mgongo na sepsisi.

  • Maambukizi huenea kwa kugusa moja kwa moja majimaji ya pua na koo.

  • Watu hujihisi wagonjwa kwa ujumla na huwa na dalili nyingine ambazo ni mbaya wakati mwingi, kulingana na eneo lililoambukizwa.

  • Kutambua bakteria katika damu au katika sampuli inayotolewa kwenye tishu zilizoambukizwa huthibitisha utambuzi.

  • Dawa za kuua bakteria na viowevu lazima vitolewe kwa kudungwa kwenye mishipa ya damu haraka iwezekanavyo.

  • Chanjo inaweza kusaidia kuzuia maambukizi ya meningokokali.

Maambukizi mengi ya meningokokali ni

  • Homa ya uti wa mgongo: Maambukizi ya tishu zinazofunika ubongo na uti wa mgongo (meninge)

  • Sepsisi: Maambukizi ya mzunguko wa damu (yanayoitwa meningokosemia yanaposababishwa na meningokosi)

Maambukizi ya mapafu, viungo, macho, moyo, rektamu na viungo vya mifumo ya uzazi na mkojo yanaweza kutokea lakini si ya kawaida sana.

Katika maeneo yenye halijoto wastani, maambukizi mengi ya meningokokali hutokea wakati wa majira ya baridi na ya kuchipua. Milipuko ya ndani inaweza kutokea, mara nyingi zaidi katika Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara kuanzia Senegali hadi Ethiopia. Eneo hili, ambalo linajumuisha nchi 26, linajulikana kama ukanda wa homa ya uti wa mgongo.

Meningokosi hukaa kwenye koo na pua za baadhi ya watu bila kusababisha dalili. Watu hao huitwa waenezaji. Mara nyingi watu huwa waenezaji baada ya milipuko. Hata hivyo, maambukizi kwa kawaida hutokea kwa watu ambao hawajawahi kuambukizwa meningokosi hapo awali, badala ya waenezaji. Maambukizi huenea kwa kugusa moja kwa moja majimaji ya pua na koo ya mtu aliyeambukizwa (ikiwa ni pamoja na waenezaji).

Watu wanaoambukizwa zaidi ni

Maambukizi pia ni ya kawaida zaidi miongoni mwa

  • Vijana na watu wazima wenye umri mdogo (umri wa miaka 16 hadi 20)

  • Makuruta wa jeshi

  • Wanafunzi wa mwaka wa kwanza wa chuo kikuu wanaoishi katika mabweni

  • Wasafiri wanaoenda maeneo ambapo ugonjwa wa meningokokali hutokea mara kwa mara

  • Watu walio na maambukizi ya VVU

  • Wanaume wanaofanya ngono na wanaume

  • Watu ambao wengu wao umeondolewa au kuharibika

  • Watu ambao hawana protini za kujalizia za kutosha, zinazosaidia mfumo wa kinga

  • Watu wanaotumia eculizumab au ravulizumab (dawa zinazozuia sehemu ya mfumo wa kinga inayoitwa mfumo wa kujalizia)

  • Wataalamu wa maikrobiolojia wanaofanya kazi inayohusiana na meningokosi

  • Watu wanaoingiliana kwa karibu ya watu walio na maambukizi ya meningokokali

Mambo mengine ambayo yanaweza kuongeza hatari ya maambukizi ya meningokokali ni pamoja na kupata maambukizi ya virusi, kuishi katika nyumba yenye watu wengi, kuwa na ugonjwa sugu, na kuvuta sigara au kuathiriwa na moshi wa sigara (kutovuta sigara moja kwa moja).

Milipuko ya maambukizi ya meningokokali ni nadra nchini Marekani na inachangia asilimia ndogo tu ya visa. Milipuko kwa kawaida hutokea miongoni mwa watu wanaotumia muda au wanaoishi katika makazi ya karibu na wengine, kwa mfano, katika mabweni, shule au vituo vya kutunza watoto mchana, na mara nyingi huwahusisha watu wenye umri wa miaka 16 hadi 23.

Dalili za Maambukizi ya Meningokokali

Watu wengi wenye maambukizi ya meningokokali hujihisi wagonjwa sana.

Homa ya uti wa mgongo mara nyingi husababisha joto jingi mwilini, maumivu ya kichwa, vipele vyekundu na shingo ngumu. Pia inaweza kusababisha kichefuchefu, kutapika na kuathiriwa kupita kiasi na mwanga.

Watoto wachanga wanaweza kuwa na matatizo ya kula na kulia kwa udhaifu, na wanaweza kuwa na hasira na kuonyesha uvivu.

Maambukizi ya mtiririko wa damu yanaweza kusababisha upele wenye madoadoa mekundu au ya zambarau. Maambukizi makali yanaweza kusababisha sepsisi, ambayo huwa na sifa za shinikizo la damu la chini sana (mshtuko), uwezekano mkubwa wa kutokwa na damu, na kutofanya kazi vizuri kwa viungo vingi (kama vile figo na ini).

Kwa nadra, maambukizi ya meningokolali husababisha ugonjwa sugu unaosababisha dalili zisizo kali na zinazojirudia ambazo kwa kiasi kikubwa huhusisha viungo na ngozi.

Utambuzi wa Maambukizi ya Meningokokali

  • Uchunguzi na kukuza seli za sampuli za damu au tishu nyingine zilizoambukizwa, ikiwa ni pamoja na majimaji ya uti wa mgongo na ubongo yanayopatikana kwa kuyatoa kwa sindano kwenye uti wa mgongo

  • Wakati mwingine mbinu ya mmenyuko wa mnyororo wa polimerasi

Madaktari hushuku maambukizi ya meningokokali kwa watu wenye dalili za kawaida, hasa ikiwa dalili zitatokea wakati wa mlipuko.

Ili kuthibitisha utambuzi, madaktari huchukua sampuli za damu au tishu nyingine zilizoambukizwa au kutoa majimaji ya uti wa mgongo (kuingiza sindano kwenye sehemu ya kiuno) ili kupata sampuli ya majimaji yanayozunguka ubongo na uti wa mgongo (majimaji ya uti wa mgongo na ubongo). Sampuli hizi huchunguzwa kwa hadubini ili kuangalia na kutambua bakteria. Sampuli pia hutumwa kwenye maabara, ambapo bakteria wanaweza kutambuliwa baada ya kukuzwa au vipimo vingine vya maabara kufanywa.

Ikiwa bakteria ni mgumu kukuza au matokeo mengine ya vipimo hayasadikiki, madaktari wanaweza kufanya vipimo ili kutambua vipande vya nyenzo za kijenetiki za bakteria. Vipimo vinavyogundua nyenzo za kijenetiki katika vijidudu huitwa vipimo vya asidi ya kiini. Mbinu ya mmenyuko wa mnyororo wa polimerasi (PCR) ni mfano wa aina hii ya kipimo. Mbinu ya PCR hufanywa kwenye sampuli za majimaji ya ubongo na uti wa mgongo, damu au tishu nyingine zilizoambukizwa. Inatumika kuzalisha nakala nyingi za jeni kutoka kwa bakteria, hivyo kufanya bakteria awe rahisi zaidi kutambuliwa.

Kipimo cha Maabara

Wakati mwingine madaktari hufanya vipimo vya damu vinavyogundua kingamwili za bakteria au kapsuli inayofunika bakteria. Hata hivyo, matokeo ya vipimo hivi bado yanapaswa kuthibitishwa kupitia kukuza seli.

Bakteria pia anaweza kupimwa ili kubaini ni dawa zipi za kuua bakteria zinazofanya kazi (mchakato unaoitwa upimaji wa uwezekano wa kuathiriwa).

Matibabu ya Maambukizi ya Meningokokali

  • Dawa za kuua bakteria zinazotolewa kwa kudungwa kwenye mshipa wa damu

  • Viowevu vinavyotolewa kwa kudungwa kwenye mshipa wa damu

  • Matumizi yanayowezekana ya dawa za kotikosteroidi

Kwa kawaida watu hulazwa katika kitengo cha wagonjwa mahututi na kupewa dawa za kuua bakteria na viowevu kwa kudungwa kwenye mishipa ya damu haraka iwezekanavyo, kabla madaktari hawajapata matokeo ya utaratibu wa kukuza bakteria yanayotambua kiumbe kinachosababisha maambukizi.

Ikiwa meningokosi itathibitishwa, madaktari hubadilisha dawa za kuua bakteria na kutumia zile ambazo vipimo vinaonyesha kuwa zitaleta ufanisi zaidi dhidi ya bakteria, kwa kawaida ceftriaxone au penicillin. Dawa hizi za kuua bakteria hutolewa kwa kudungwa kwenye mishipa ya damu.

Madaktari huwapatia watoto na watu wazima ambao wanashuku kuwa wana homa ya uti wa mgongo dawa za kotikosteroidi (kama vile dexamethasone) kwa sababu dawa hizi zinaweza kupunguza uharibifu wa neva unaosababishwa na maambukizi. Hata hivyo, ikiwa homa ya uti wa mgongo imesababishwa na Neisseria meningitidis, madaktari kwa kawaida wanaweza kuacha kutoa dawa za kotikosteroidi kwa sababu dawa hizi zinaonekana tu kuwasaidia watu ambao homa yao ya uti wa mgongo inasababishwa na Streptococcus pneumoniae au Haemophilus influenzae. Huenda dawa za kotikosteroidi zikahitaji kuendelea kutumika kwa watu ambao tezi zao za adrenali hazitoi kotikosteroidi cortisol ya kutosha.

Ubashiri wa Maambukizi ya Meningokokali

Kwa ujumla, homa ya uti wa mgongo ya meningokokali husababisha kifo kwa 10 hadi 15% ya watu.

Maambukizi mabaya ya meningokokali kwenye mtiririko wa damu yenye mshtuko wa septic husababisha kifo kwa hadi 40% ya watu.

Kati ya watu wanaopona kutokana na homa ya uti wa mgongo ya meningokokali, 10 hadi 20% hupata matatizo makubwa, kama vile kupoteza uwezo wa kusikia kabisa, ulemavu wa akili au matatizo ya maambukizi ya mtiririko wa damu, ikiwa ni pamoja na uozo wa vidole vya mikono, vidole vya miguu, au miguu na mikono, ambayo inaweza kuhitaji kukatwa.

Uzuiaji wa Maambukizi ya Meningokokali

Baada ya kushikwa na homa ya uti wa mgongo

Wanafamilia, wafanyakazi wa tiba na watu wengine waliokuwa na mwingiliano wa karibu na watu walio na maambukizi ya meningokokali wanapaswa kupewa dawa za kuua bakteria ili kuzuia maambukizi kutokea. Dawa za kuua bakteria zinaweza kutolewa kwa kumeza au kwa kudungwa sindano.

Kuchanja

Ili kupata maelezo zaidi, tazama pia Chanjo ya Meningokokali na ratiba za chanjo kwa watoto na vijana na watu wazima kutoka Vituo vya Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa (CDC).

Wakati wa mlipuko, chanjo ya meningokokali pia hutolewa (pamoja na dawa za kuua bakteria) kwa watu wanaoingiliana kwa karibu na mtu aliye na maambukizi ya meningokokali.

Taarifa Zaidi

Nyenzo zifuatazo za lugha ya Kiingereza zinaweza kuwa muhimu. Tafadhali kumbuka kuwa MWONGOZO hauwajibiki kwa maudhui ya nyenzo hizi.

Angalia tovuti zifuatazo za serikali ya Marekani kwa taarifa za kina kuhusu kila kitu kuanzia habari kuhusu milipuko na sababu za hatari hadi nyenzo za elimu na viungo vya haraka vya mada zinazohusiana:

  1. Vituo vya Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa (CDC): Ugonjwa wa Meningokokali

  2. CDC: Ratiba ya Chanjo kwa Watoto na Vijana kufikia Umri wa

  3. CDC: Ratiba ya chanjo za watu wazima kwa umri