Neuroblastoma

NaKee Kiat Yeo, MD, Harvard Medical School
Imekaguliwa naMichael SD Agus, MD, Harvard Medical School
Imepitiwa/Imerekebishwa Jun 2024 | Imebadilishwa Jul 2024
v822682_sw

Neuroblastoma ni saratani ya kawaida ya utotoni ambayo hukua katika sehemu za mfumo wa neva au tezi za adrenali.

  • Kinachosababisha neuroblastoma mara nyingi hakijulikani.

  • Dalili hutegemea mahali ambapo neuroblastoma imekua, kama vile tumbo, kifua, mfupa, ngozi, au uti wa mgongo.

  • Kwa kawaida utambuzi huhusisha kipimo cha picha na bayopsi.

  • Matibabu hutegemea umri wa mtoto na sifa maalum za saratani na inaweza kujumuisha upasuaji, tibakemikali na tiba kwa njia ya eksirei.

(Angalia pia Muhtasari wa Saratani ya Utotoni.)

Neuroblastoma hutokea katika aina fulani ya tishu za neva zilizo katika sehemu nyingi za mwili. Kwa kawaida huanzia kwenye neva za tumboni au kifuani, hasa katika tezi za adrenali (iko juu ya kila figo). Katika zaidi ya nusu ya watoto, saratani huwa imeenea hadi sehemu nyingine za mwili (kuenea maeneo mengine) kufikia wakati daktari anaposhauriwa.

Neuroblastoma ndiyo saratani ya kawaida kati ya watoto wachanga. Karibu 90% ya neuroblastoma zote hutokea kwa watoto walio chini ya umri wa miaka 5. Isipokuwa katika hali nadra sana, neuroblastoma hutokea kwa watoto pekee.

Kinachosababisha neuroblastoma mara nyingi hakijulikani. Uvimbe mwingi hutokea ghafla. Mara chache, neuroblastoma hurithiwa katika familia.

Je, Ulijua...

  • Neuroblastoma ndiyo saratani ya kawaida kati ya watoto wachanga.

Dalili za Neuroblastoma

Dalili za neuroblastoma hutegemea mahali ambapo neuroblastoma ilianzia na kama imeenea na ni wapi imeenea, kama ilivyo katika yafuatayo:

  • Inayoanzia tumboni: Dalili za kawaida ni pamoja na tumbo kubwa, hisia ya kujaa, kupungua kwa hamu ya kula, na maumivu ya tumbo.

  • Inayoanzia kifuani au shingoni: Mtoto anaweza kukohoa au kupata shida kupumua.

  • Kuenea hadi kwenye mifupa: Mtoto ana maumivu ya mifupa. Ikiwa saratani itafikia uboho, idadi ya aina mbalimbali za seli za damu inaweza kupungua, na kusababisha dalili nyingine. Kwa mfano, kupungua kwa idadi ya seli nyekundu za damu (anemia) husababisha uchovu na wakati mwingine ngozi iliyopauka (iliyokwajuka). Kupungua kwa idadi ya chembe za damu husababisha michubuko rahisi na madoa madogo ya zambarau kwenye ngozi. Kupungua kwa idadi ya seli nyeupe za damu huongeza hatari ya maambukizi.

  • Kuenea hadi kwenye ngozi: Vipu huonekana.

  • Kuenea hadi kwenye uti wa mgongo: Mikono na miguu inaweza kuhisi dhaifu na yenye ganzi, au watoto huenda wasiweze kudhibiti baadhi ya sehemu za mwili kwa hiari.

Mara chache sana, watoto huwa na dalili za ugonjwa unaoitwa ugonjwa wa Horner. Katika ugonjwa wa Horner, uvimbe shingoni husukuma mishipa inayoathiri upande mmoja wa uso. Watoto huwa na kope lililoinama, mboni dogo, na kutokwa na jasho kidogo upande mmoja wa uso.

Neublastoma nyingi hutoa katekolamini. Katekolamini ni homoni zinazoongeza mapigo ya moyo na kusababisha wasiwasi. Magonjwa mengine yanayohusiana na saratani (yanayoitwa magonjwa ya paraneoplastiki) yanaweza kutokea, kama vile mwendo wa macho usiodhibitiwa (opsoclonus) na mikazo ya haraka ya mikono na miguu (myoclonus), kuhara maji, au shinikizo la juu la damu.

Utambuzi wa Neuroblastoma

  • Tomografia ya kompyuta (CT) au upigaji picha kwa mwangwi wa sumaku (MRI)

  • Biopsi

  • Wakati mwingine uchanganuzi wa uboho na vipimo vya mkojo

Neuroblastoma hupatikana sana watoto wanapotathminiwa kwa dalili walizonazo.

Kabla ya kuzaliwa, tafiti za kawaida za picha za mawimbi ya sauti kabla ya kujifungua mara kwa mara hutambua neuroblastoma katika kijusi.

Baada ya kuzaliwa, ikiwa saratani imekua vya kutosha, daktari anaweza kuhisi uvimbe tumboni mwa mtoto.

Daktari anayeshuku neuroblastoma hufanya CT au MRI ya tumbo. Ikiwa uvimbe unapatikana, sampuli inachukuliwa na kupelekwa kwenye maabara kwa uchunguzi (bayopsi). Sampuli ya uboho inaweza kuchukuliwa ili kutafuta seli za saratani (angalia Uchunguzi wa Uboho).

Sampuli ya mkojo inaweza kupimwa kwa viwango vya juu kupita kiasi vya katekolamini (ambayo inaweza kutengenezwa na uvimbe).

Ili kuona iwapo saratani imeenea, daktari anaweza kufanya yafuatayo:

  • CT au MRI ya tumbo, fupanyonga, na kifua, na wakati mwingine ubongo

  • Uchunguzi wa sampuli ya tishu au seli kwa bonge lolote lililotambuliwa

  • Uchunguzi wa sampuli ya uboho

  • Uchunguzi wa mfupa au uchunguzi unaotumia nyenzo yenye mionzi nunurishi inayojulikana kama metaiodobenzylguanidine (MIBG) ambayo husaidia madaktari kuona kama neuroblastoma imeenea

Daktari hutumia taarifa hizi zote kubaini kama uvimbe una hatari ndogo, hatari ya wastani au hatari kubwa.

Matibabu ya Neuroblastoma

  • Kuondolewa kwa njia ya upasuaji

  • Tibakemikali

  • Wakati mwingine tiba ya mionzi

  • Wakati mwingine upandikizaji wa seli shina

  • Tiba ya kingamaradhi

(Angalia pia Kanuni za Matibabu ya Saratani.)

Matibabu ya neuroblastoma yanategemea aina ya hatari.

Neuroblastoma ambayo haijaenea na ina hatari ndogo mara nyingi inaweza kuondolewa na kuponywa kupitia upasuaji.

Watoto walio na ugonjwa wa hatari ya wastani au hatari kubwa hupewa tibakemikali kama vile vincristine, cyclophosphamide, doxorubicin, etoposide na cisplatin.

Tibakemikali ya kiwango cha juu na uhamishaji wa seli shina hutumika mara nyingi kwa watoto walio na ugonjwa wenye hatari kubwa. Ili kupunguza hatari ya saratani kurudi baada ya tibakemikali ya kiwango cha juu na uhamishaji wa seli shina, watoto hawa hupewa retinoidi, ambayo ni kemikali inayohusiana na vitamini ya A.

Tiba kwa njia ya eksirei inaweza kutumika kwa watoto walio na ugonjwa wa hatari ya wastani au wakati uvimbe hauwezi kufanyiwa upasuaji na ni matibabu ya kawaida kwa uvimbe kwa watoto walio na ugonjwa wenye hatari ya juu.

Tiba ya kinga mwili hutumika kutibu watoto walio na ugonjwa wenye hatari ya juu. Tiba hii husaidia kuchochea mfumo wa kinga mwili dhidi ya saratani.

Ubashiri wa Neuroblastoma

Ubashiri hutegemea mambo kadhaa kama vile umri wa mtoto wakati wa utambuzi, kama uvimbe umeenea, na sifa fulani za uvimbe zinazoitwa sifa za kibayolojia (kwa mfano, jinsi uvimbe unavyoonekana chini ya hadubini na baadhi ya sifa za DNA ndani ya seli za uvimbe). Watoto wadogo ambao saratani ambayo haijaenea wana ubashiri bora zaidi.

Viwango vya uwezekano wa kuishi kwa watoto walio na ugonjwa wenye hatari ya chini na hatari ya wastani ni takriban 90 hadi 95%.

Kiwango cha uwezekano wa kuishi kwa watoto walio na ugonjwa wenye hatari ya juu kilikuwa karibu 15% lakini kimeimarika hadi zaidi ya 50% kwa kutumia mbinu mpya na zilizoimarishwa za tiba mchanganyiko.

Taarifa Zaidi

Nyenzo zifuatazo za lugha ya Kiingereza zinaweza kuwa muhimu. Tafadhali kumbuka kuwa Mwongozo hauwajibiki kwa maudhui ya nyenzo hizi.

  1. The American Cancer Society: Ikiwa Mtoto Wako Ametambuliwa kuwa na Saratani: Rasilimali kwa wazazi na wapendwa wa mtoto ambaye ana saratani ambayo hutoa taarifa kuhusu jinsi ya kukabiliana na baadhi ya matatizo na maswali yanayojitokeza mara tu baada ya mtoto kugunduliwa na ugonjwa huo