Ependymomas

NaKee Kiat Yeo, MD, Harvard Medical School
Imekaguliwa naMichael SD Agus, MD, Harvard Medical School
Imepitiwa/Imerekebishwa Jun 2024 | Imebadilishwa Jul 2024
v26516859_sw

Ependymoma ni uvimbe unaokua polepole unaotokana na seli kuzunguka nafasi ndani ya ubongo (ventrikali) au uti wa mgongo. Ependymoma kwa kawaida huwa saratani (inayodhuru).

  • Chanzo cha ependymoma hakijulikani.

  • Dalili hutegemea eneo la uvimbe na zinaweza kujumuisha maumivu ya kichwa, kutapika, uchovu na matatizo ya kuwa na usawa.

  • Utambuzi hufanywa kwa kutumia kipimo cha picha na sampuli ya tishu na seli.

  • Matibabu ni pamoja na upasuaji, tiba kwa njia ya eksirei, na wakati mwingine tibakemikali.

  • Utabiri wa ugonjwa hutegemea umri wa mtoto na kiasi cha saratani kinachoondolewa.

Ependymoma ndio uvimbe kuu wa tatu wa mfumo mkuu wa neva kwa watoto, na kuchangia 10% ya uvimbe wa ubongo kwa watoto. (Mfumo mkuu wa neva unajumuisha ubongo na uti wa mgongo.) Watoto wengi wanaotambuliwa kuwa na ependymoma huwa na umri wa takriban miaka 6. Hata hivyo, takriban 30% ya visa hutokea kwa watoto walio chini ya umri wa miaka 3.

Kwa watoto, ependymoma nyingi hukua ndani au karibu na eneo nyuma ya ubongo chini ya fuvu linaloitwa fosa ya nyuma ya fuvu. Eneo hili lina serebelamu (ambayo husaidia kudhibiti uratibu na usawa) na shina la ubongo (ambalo hudhibiti kazi muhimu za mwili kama vile kupumua).

Ependymoma pia hutokea katika sehemu ya juu ya ubongo inayoitwa eneo la sehemu ya juu ya tentoriamu ya serebeli. Eneo hili lina ubongombele, nafasi zilizojaa maji (ventrikali), choroid plexus, hipothalamasi, tezi ya pineal, tezi ya pituitari na neva ya macho.

Wakati mwingine ependymoma hukua kwenye uti wa mgongo.

Dalili za Ependymomas

Dalili za ependymoma hutegemea eneo la uvimbe.

Kwa ependymomas katika eneo la sehemu ya juu ya tentoriamu ya serebeli, dalili zinaweza kujumuisha mabadiliko ya hisia au nafsi, ugumu wa kumakinika, maumivu ya kichwa, kifafa, na utendaji usio wa kawaida wa eneo mahususi la mwili.

Kwa ependymoma katika fosa ya nyuma ya fuvu, dalili kwa kawaida huhusiana na shinikizo lililoongezeka ndani ya fuvu la kichwa (shinikizo la ndani ya fuvu). Huenda watoto wachanga wasifikie hatua muhimu za ukuaji. Wanaweza kuwa na hasira kali, kuwa na mzingo wa kichwa ulioongezeka, na hawana hamu ya kula. Watoto wakubwa huwa na kichefuchefu, kutapika, maumivu ya kichwa, uchovu, na matatizo ya usawa, uratibu na kutembea.

Kwa ependymoma kwenye uti wa mgongo, dalili zinaweza kujumuisha maumivu ya mgongo, udhaifu, ganzi/mchonyoto na ugumu wa kudhibiti haja ndogo na haja kubwa.

Utambuzi wa Ependymomas

  • Upigaji picha kwa mwangwi wa sumaku (MRI) na uchunguzi wa sampuli ya tishu na seli

Utambuzi wa ependymoma unategemea matokeo ya MRI.

Ikiwa uvimbe unapatikana, sampuli inachukuliwa na kupelekwa kwenye maabara kwa uchunguzi (bayopsi).

Matibabu ya Ependymomas

  • Upasuaji, tiba kwa njia ya eksirei, na wakati mwingine tibakemikali

(Angalia pia Kanuni za Matibabu ya Saratani.)

Madaktari kwanza huondoa kwa upasuaji kiasi kikubwa cha uvimbe iwezekanavyo kwa njia salama.

Tiba kwa njia ya eksirei huongeza kiwango cha kuishi na kwa kawaida hufanyika baada ya upasuaji.

Tibakemikali haionekani kuongeza kiwango cha kuishi, lakini, kwa baadhi ya watoto, inaweza kusaidia kupunguza uvimbe kabla ya upasuaji au tiba kwa njia ya eksirei.

Ubashiri wa Ependymomas

Kiwango cha jinsi mtoto anavyofanya vizuri kinategemea umri wa mtoto, aina ya ependymoma, na ni kiasi gani cha uvimbe kinachoweza kuondolewa.

Watoto wanaopona wako katika hatari ya kupata matatizo ya ubongo, uti wa mgongo, na neva kutokana na madhara ya upasuaji na tiba kwa njia ya eksirei.

Taarifa Zaidi

Nyenzo zifuatazo za lugha ya Kiingereza zinaweza kuwa muhimu. Tafadhali kumbuka kuwa Mwongozo hauwajibiki kwa maudhui ya nyenzo hizi.

  1. The American Cancer Society: Ikiwa Mtoto Wako Ametambuliwa kuwa na Saratani: Rasilimali kwa wazazi na wapendwa wa mtoto ambaye ana saratani ambayo hutoa taarifa kuhusu jinsi ya kukabiliana na baadhi ya matatizo na maswali yanayojitokeza mara tu baada ya mtoto kugunduliwa na ugonjwa huo