Tabia za Kulala kwa Watoto Waliozaliwa Karibuni na Watoto Wachanga

NaDeborah M. Consolini, MD, Thomas Jefferson University Hospital
Imekaguliwa naAlicia R. Pekarsky, MD, State University of New York Upstate Medical University, Upstate Golisano Children's Hospital
Imepitiwa/Imerekebishwa Sept 2023 | Imebadilishwa Jul 2025
v813779_sw

Kwa kuwa mfumo wa neva wa watoto wachanga haujakomaa kikamilifu, huwa wanalala mara nyingi lakini kwa vipindi vifupi vya saa moja au mbili tu, iwe mchana au usiku. Kufikia umri wa wiki 4 hadi 6, watoto wengi huanza kuwa na mzunguko wa kuamka kwa saa 4 na kulala kwa saa 4. Kufikia umri wa miezi 4 hadi 6, watoto wachanga kwa kawaida huwa na uwezo wa kuzoea ratiba ya usingizi wa mchana na wa usiku. Wanapofikisha umri wa mwaka 1, watoto wengi hulala mfululizo kwa saa 8 hadi 9 usiku. Hata hivyo, matatizo ya usingizi ni ya kawaida na yanaweza kutokea katika nyakati mbalimbali katika miaka michache ya kwanza ya maisha (tazama Matatizo ya Usingizi kwa Watoto).

Sababu zinazoathiri mifumo ya usingizi hutofautiana kulingana na umri wa mtoto. Katika umri wa miezi 9 na tena karibu miezi 18, matatizo ya usingizi huwa ya kawaida kwa sababu

  • Wasiwasi wa kutengana huanza kujitokeza.

  • Watoto huanza kusonga na kutembea kwa kujitegemea na kuwa na udhibiti zaidi wa mazingira yao.

  • Wanaweza kulala sana jioni.

  • Wanaweza kuchangamka sana wanapocheza kabla ya wakati wa kulala.

  • Ndoto mbaya huanza kutokea mara nyingi zaidi.

Wazazi wanaweza kuwasaidia watoto kulala usiku kwa kuwashughulikia na kupunguza uchangamfu jioni, na kwa kuhakikisha chumba cha mtoto ni chenye giza usiku, jambo muhimu kwa ukuaji wa kawaida wa uwezo wa kuona. Watoto wanapaswa kuhimizwa mapema waweze kulala pekee yao na si mikononi mwa mzazi. Kwa njia hii, wataweza kujituliza wenyewe wanapoamka katikati ya usiku.

Ili kupunguza hatari ya ugonjwa wa kifo cha ghafla cha watoto wachanga (SIDS), watoto wachanga wanapaswa kulala chali kila wakati, si kwa tumbo wala kwa ubavu. Pendekezo hili limechangia kwa kiasi kikubwa kupunguza matukio ya SIDS katika miaka ya hivi karibuni. Pia, watoto wachanga hawapaswi kulala wakiwa na mito laini, vinyago, au blanketi nzito, kwa sababu vinaweza kuzuia kupumua. Kumlaza mtoto akiwa na kidude cha kunyonya (pacifier) kunaweza pia kusaidia kupunguza hatari ya SIDS (watoto wanaonyonyeshwa wanapaswa kuwa na angalau mwezi 1 au wawe tayari wamezoea kunyonya kabla ya kupewa kidude cha kunyonya). (Tazama pia Kinga ya SIDS.)

Kulala-pamoja

Kulala pamoja ni hali ambapo mzazi na mtoto hulala karibu ili kila mmoja aweze kumwona, kumsikia na/au kumgusa mwenzake. Mipango ya kulala pamoja inaweza kujumuisha

  • Kushiriki kitanda (mtoto hulala kitanda kimoja na mzazi)

  • Kushiriki chumba (mtoto hulala kitanda tofauti lakini katika chumba kimoja na mzazi)

Kushiriki kitanda kati ya wazazi na watoto wachanga ni jambo la kawaida lakini lnaweza kuzua mjadala. Mara nyingi wazazi huchagua kushiriki kitanda kwa sababu za kitamaduni au binafsi, kama urahisi wa kulisha, kuimarisha uhusiano, kuamini kuwa uangalizi wao pekee ndio unaoweza kumlinda mtoto, na kuamini kuwa hata wakiwa wamelala bado wanaweza kuendelea kumwangalia mtoto. Hata hivyo, kushiriki kitanda kumehusishwa na kuongezeka kwa hatari ya SIDS, na kunaweza kusababisha majeraha au kifo kwa sababu mtoto anaweza kukosa hewa, kunaswa, au kunyongwa.

Kushiriki chumba bila kushiriki kitanda huruhusu wazazi kuwa karibu na mtoto kwa ajili ya kulisha na uangalizi, ni salama zaidi kuliko kushiriki kitanda au mtoto kulala peke yake chumbani, na kunahusishwa na hatari ndogo ya SIDS. Kwa sababu hizi, madaktari wanapendekeza kushiriki chumba bila kushiriki kitanda kama mpangilio bora wa kulala kwa wazazi na watoto wachanga katika miezi ya kwanza ya maisha.