Fibroadenoma za matiti ni uivimbe mdogo, laini, imara, wa mviringo usio na saratani unaoundwa na tishu za nyuzinyuzi na za tezi.
(Angalia pia Muhtasari wa Matatizo ya Matiti na Uvimbe wa Matiti.)
Fibroadenoma za matiti kwa kawaida huonekana kwa wanawake vijana, wakiwemo wasichana wa balehe. Kisababishaji hakijulikani. Kwa watu wazima, fibroadenomas za matiti zinaweza kupungua kwa ukubwa baada ya muda, lakini kwa wabaleghe, huwa zinaendelea kukua.
Fibroadenoma za matiti zinaweza kudhaniwa kuwa ni saratani ya matiti, lakini si saratani. Baadhi ya fibroadenoma hazionekani kuongeza hatari ya saratani ya matiti. Hata hivyo, fibroadenoma tata (ambazo zina vipengele vingi, kama vile sisti, tishu za kovu, na uvimbe mgumu) zinaweza kuongeza hatari kidogo.
Vivimbe havina maumivu na ni rahisi kusogezeka, na vina kingo zilizoainishwa vizuri ambazo zinaweza kuhisiwa wakati wa kujichunguza matiti. Sifa hizi humwonyesha daktari kwamba uvimbe una uwezekano mdogo wa kuwa za saratani. Hata hivyo, ili kuhakikisha kwamba si saratani, daktari kwa kawaida huondoa sehemu ya uvimbe au uvimbe wote ili kuchunguzwa chini ya darubini (bayopsi). Hutumika dawa ya ganzi ya ndani.
Fibroadenoma za matiti kwa kawaida huondolewa iwapo zitakua au zitasababisha dalili. Kwa sababu fibroadenoma kwa vijana wa balehe hukua, zinapaswa kuondolewa. Hata hivyo, fibroadenoma mara nyingi hujirudia. Ikiwa uvimbe kadhaa umeondolewa na kugundulika kuwa si wa saratani, mwanamke na daktari wake wanaweza kuamua kutoondoa uvimbe mpya unaojitokeza ili kuepuka kuondoa mara kwa mara. Bila kujali kama fibroadenoma zimeondolewa au la, mwanamke anapaswa kufanyiwa uchunguzi wa mara kwa mara ili daktari wake aweze kuchunguza iwapo kuna mabadiliko.