Malaria

Imepitiwa/Imerekebishwa Imebadilishwa Aug 2025
v39738298_sw

Malaria ni nini?

Malaria ni maambukizi ya protozoa wadogo sana waitwao Plasmodium. Protozoa ni aina ya vimelea.

  • Malaria huenezwa na mbu walioambukizwa

  • Kila mwaka mamilioni ya watu duniani kote hupata malaria

  • Watu zaidi ya nusu milioni walikufa kutokana na malaria mwaka 2023, wengi wao wakiwa ni watoto walio na umri wa chini ya miaka 5

  • Malaria kwa kawaida husababisha homa, maumivu ya kichwa na homa ya baridi

  • Inatambuliwa kwa kipimo cha damu na kwa uchunguzi wa sampuli ya damu kwenye hadubini

  • Dawa kadhaa hutibu malaria, lakini vimelea vinakuwa sugu kwa dawa

Malaria hutokea hasa katika sehemu hizi za dunia:

  • Amerika ya Kusini (pamoja na sehemu za kaskazini za Argentina)

  • Amerika ya Kati

  • Afrika

  • India na sehemu zingine za Asia ya Kusini

  • Mashariki ya Kati (pamoja na Uturuki, Siria, Irani, na Iraq)

  • Asia ya Kusini-mashariki

  • Korea Kaskazini na Kusini

  • Meksiko

  • Haiti

  • Jamhuri ya Dominika

  • Asia ya Kati

Je, nini husababisha malaria?

Kuna aina 5 za vimelea vya Plasmodium vinavyosababisha malaria kwa watu.

  • Mbu anapomuuma mtu aliyeambukizwa, anaweza kuambukizwa na vimelea

  • Mtu anayefuata atakayeumwa na mbu huyo anaweza kupata maambukizi

Vimelea vya malaria kwanza huenda kwenye ini ili vikomae na kuzaliana. Kisha vimelea huingia kwenye damu na kuzaliana ndani ya seli nyekundu za damu yako.

  • Mwishowe seli nyeupe za damu hupasuka na kuachia vimelea, ambavyo huambukiza seli nyekundu za damu zaidi

  • Kama seli nyekundu za damu zimeharibiwa nyingi, unaweza kupata hali ya kuwa na idadi ndogo ya seli nyekundu za damu (anemia)

Zipi ni dalili za malaria?

Huenda usiwe na dalili kwa siku kadhaa au hata kwa miaka kadhaa baada ya kuumwa na mbu mwenye maambukizi. Kisha una:

  • Homa kali

  • Mzizimo wa kutetemeka (tetemeka sana)

  • Maumivu ya kichwa, misuli kuuma, na kuumwa sana

  • Uchovu mwingi

Homa na mzizimo huja na kupotea kila baada ya siku kadhaa. Jinsi maambukizi yanavyoendelea, unaweza kupata:

Kama ni mjamzito, unaweza kuugua sana ikiwa una malaria. Malaria inaweza kusababisha mtoto wako kuzaliwa mapema sana (kuzaliwa kabla ya wakati) au inaweza kusababisha mtoto wako kufa mapema katika ujauzito wako (kuharibika mimba) au kufa katikati ya safari ya ujauzito wako (kuzaliwa mfu). Mtoto wako anaweza kuzaliwa na uzito mdogo au anaweza kuzaliwa na maambukizi.

Aina hatari zaidi ya malaria inaitwa malaria ya falciparum. Malaria ya falciparum hasa ni hatari kwa sababu seli nyekundu za damu zilizo ambukizwa zinaweza kuziba mishipa midogo ya damu na kusababisha uharibifu wa viungo. Vizuizi hivyo vinaweza kuharibu ubongo, figo, mapafu, njia ya mmeng'enyo wa chakula na ogani zingine. Aina zingine za malaria huwa hazifanyi hivi.

Malaria ya falciparum pia husababisha dalili nyingine kutegemea na viungo vilivyoambukizwa:

  • Ubongo: Kifafa, kuchanganyikiwa, kupoteza fahamu, kifo

  • Mapafu: Kupumua kwa shida

  • Figo: Mkojo mweusi, figo kushindwa kufanya kazi

  • Njia ya mmeng'enyo wa chakula: Kuharisha

  • Homoni: Kiwango cha chini cha sukari kwenye damu (hipoglisemia)

Je, madaktari wanawezaje kujua ikiwa nina malaria?

Madaktari hufanya:

  • Kipimo cha damu cha haraka

  • Uchunguzi wa sampuli ya damu kwenye hadubini

Kipimo cha haraka huchukua takriban dakika 20. Ili kufanya kipimo hiki, madaktari huchukua sampuli ya damu yako na kemikali fulani na kuziweka kwenye kadi maalum ya kipimo. Mistari maalum huonekana kwenye kadi ikiwa una malaria.

Madaktari pia watachukua sampuli ya damu yako na kuichunguza kwenye hadubini. Wana uwezo wa kuona vimelea katika damu yako kwa kutumia hadubini.

Ikiwezekana, madaktari hufanya vipimo vyote viwili.

Je, madaktari hutibu vipi malaria?

Dawa za malaria hutegemea aina ya vimelea ulivyonavyo na ulikovipata. Katika baadhi ya maeneo ya dunia, vimelea vya malaria ni sugu kwa dawa nyingi za malaria. "Sugu" maana yake vimelea havifi tena au kudhoofishwa na dawa ambazo kwa kawaida zinaweza kuviua au kuvidhoofisha.

Katika baadhi ya maeneo ambako malaria ipo sana, dawa za malaria zinazouzwa katika maduka ya dawa ya mtaani zinaweza kuwa za kughushi. Ikiwa unasafiri kwenda maeneo ya mbali yenye hatari kubwa, daktari wako anaweza kukushauri ubebe dawa za malaria kama tahadhari iwapo utapata maambukizi. 

Ninawezaje kuzuia malaria?

Shirika la Afya Duniani (WHO) linapendekeza matumizi ya chanjo ya malaria kwa watoto wanaoishi katika maeneo ambayo malaria ipo sana na ambako kuenea kwa malaria ya falciparum ni kwa kiwango cha kati hadi cha juu.

Iwapo utatembelea au unaishi katika eneo ambalo lina malaria, unapaswa:

  • Kuepuka ming'ato ya mbu

  • Tumia dawa za kuzuia ili kuua vimelea vya malaria

Ili kuepuka kuumwa na mbu:

  • Puliza dawa ya kuua wadudu ndani ya makazi na majengo ya nje.

  • Weka nyavu kwenye milango na madirisha

  • Lala ndani ya chandarua cha kuzuia mbu chenye kiuwa wadudu cha permethrin

  • Jipake dawa za kufukuza mbu zenye DEET

  • Vaa suruali ndefu and mashati ya mikono mirefu, hasa jioni na alfajiri

  • Ikiwa utakuwa katika mazingira yenye mbu wengi, vaa nguo na utumie vitu (kama vile buti, suruali soksi na hema) ambavyo vimepakwa permethrin.

Watu pia wanaweza kusafisha maji yoyote yaliyotuama (kama vile kwenye matairi chakavu, vyungu vya maua au madimbwi), ambapo mbu hupenda kuzaliana.

Unaweza kutumia dawa ili kuzuia malaria. Dawa nyingi tofauti zinapatikana. Daktari wako anaweza kukushauri ni ipi inafaa kulingana na mahali unaposafiri na kwa hali ya afya yako. Utapaswa kuanza kutumia dawa kabla ya kusafiri.