Actinomycosis ni maambukizi sugu yanayosababishwa hasa na bakteria wa anaerobiki. Actinomyces israelii. Aina hii ya bakteria kwa kawaida huishi kwenye nyufa kati ya meno na fizi, kwenye mafindofindo, na kwenye utando wa ute unaofunika utumbo na uke.
Maambukizi hutokea tu pale tishu zinapoharibika, hali inayowezesha bakteria kuingia kwenye tishu za ndani zaidi.
Majipu hutokea katika maeneo mbalimbali, kama vile utumbo au usoni, na husababisha maumivu, homa, na dalili nyingine.
Dalili huashiria utambuzi wa ugonjwa, na madaktari huthibitisha kwa kutambua bakteria katika sampuli ya tishu iliyoambukizwa.
Majipu hupasuliwa na kutolewa usaha, na dawa za viuavijasumu hutolewa.
Kwa utambuzi wa mapema na matibabu sahihi, watu wengi hupona kabisa.
Bakteria wa actinomyces hawahitaji oksijeni ili kuishi. Yaani, bakteria hawa ni anaerobi.
Bakteria wa actinomyces husababisha maambukizi tu pale uso wa tishu wanazoishi unapovunjika au kuharibika, na kuwawezesha kuingia kwenye tishu nyingine za ndani zaidi ambazo hazina kinga dhidi yao. Kadiri maambukizi yanavyoenea, tishu za kovu na njia zisizo za kawaida zinazoitwa fistula (au njia) huundwa. Baada ya miezi hadi miaka, fistula hatimaye zinaweza kufika kwenye ngozi na kuruhusu usaha kutoka. Mifuko ya usaha (majipu) inaweza kutokea kifuani, tumboni, usoni, au shingoni.
Wanaume huathirika mara nyingi zaidi, lakini actinomycosis wakati mwingine hutokea kwa wanawake wanaotumia kifaa cha uzazi wa mpango cha ndani ya uterasi (IUD).
Dalili za Aktinomikosisi
Actinomycosis ina aina nyingi. Zote husababisha majipu, tishu za kovu, na fistula.
Aktinomikosisi ya tumbo
Bakteria wa actinomycosis huambukiza utumbo, kwa kawaida eneo lililo karibu na kidole tumbo (apendiksi), na utando wa ndani wa tundu la tumbo (peritoneamu).
Maumivu sugu ya tumbo, homa, kutapika, kuhara au kukosa choo, na kupungua uzito kwa kiasi kikubwa ni dalili za kawaida.
Fistula inaweza kutokea kutoka ndani ya tumbo hadi kwenye ngozi iliyo juu yake, na pia kati ya utumbo na viungo vingine.
Aktinomikosisi ya tumbo la uzazi
Bakteria husambaa hadi kwenye uterasi, kwa kawaida kutoka kwenye kifaa cha uzazi wa mpango cha ndani ya uterasi (IUD) ambacho kimekuwapo kwa miaka mingi.
Majipu na tishu za kovu zinaweza kutokea kwenye mirija ya falopia, na viungo vilivyo karibu kama vile kibofu cha mkojo na mirija ya mkojo (ureta). Fistula inaweza kutokea kati ya viungo hivi.
Dalili ni pamoja na maumivu sugu ya tumbo au fupa nyonga, homa, kupungua uzito, na kutokwa damu pamoja na majimaji/uchafu kutoka ukeni.
Aktinomikosisi ya shingo na uso
Kwa kawaida, uvimbe mdogo, mgumu, na wakati mwingine wenye maumivu hutokea mdomoni na usoni, shingoni, au kwenye ngozi iliyo chini ya taya (hali inayojulikana kama taya lenye uvimbe). Uvimbe huu unaweza kulainika na kutoa usaha wenye chembechembe ndogo, za mviringo, zenye rangi ya manjano.
Maambukizi yanaweza kuenea hadi kwenye shavu, ulimi, koo, tezi za mate, fuvu la kichwa, mifupa ya shingo (pingili za shingo), mifupa ya uso, ubongo, au nafasi iliyo ndani ya tishu zinazoufunika ubongo (utando wa uti wa mgongo na ubongo).
Aktinomikosisi ya kifua
Aina hii huathiri kifua (kidari). Watu hupata maumivu sugu ya kifua na homa. Hupunguza uzito na kukohoa, wakati mwingine wakitoa makohozi. Huenda watu huambukizwa wanapovuta hadi kwenye mapafu majimaji yenye bakteria.
Majipu yanaweza kutokea kwenye mapafu na hatimaye kuenea hadi kwenye utando kati ya mapafu na ukuta wa kifua (pleura). Huko, majipu husababisha muwasho (pleuraitisi), na majimaji yaliyoambukizwa hujilimbikiza (hali inayoitwa empyema). Fistula inaweza kutokea, na kuwezesha maambukizi kuenea hadi kwenye mbavu, ngozi ya kifua, na uti wa mgongo.
Maambukizi yanaweza kuenea kwa kiasi kikubwa kabla hayajasababisha dalili zozote. Dalili ni pamoja na maumivu ya kifua, homa, na kikohozi chenye makohozi.
Aktinomikosisi ya jumla
Mara chache, bakteria husafirishwa kupitia damu na kuambukiza viungo vingine, kama vile ubongo, uti wa mgongo, mapafu, ini, figo, na vali za moyo. Kwa wanawake, viungo vya uzazi vinaweza kuambukizwa.
Dalili hutofautiana kulingana na viungo vilivyoathiriwa. Kwa mfano, watu wanaweza kuwa na maumivu ya kichwa, maumivu ya mgongo, au maumivu ya tumbo.
Utambuzi wa Aktinomikosisi
Uchunguzi na ukuzaji wa bakteria kwa ajili ya uchunguzi wa sampuli ya makohozi, usaha, au tishu
Wakati mwingine vipimo vya picha
Madaktari hushuku actinomycosis kwa watu walio na majipu, tishu za kovu, na fistula zinazoashiria ugonjwa wa actinomycosis.
Madaktari huchukua sampuli za makohozi, usaha, au tishu ili kuchunguza uwepo wa aina mbalimbali za bakteria wa Actinomycosis, kama vile Actinomyces israelii. Mara nyingi, sindano huingizwa kupitia ngozi ili kuchukua sampuli kutoka kwenye jipu au tishu iliyoambukizwa. Wakati mwingine, tomografia ya kompyuta (CT) au uchunguzi wa picha ya mawimbi ya sauti hutumiwa kuwasaidia madaktari kuelekeza sindano kwenye eneo lililoambukizwa. Wakati mwingine upasuaji huhitajika ili kutoa sampuli. Sampuli huchunguzwa kwa darubini na kutumwa maabara, ambako bakteria, ikiwa wapo, wanaweza kukuzwa (kuoteshwa).
Utambuzi wa bakteria katika sampuli ya makohozi, usaha, au tishu unathibitisha utambuzi.
Wakati mwingine vipimo vya picha (eksirei au CT) hufanywa ili kubaini idadi, ukubwa, na mahali halisi pa majipu.
Matibabu ya Aktinomikosisi
Kutoa usaha kwenye majipu
Dawa za kuua bakteria
Matibabu ya actinomycosis yanajumuisha
Kutoa usaha kwenye majipu kwa kutumia sindano (ambayo kwa kawaida huingizwa kupitia ngozi) au kwa upasuaji.
Kutoa dozi kubwa za dawa za viuavijasumu
Viuavijasumu kama penicillin au tetracycline lazima vitumike kwa angalau miezi 2 na wakati mwingine huhitajika kwa zaidi ya miezi 12.
CT au upigaji picha wa mwangwi wa sumaku (MRI) unaweza kutumika kubaini kama majipu yanapungua au kupona. Upasuaji unaweza kuhitajika, hasa ikiwa maambukizi yanaathiri maeneo muhimu kama vile uti wa mgongo.
Wanawake walio na actinomycosis ya fupa nyonga huondolewa kifaa chao cha uzazi wa mpango cha ndani ya uterasi (IUD) na hupewa penicillin. Maambukizi makubwa ya fupa nyonga yanaweza kuhitaji utoaji wa usaha wa ziada kutoka kwenye majipu. Wakati mwingine uterasi, mirija ya falopia na ovari huhitaji kuondolewa.
Ubashiri wa Aktinomikosisi
Ikiwa actinomycosis itatambuliwa mapema na kutibiwa ipasavyo, watu wengi hupona kabisa.
Ubashiri wa ugonjwa hutegemea aina ya actinomycosis aliyonayo mtu na ni sehemu zipi za mwili zilizoathirika. Ubashiri wa ugonjwa ni bora zaidi kwenye aina ya shingo na uso na ni mbaya zaidi kwa aina za kifua, tumbo, na aina za jumla, hasa ikiwa ubongo na uti wa mgongo vimeathirika.