Kubalehe Mapema

(Ubalehe wa Mapema)

NaAndrew Calabria, MD, The Children's Hospital of Philadelphia
Imekaguliwa naMichael SD Agus, MD, Harvard Medical School
Imepitiwa/Imerekebishwa Imebadilishwa Apr 2024
v1562542_sw

Kubalehe mapema (ubalehe wa mapema) ni kukomaa kwa viungo vya uzazi ambako huanza kabla ya umri wastani.

  • Kisababishaji cha kubalehe mapema mara nyingi hakijulikani, lakini kinaweza kusababishwa na kasoro za kimuundo au uvimbe kwenye ubongo.

  • Dalili ni pamoja na ukuaji wa mapema wa haraka na ukuaji wa mapema wa nywele za sehemu za siri na kwapani.

  • Utambuzi huo unategemea vipimo vya eksirei, vipimo vya damu, na vipimo vya upigaji picha.

  • Matibabu hutegemea aina ya ubalehe wa mapema lakini yanaweza kujumuisha matibabu ya homoni.

Ubalehe wa Kawaida

Kubalehe ni mfuatano wa matukio ambapo mabadiliko ya mwili hutokea, na kusababisha sifa za kimwili za mtu mzima na uwezo wa kuzalisha upya. Kwa kawaida, mabadiliko haya hutokea kwa mfululizo wakati wa kubalehe, hivyo kusababisha ukomavu wa kijinsia.

Mwanzo wa kubalehe hutokea wakati hipothalamus i(eneo la ubongo linalodhibiti tezi ya pituitari) huanza kutoa ishara za kemikali zinazoitwa homoni inayotoa gonadotropini. Tezi ya pituitari huitikia ishara hii kwa kutoa homoni zinazoitwa gonadotropini (homoni ya luteini na homoni ya kuchochea foliko), ambazo huchochea ukuaji wa tezi za viungo vya sehemu ya siri—pumbu (korodani) kwa wavulana na ovari kwa wasichana. Tezi hizi za viungo vya sehemu ya siri hutoa homoni za jinsia, kama vile testosteroni au estrojeni, zinazosababisha kubalehe.

Kwa wavulana, Ishara za kwanza za kubalehe ni kuongezeka kwa pumbu na kifuko cha pumbu, ikifuatiwa na kurefuka kwa uume. Nywele za sehemu za siri na za chini ya kwapa (nywele za kwapani) hutokea baadaye. Kwa wavulana, kubalehe kwa kawaida huanza kati ya umri wa miaka 9 na 14 (angalia Ubalehe kwa Wavulana).

Kwa wasichana, mabadiliko ya kwanza ya kubalehe kwa kawaida huwa mwanzo wa ukuaji wa matiti (kuchipua matiti). Muda mfupi baadaye, nywele za sehemu za siri na kwapani zinaanza kukua. Kwa wasichana, kubalehe kwa kawaida huanza kati ya umri wa miaka 8 na 13 (angalia Ubalehe kwa Wasichana).

Hatua katika Ukuaji wa Viungo vya Uzazi kwa Wasichana na Wavulana

Wakati wa kubaleghe, ukuaji wa kijinsia hutokea kwa utaratibu fulani. Hata hivyo, mabadiliko hutokea na kuendelea kwa wakati tofauti kwa kila mtu.

Kwa wasichana, kubaleghe huanza karibu na umri wa miaka 8 hadi 13 na hudumu kama miaka 4.

Kwa wavulana, kubalehe huanzia takribani umri wa miaka 10 hadi 14 na hudumu kama miaka 4 hadi 6.

Chati hii inaonyesha utaratibu wa kawaida na kipindi cha kawaida cha ukuaji wa kijinsia.

Katika jinsia zote mbili, karibia wakati wa kubalehe, tezi ya adrenali pia huanza kutoa homoni zinazosababisha kuonekana kwa nywele za sehemu za siri na kwapa. Homoni hizi za adrenali hudhibitiwa na ishara tofauti za kemikali kuliko homoni zingine za kubalehe.

Nchini Marekani, kubalehe kunaonekana kutokea mapema kuliko hapo awali, hasa kwa wasichana. Zaidi ya hayo, ukuaji wa matiti unazidi kutokea katika umri mdogo, mwenendo unaoakisi janga la ugonjwa wa unene kupita kiasi, kwa sababu uwiano wa juu wa uzani na kimo cha mwili (BMI) kinahusishwa na ukuaji wa matiti mapema zaidi. Kwa wasichana, muda wa kubalehe huathiriwa pia na rangi na kabila. Kubalehe huanza mapema kwa wasichana Weusi na Wahispania ikilinganishwa na wasichana Weupe.

Ubalehe wa Mapema

Katika ubalehe wa mapema, mwili wa mtoto huanza kubadilika na kuwa mwili wa mtu mzima mapema kuliko ilivyotarajiwa. Ufafanuzi wa ubalehe wa mapema kwa kawaida umekuwa kabla ya umri wa miaka 8 kwa wasichana au umri wa miaka 9 kwa wavulana.

Kuna aina 3 za ubalehe wa mapema:

  • Ubalehe wa mapema wa kati

  • Ubalehe wa mapema wa pembezoni

  • Ubalehe usio kamili

Vyanzo na dalili hutofautiana kati ya aina hizo 3.

Ubalehe wa mapema wa kati

Aina hii ya ubalehe wa mapema ni ya kawaida zaidi kwa ujumla na hutokea mara 5 hadi 10 zaidi kwa wasichana.

Ubalehe wa aina hii husababishwa na kutolewa mapema kwa homoni fulani za jinsia (gonadotropini) kutoka kwenye tezi ya pituitari. Homoni hizi husababisha ovari au pumbu (tezi za viungo vya sehemu ya siri) ili kukomaa na kukuwa kubwa. Mara tu tezi za viungo vya sehemu ya siri zinapokomaa, huanza kutoa homoni zingine za jinsia, kama vile estrojeni au testosteroni, ambayo husababisha kubalehe. Mabadiliko ya kimwili kwa kawaida huwa yale ya ubalehe wa kawaida kwa mtoto wa jinsia hiyo, isipokuwa yanapoanza katika umri mdogo.

Wavulana huonyesha ongezekaji wa ukubwa wa pumbu, kurefuka kwa uume, na ukuaji wa nywele za uso, kwapa, na sehemu za siri, na huonekana kama wanaume.

Wasichana hukua matiti na nywele za sehemu za siri na nywele za makwapa na wanaweza kuanza kupata hedhi.

Katika jinsia zote, kuna ukuaji wa haraka unaosababisha ongezeko la kimo kwa kasi sana. Hata hivyo, tofauti na katika ubalehe wa kawaida, ongezeko la kasi la kimo katika ubalehe wa mapema huisha mapema hivyo watoto huwa wafupi wanapokuwa watu wazima kuliko inavyotarajiwa.

Kwa wasichana wengi, madaktari kwa kawaida hawapati sababu ya kutolewa kwa homoni mapema, lakini wakati mwingine husababishwa na uvimbe au kasoro nyingine katika ubongo, kwa kawaida katika tezi ya pituitari au hipothalamasi (eneo la ubongo linalodhibiti tezi ya pituitari). Hata hivyo, kasoro katika ubongo ina uwezekano mkubwa wa kupatikana kwa wavulana.

Neurofibromatosis (ugonjwa ambapo ukuaji mwingi wa tishu za neva hukua chini ya ngozi na katika sehemu zingine za mwili) na magonjwa mengine ya nadra pia yamehusishwa na ubalehe wa mapema.

Wakati mwingine ubalehe wa mapema unaochochewa na mfumo wa ubongo husababishwa na matumizi ya matibabu ya matatizo fulani (kama vile upasuaji, mionzi, au matibabu ya kemotherapi ya kutibu saratani).

Watoto ambao wana wanafamilia waliobalehe mapema wako katika hatari kubwa ya kupata ugonjwa huo.

Ubalehe wa mapema wa pembezoni

Aina hii ya kubalehe mapema inatokea kwa nadra. Katika ubalehe wa mapema unaosababishwa na vyanzo vilivyo nje ya mfumo wa ubongo, kutolewa kwa estrojeni au testosteroni (na testosteroni kama homoni zinazoitwa adrojeni) hakuchochewi na gonadotropini kutoka tezi ya pituitari. Badala yake, viwango vya juu vya adrojeni au estrojeni huzalishwa na uvimbe au kasoro nyingine katika tezi ya adrenali au katika korodani au ovari ambayo haijakomaa. Homoni hizi hazisababishi pumbu au ovari zenyewe kukomaa bali husababisha ukuaji wa sifa zingine za jinsia.

Kwa sababu wavulana na wasichana waliobalehe mapema wanaweza kuzalisha estrojeni au androjeni, mabadiliko ya mwili ya kubalehe hutegemea homoni inayozalishwa badala ya jinsia ya mtoto. Hivyo, uvimbe na mambo yasiyo ya kawaida yanayozalisha estrojeni husababisha ukuaji wa tishu za matiti kwa wavulana na wasichana, ilhali zile zinazozalisha androjeni husababisha ukuaji wa nywele za sehemu za siri na kwapa, harufu mbaya ya mwili wa mtu mzima, na chunusi kwa wavulana na wasichana na, kwa wavulana, kupanuka kwa uume (lakini si pumbu).

Ubalehe usio kamili

Baadhi ya watoto huonyesha dalili chache tu za kubalehe mapema. Kwa kawaida huwa na ukuaji wa matiti kabla ya wakati (thelarche) au ukuaji wa nywele za sehemu za siri kabla ya wakati (adrenarche) bila mabadiliko yoyote mengine ya kubalehe kama vile ukuaji wa pumbu au ovari, hedhi, au ukuaji wa haraka. Baadhi ya wasichana huanza kukua matiti katika miaka 2 ya kwanza ya maisha, lakini hawana viwango vilivyoongezeka vya homoni. Watoto walio na ukuaji wa nywele za sehemu za siri mapema (kwa kawaida kati ya umri wa miaka 6 na 8) mara nyingi huwa na harufu ya mwili na chunusi kama ya watu wazima. Mabadiliko yanaendelea kutokea polepole.

Mabadiliko haya ya awali ya mwili hayasababishwi na ugonjwa, na ni watoto wachache tu wanaoendelea kubalehe mapema. Ukuaji wa nywele za sehemu za siri wa mapema hutokea kwa sababu tezi ya adrenali huongeza kiwango cha androjeni inayozalisha. Hata hivyo, viwango vya gonadotropini na estrojeni haviongezeki kadri nywele za sehemu za siri zinavyokua mapema.

Utambuzi wa Ubalehe wa Mapema

  • Vipimo vya eksirei ya mkono na kifundo cha mkono

  • Vipimo vya damu

  • Uwezekano wa kupiga picha viungo fulani

Wakati wowote mtoto anapopata dalili za kubalehe mapema, kukua kwa haraka, au kubalehe kusiko kwa kawaida, madaktari hupiga eksirei ya mkono na kifundo cha mkono ili kukadiri ukomavu wa mfupa (unaoitwa kipimo cha eksirei cha kubaini umri wa mfupa).

Ikiwa kipimo cha eksirei cha kubaini umri wa mfupa kinaonyesha kwamba mifupa ya mtoto ina mwonekano wa kukomaa zaidi kuliko inavyopaswa kwa mtoto wa kawaida wa umri huo, utathmini kamili zaidi kwa kawaida unaonyeshwa.

Vipimo vya damu hufanywa ili kubaini viwango vya homoni.

Ikiwa viwango vya homoni viko juu, madaktari wanaweza kufanya kipimo cha ultrasonografia ya fupanyonga na tezi za adrenali ili kuangalia kama kuna uvimbe wa ovari au adrenali. Madaktari pia wanaweza kufanya kipimo cha upigaji picha wa mwangwi wa sumaku (MRI) cha ubongo ili kuangalia kama kuna mambo yasiyo ya kawaida ya kimuundo au uvimbe wa hipothalamasi au tezi ya pituitari.

Madaktari wanaweza kufanya upimaji wa jeni kwa watoto ambao wana wanafamilia ambao wamebalehe mapema.

Matibabu ya Ubalehe wa Mapema

  • Matibabu ya kisababishi

  • Matibabu ya homoni ya sintetiki

Matibabu ya kubalehe mapema kwa kawaida hayahitajiki kwa watoto ambao wana ukuaji wa nywele za sehemu za siri na kwapa pekee kabla ya wakati, lakini uchunguzi wa mara kwa mara unahitajika ili kuangalia kama kuna maendeleo ya baadaye ya kubalehe mapema. Watoto ambao ukuaji wa matiti yao ulianza kabla ya umri wa miaka 2 hutathminiwa ikiwa ukuaji wa matiti unaendelea baada ya umri wa miaka 2.

Kutibu kisababishaji kinachotambulika cha kubalehe mapema, kama vile kuondoa uvimbe au sisti, kunaweza kuzuia kuendelea kwa kubalehe.

Wakati hakuna kisababishaji kinachoweza kutibika kinachotambuliwa katika ubalehe wa mapema, dawa zinaweza kupunguza kasi ya ubalehe. Uamuzi wa kutoa dawa unategemea mambo mengi, ikiwa ni pamoja na umri wa mtoto, jinsi ubalehe unavyoendelea kwa kasi, jinsi mtoto anavyokua kwa kasi, na kimo ambacho madaktari wanafikiri mtoto atakuwa nacho. Malengo ya matibabu ya dawa ni kumruhusu mtoto kukua hadi kimo cha kawaida cha mtu mzima na kupunguza wasiwasi wowote ambao mtoto anahisi kutokana na yeye kukua mapema kuliko wanarika.

Chaguo za matibabu ni pamoja na udungaji wa sindano za homoni za sintetiki zinazozuia uzalishaji wa homoni za jinsia. Sindano hutolewa kila mwezi, kila baada ya miezi 3, au baada ya kila miezi 6. Homoni hizo zinaweza pia kutolewa kwa kutumia kipandikizi kinachoingizwa chini ya ngozi baada ya kila miezi 12.

Ubalehe wa pembeni kabla ya wakati unaweza kusimamishwa kwa dawa zinazozuia utendaji wa homoni za jinsia.