Medulloblastoma ni uvimbe wa ubongo unaokua kwa kasi unaokua katika serebelamu (sehemu ya ubongo inayosaidia kudhibiti uratibu na usawa). Medulloblastoma zote ni saratani (zinadhuru).
Chanzo cha medulloblastoma hakijulikani.
Watoto wanaweza kutapika mara kwa mara, kuwa na matatizo ya kupata usawa, maumivu ya kichwa, kichefuchefu, uchovu, au kuona picha mbili za kitu kimoja.
Utambuzi kwa kawaida huhusisha kipimo cha picha, uchunguzi wa sampuli ya tishu na seli na kutoa maji ya uti wa mgongo.
Matibabu ni upasuaji, tibakemikali na tiba kwa njia ya eksirei.
Ubashiri wa ugonjwa hutegemea kama saratani ina hatari ya wastani au hatari kubwa.
(Angalia pia Muhtasari wa Uvimbe wa Ubongo na Uti wa Mgongo kwa Watoto.)
Medulloblastoma ni mojawapo ya uvimbe unaodhuru zaidi wa ubongo unaoenea zaidi kwa watoto. Uvimbe huu hutokea sana kwa watoto wenye umri wa miaka 3 hadi 4 au miaka 8 hadi 10, lakini unaweza kutokea kwa watoto wachanga na katika ujana wao wote.
Medulloblastoma hukua katika sehemu ya ubongo inayodhibiti uratibu na usawa (serebelamu), ambayo iko nyuma ya ubongo chini ya ubongombele.
Medulloblastoma huenea hadi sehemu nyingine za ubongo na kwenye uti wa mgongo. Katika hali nadra, huenea hadi sehemu nyingine za mwili.
Kinachosababisha medulloblastoma hakijulikani wazi. Wakati mwingine hutokea kwa watu wenye matatizo fulani ya kurithi (kama vile ugonjwa wa Gorlin au ugonjwa wa Turcot).
Dalili za Medulloblastomas
Dalili za medulloblastoma kwa kawaida huhusiana na shinikizo lililoongezeka ndani ya fuvu la kichwa (shinikizo la ndani ya fuvu) na kutofanya kazi vizuri kwa serebelamu.
Dalili zinaweza kujumuisha kutapika, kukosa mwelekeo, kutembea kwa kuyumbayumba, au matatizo ya kudumisha usawa. Watoto pia wanaweza kuwa na maumivu ya kichwa, kichefuchefu, uchovu, na kuona picha mbili za kitu kimoja.
Utambuzi wa Medulloblastomas
Upigaji picha kwa mwangwi wa sumaku (MRI)
Uchunguzi wa sampuli ya tishu na seli au upasuaji mara nyingi ili kuondoa uvimbe mzima
Kinga majimaji ya uti wa mgongo
Ili kufanya utambuzi wa medulloblastoma, madaktari hufanya MRI wakitumia kiambato cha utofautishaji (viini vinavyofanya miundo iwe wazi zaidi kuonekana kwenye vipimo vya picha) ili kutafuta uvimbe. Kisha, wanachukua sampuli ya tishu kutoka kwenye uvimbe na kuichunguza chini ya hadubini (uchunguzi wa tishu). Wanaweza pia kufanya vipimo maalum vya kijenetiki kwenye sampuli ili kusaidia katika utambuzi na matibabu. Kwa kawaida, badala ya kuondoa sehemu tu ya uvimbe ili kupata sampuli, uvimbe wote huondolewa kupitia upasuaji na kupelekwa kwa uchunguzi.
Ili kubaini iwapo uvimbe umeenea, madaktari hufanya MRI ya uti wa mgongo na kutoa maji ya uti wa mgongo (kutobolewa kwa kiuno—angalia mchoro ). Uondoaji wa maji ya uti wa mgongo hufanywa ili kupata maji ya ubongo na uti wa mgongo kwa uchunguzi chini ya hadubini ili kutafuta seli za saratani.
Baada ya upasuaji kufanywa, madaktari hufanya MRI nyingine ili kuona kama uvimbe umeondolewa kabisa. Matokeo ya vipimo hivi huwasaidia madaktari kubaini kama uvimbe una hatari ya wastani au hatari kubwa.
Hatari huwa wastani ikiwa
Uvimbe wote au karibu wote unaweza kuondolewa wakati wa upasuaji.
Uvimbe haujaenea hadi sehemu nyingine za ubongo, maji ya uti wa mgongo, au kwingineko mwilini.
Hatari huwa kubwa ikiwa
Kiasi kikubwa cha uvimbe hakiwezi kuondolewa wakati wa upasuaji.
Uvimbe umeenea hadi sehemu nyingine za ubongo, uti wa mgongo, au kwingineko mwilini.
Katika miaka ya hivi majuzi, matokeo ya upimaji wa jeni wa uvimbe wenyewe yameonyeshwa kuwa na athari kwenye matokeo na hatari.
Matibabu ya Medulloblastomas
Upasuaji, tiba kwa njia ya eksirei na tibakemikali
(Angalia pia Kanuni za Matibabu ya Saratani.)
Medulloblastoma hutibiwa vyema kwa kuondoa uvimbe kupitia upasuaji na kutumia tibakemikali na tiba kwa njia ya eksirei. Baadhi ya watoto walio chini ya umri wa miaka 3 wanaweza kutibiwa kwa ufanisi kupitia upasuaji na tibakemikali pekee.
Baadhi ya watoto wanaweza kusaidiwa na uhamishaji wa seli shina unaotumia seli zao wenyewe (unaoitwa uhamishaji wa seli shina kwa kutumia seli za mtu binafsi).
Ubashiri wa Medulloblastomas
Jinsi watoto wanavyoendelea vizuri baada ya matibabu kwa ujumla hutegemea kama wameainishwa kama wenye uvimbe wenye hatari ya wastani au hatari kubwa.
Kwa watoto walio na umri wa zaidi ya miaka 3, uwezekano wa kuishi bila saratani kwa miaka 5 ni takriban 80% ikiwa uvimbe una hatari ya wastani na takriban 60 hadi 70% ikiwa una hatari kubwa.
Kwa watoto wa umri wa miaka 3 na chini, matokeo ni magumu kutabiri, lakini uwezekano wa kuishi kwa ujumla ni duni. Katika takriban 40% ya watoto hawa, uvimbe huwa umeenea wakati wa utambuzi. Aidha, tiba kwa njia ya eksirei kwa kawaida hucheleweshwa au haifanywi katika kundi hili la umri ili kuepuka madhara yanayoathiri ubongo unaokua. Watoto wanaonusurika wako katika hatari ya kupata matatizo makubwa ya kiakili ya kudumu. Kwa mfano, ukuaji wa kiakili una uwezekano mkubwa wa kuathiriwa, na wanaweza kuwa na ugumu wa kujifunza, kukumbuka, na kufanya maamuzi.
Aina fulani za medulloblastoma zina ubashiri mzuri sana, huku uwezekano wa kuishi kwa jumla ukifikia 90 hadi 100%.
Taarifa Zaidi
Nyenzo zifuatazo za lugha ya Kiingereza zinaweza kuwa muhimu. Tafadhali kumbuka kuwa Mwongozo hauwajibiki kwa maudhui ya nyenzo hizi.
The American Cancer Society: Ikiwa Mtoto Wako Ametambuliwa kuwa na Saratani: Rasilimali kwa wazazi na wapendwa wa mtoto ambaye ana saratani ambayo hutoa taarifa kuhusu jinsi ya kukabiliana na baadhi ya matatizo na maswali yanayojitokeza mara tu baada ya mtoto kugunduliwa na ugonjwa huo