Astrocytoma ni uvimbe katika mfumo mkuu wa neva (mfumo mkuu wa neva unajumuisha ubongo na uti wa mgongo). Astrocytoma hutokana na seli zenye umbo la nyota (astrosaiti) ambazo husaidia seli za neva katika ubongo au uti wa mgongo kufanya kazi. Uvimbe huu unaweza kuwa saratani (unaodhuru) au usiwe saratani (usiodhuru).
Chanzo cha astrocytoma hakijulikani.
Watoto wanaweza kuwa na ugumu wa kutembea, udhaifu, mabadiliko ya uwezo wa kuona, kutapika, na maumivu ya kichwa.
Kwa kawaida utambuzi huhusisha kipimo cha picha na bayopsi.
Chaguo za matibabu ni pamoja na upasuaji, tibakemikali na tiba kwa njia ya eksirei.
Astrocytoma ndio uvimbe wa kawaida zaidi wa ubongo na uti wa mgongo kwa watoto, na kuchangia takriban 40% ya visa. Uvimbe huu kwa kawaida hutambuliwa kati ya umri wa miaka 5 na 9. Uvimbe huu unaweza kutokea popote kwenye ubongo au uti wa mgongo lakini hutokea zaidi kwenye serebelamu (eneo karibu na sehemu ya chini ya ubongo linaloratibu mwendo wa mwili).
Astrocytoma ni aina ya uvimbe wa ubongo unaoitwa glioma.
Dalili za Astrocytomas
Shinikizo ndani ya fuvu la kichwa huongezeka, na kusababisha maumivu ya kichwa (mara nyingi watoto wanapoamka kwa mara ya kwanza), kutapika, na utepetevu. Watoto wanaweza kupoteza uratibu wao na kupata shida kutembea. Uwezo wa kuona unaweza kuwa na ukungu au kupotea, na macho yanaweza kuvimba. Mtoto anaweza kuwa na nistagmasi, ambapo macho hukukutua bila hiari kuelekea upande mmoja, kisha kurudi nyuma.
Astrocytoma kwenye uti wa mgongo zinaweza kusababisha maumivu ya mgongo, ugumu wa kutembea, kuwa mwenye ganzi, mabadiliko katika kwenda haja kubwa au ndogo na udhaifu wa misuli.
Utambuzi wa Astrocytomas
Upigaji picha kwa mvumo wa sumaku
Biopsi
Picha ya mvumo wa sumaku (MRI) kwa kawaida hupigwa. Kabla ya MRI kupigwa, kiambato cha utofautishaji hudungwa kwenye mshipa (kupitia mishipa). Viambato vya utofautishaji ni viini vinavyofanya viungo na miundo mingine iwe wazi zaidi kuonekana kwenye vipimo vya picha. Ikiwa MRI haipatikani, tomografia ya kompyuta (CT) hutumika, lakini haitoi maelezo mengi.
Kisha madaktari kwa kawaida huchukua sampuli ya tishu kutoka kwenye uvimbe na kuichunguza chini ya hadubini (uchunguzi wa sampuli ya tishu) kwa sababu matibabu hutegemea jinsi seli za uvimbe zinavyoonekana kutokuwa kawaida (daraja la seli za uvimbe). Astrosaitoma kwa kawaida huainishwa kama daraja la chini (kwa mfano, pilocytic astrocytoma) au daraja la juu (kwa mfano, anaplastic astrocytoma). Uvimbe wa daraja la 1 na la 2 ni wa daraja la chini, na uvimbe wa daraja la 3 na la 4 ni wa daraja la juu.
Matibabu ya Astrocytomas
Upasuaji (ikiwezekana)
Tiba kwa njia ya eksirei, tibakemikali au zote mbili
(Angalia pia Kanuni za Matibabu ya Saratani.)
Astrocytoma nyingi za daraja la chinihuondolewa kwa upasuaji. Ikiwa astrocytoma itaondolewa kabisa, watoto huenda wasihitaji matibabu mengine yoyote.
Wakati mwingine, upasuaji hauwezekani. Tibakemikali hutumika kwa watoto ambao wana uvimbe usioweza kuondolewa kwa upasuaji au unaoendelea au kurudi baada ya upasuaji.
Tiba kwa njia ya eksirei haitumiki sana kutibu watoto wenye astrocytoma za daraja la chini kwa sababu inaweza kuathiri ukuaji na maendeleo ya ubongo.
Astrocytoma nyingi za daraja la chini zinaweza kutibiwa kwa mafanikio, na watoto wanaweza kuishi maisha marefu.
Astrocytoma za daraja la juu hutibiwa kwa mchanganyiko wa upasuaji (ikiwezekana), tiba kwa njia ya eksirei, na tibakemikali (angalia Tiba Mchanganyiko ya Saratani).
Matarajio huwa mabaya zaidi kwa watoto wenye uvimbe wa daraja la juu, na kiwango cha jumla cha kupona ni 20 hadi 30% tu miaka 3 baada ya matibabu.
Taarifa Zaidi
Nyenzo zifuatazo za lugha ya Kiingereza zinaweza kuwa muhimu. Tafadhali kumbuka kuwa Mwongozo hauwajibiki kwa maudhui ya nyenzo hizi.
The American Cancer Society: Ikiwa Mtoto Wako Ametambuliwa kuwa na Saratani: Rasilimali kwa wazazi na wapendwa wa mtoto ambaye ana saratani ambayo hutoa taarifa kuhusu jinsi ya kukabiliana na baadhi ya matatizo na maswali yanayojitokeza mara tu baada ya mtoto kugunduliwa na ugonjwa huo