Kupasuka kwa Uterasi

NaJulie S. Moldenhauer, MD, Children's Hospital of Philadelphia
Imekaguliwa naSusan L. Hendrix, DO, Michigan State University College of Osteopathic Medicine
Imepitiwa/Imerekebishwa Jan 2024 | Imebadilishwa Mar 2024
v8578511_sw

Kupasuka kwa uterasi ni mchaniko wa uterasi mwishoni mwa kipindi cha ujauzito au wakati wa uchungu wa uzazi, ambao kwa kawaida hutokea kwa wanawake waliowahi kufanyiwa upasuaji wa awali wa uterasi (kama vile upasuaji wa kumtoa mtoto). Kupasuka kwa uterasi kunaweza kusababisha kijusi kuelea ndani ya fumbatio.

Kupasuka kwa uterasi ni jambo nadra sana. Ni hali ya dharura inayohitaji matibabu ya haraka.

Uterasi inaweza kupasuka kabla au wakati wa uchungu wa uzazi.

Yafuatayo huongeza hatari ya uterasi kupasuka:

  • Wanawake waliowahi kujifungua kwa njia ya upasuaji, hasa ikiwa uchungu wa uzazi utachochewa kwa dawa badala ya kuanza wenyewe.

  • Wanawake waliowahi kufanyiwa upasuaji mwingine wowote kwenye uterasi.

  • Uterasi imetanuka kupita kiasi (kwa mfano, kutokana na kuwa na kiowevu cha uterasi kingi sana au kuwa na vijusi kadhaa).

  • Kijusi kiko katika mkao usio sahihi wa kuzaliwa na kinalazimika kugeuzwa.

Kupasuka huko husababisha maumivu makali na endelevu kwenye fumbatio la mwanamke mjamzito na mapigo ya moyo ya kijusi kuwa ya taratibu sana.

Ili kuthibitisha utambuzi wa uterasi iliyopasuka, madaktari wanaweza kukata fumbatio kidogo ili waweze kuiona uterasi moja kwa moja. Utaratibu huu unaitwa laparotomi.

Ni lazima kijusi kitolewe papo hapo kwa upasuaji. Kisha uterasi hurekebishwa kwa upasuaji. Wakati mwingine kuiondoa uterasi (histerektomia) ni lazima.