Homa ya Q

NaWilliam A. Petri, Jr, MD, PhD, University of Virginia School of Medicine
Imekaguliwa naBrenda L. Tesini, MD, University of Rochester School of Medicine and Dentistry
Imepitiwa/Imerekebishwa Imebadilishwa Jan 2024
v27409992_sw

Homa ya Q inahusiana na magonjwa ya rickettsial na husababishwa na Coxiella burnetii, ambao wanaishi zaidi katika kondoo, ng'ombe na mbuzi.

  • Baadhi ya watu wana dalili nyepesi, lakini wengi wana dalili kama za mafua, kama vile homa, maumivu makali ya kichwa, kibaridi, kikohozi kikavu, udhaifu mkubwa na maumivu ya misuli.

  • Watu wachache hupata homa sugu ya Q, ugonjwa mbaya ambao unaweza kuathiri moyo.

  • Ikiwa watu wanaweza kuwa wamekaribia kondoo, ng'ombe au mbuzi na madaktari wanashuku homa ya Q, wanaweza kufanya vipimo vya damu na kuchunguza sampuli ya tishu zilizoambukizwa ili kuthibitisha maambukizi.

  • Watu wenye homa ya Q hutibiwa kwa dawa ya kiuavijasumu, kwa kawaida kwa wiki chache, lakini ikiwa homa sugu ya Q itatokea, matibabu inahitajika kwa miezi au miaka.

Bakteria zinazosababisha homa ya Q, kama vile rickettsiae, inaweza kuishi ndani ya seli za viumbe vingine pekee.

Homa ya Q hutokea duniani kote. Bakteria wanaosababisha homa ya Q huishi hasa katika kondoo, ng'ombe na mbuzi. Wanyama walioambukizwa (ambao mara nyingi hawaonyeshi dalili) humwaga bakteria kwenye maziwa, mkojo na kinyesi chao. Watu huambukizwa wanapovuta matone yanayopeperushwa hewani yenye bakteria au wanapokunywa maziwa mabichi yaliyochafuliwa (yasiyosafishwa). Matone yanayotoka hewani yenye bakteria yanaweza kusafiri umbali mrefu na kuathiri watu wanaoishi karibu na shamba la mbuzi au kondoo walioambukizwa. Mara chache sana, ugonjwa huenezwa kutoka kwa mtu mmoja hadi mwingine.

Watu walio katika hatari ya kupata homa ya Q ni pamoja na wafuatao:

  • Madaktari wa mifugo

  • Wafanyakazi wa kiwanda cha kusindika nyama

  • Wafanyakazi wa machinjio na maziwa

  • Wakulima wa mifugo

  • Watafiti katika maabara ambapo kondoo hufugwa

  • Watu wanaoishi ndani ya maili kadhaa chini ya upepo kutoka shamba lenye wanyama walioambukizwa

Bakteria wanaosababisha homa ya Q huishi kwenye vumbi na kinyesi kwa miezi kadhaa. Hata bakteria moja inaweza kusababisha maambukizi. Kwa sababu ya sifa hizi, bakteria hawa huchukuliwa kuwa ajenti anayewezekana wa vita vya kibiolojia.

Dalili za Homa ya Q

Takriban siku 9 hadi 28 baada ya bakteria kuingia mwilini, dalili huanza kwa ghafla. Baadhi ya watu hupaya dalili nyepesi au hawana dalili zozote. Watu wengine hupata dalili kama za mafua.

Dalili za homa ya Q ni pamoja na homa, maumivu makali ya kichwa, kibaridi, udhaifu mkubwa, maumivu ya misuli, kupoteza hamu ya kula, na kutokwa na jasho, lakini hakuna upele. Mapafu mara nyingi huathirika, na kusababisha kikohozi kikavu (kisichotoa makohozi), maumivu ya kifua, na upungufu wa pumzi (unaosababishwa na nimonia). Dalili zinaweza kuwa kali kwa wazee na kwa watu ambao wamedhoofikakutokana na ugonjwa fulani.

Mara kwa mara, ini huhusika. Watu hupata maumivu katika sehemu ya juu kulia ya tumbo na wakati mwingine homa ya nyongo ya manjano.

Wanawake walioambukizwa wakati wa ujauzito wana hatari kubwa ya kuharibika kwa mimba au kujifungua kabla ya wakati.

Ugonjwa wa uchovu baada ya homa ya Q unaweza kutokea kwa hadi 20% ya watu walio na homa ya Q. Watu wanaweza kuwa na uchovu mkali, maumivu ya misuli, maumivu ya kichwa, unyeti kwa mwanga, mabadiliko ya hisia, na ugumu wa kulala.

Homa sugu ya Q ni ugonjwa mbaya unaotokea kwa chini ya 5% ya watu walioambukizwa. Inaweza kutokea kutoka wiki chache hadi miaka mingi baada ya maambukizi ya awali. Hatari ni kubwa zaidi kwa wafuatao:

  • Wanawake wajawazito

  • Watu ambao kinga yao ya mwili imedhoofika kutokana na ugonjwa au dawa

  • Watu wenye ugonjwa wa vali ya moyo

Homa sugu ya Q mara nyingi huhusisha utando wa moyo na vali za moyo (inayoitwa uvimbe wa moyo wa homa ya Q). Wakati mwingine huhusisha mifupa, viungo bandia na ini.

Bila matibabu, ni 1% tu ya watu wenye homa ya Q hufa. Endokadaitisi ya homa ya Q karibu kila mara huwa mbaya lakini kwa matibabu ya viuavijasumu, vifo ni chini ya 5%.

Utambuzi wa Homa ya Q

  • Uchunguzi wa tishu na upimaji wa tishu zilizoambukizwa.

  • Vipimo vya damu

  • Wakati mwingine eksirei ya kifua

Dalili za homa ya Q zinafanana na zile za magonjwa mengine na hivyo haziwasaidii madaktari katika utambuzi. Ikiwa madaktari wanashuku kuwa kuna homa ya Q, huwauliza kama watu walikuwa shambani au karibu na shamba kwa sababu bakteria wanaosababisha homa ya Q huishi hasa katika ng'ombe, kondoo na mbuzi.

Ili kuthibitisha utambuzi, madaktari wanaweza kufanya kipimo cha kuakisi mwanga cha kinga mwili kuangalia kingamwili katika sampuli za damu. Hata hivyo, kufanya kipimo mara moja hakutoshi. Kipimo lazima kirudiwe wiki 3 hadi 6 baadaye ili kuangalia kama kuna ongezeko katika kiwango cha kingamwili. Kwa hivyo, vipimo vya kingamwili kwa kawaida havisaidii kutambua maambukizi mara tu baada ya mtu kuugua lakini vinaweza kusaidia kuthibitisha utambuzi baadaye. Zaidi ya hayo, madaktari hutumia mbinu ya mmenyuko wa polima (PCR) ili kuwawezesha kutambua bakteria kwa haraka zaidi.

Madaktari wanaweza kufanya uchunguzi wa tishu zilizoambukizwa.

Ikiwa watu wana kikohozi au dalili zingine za kupumua, madaktari hupiga eksrei a kifua.

Matibabu ya Homa ya Q

  • Dawa za kuua bakteria

Maambukizi ya awali hutibiwa kwa doxycycline (aina ya dawa ya kiuavijasumu inayoitwa tetracycline), ineyomezwa kwa mdomo. Watu hutumia dawa ya kiuavijasumu hadi watakapopona na kutokuwa na homa kwa takriban siku 5, lakini lazima watumie kwa angalau siku 7. Kwa kawaida, wiki 2 za matibabu zinahitajika. Matibabu marefu yanaweza kuhitajika kwa ugonjwa mbaya.

Ingawa baadhi ya tetracycline zinazotumiwa kwa zaidi ya siku 10 zinaweza kusababisha madoa ya meno kwa watoto walio chini ya umri wa miaka 8, doxycycline inashauriwa kutolewa kwa kipindi kifupi (siku 5 hadi 10) kwa watoto wa rika zote na inaweza kutumika bila kusababisha madoa ya meno au kudhoofisha enameli ya jino (angalia pia Vituo vya Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa (CDC): Utafiti kuhusu doxycycline na madoa ya meno).

Endokadaitisi ya homa ya Q

Ikiwa moyo umeathiriwa, matibabu hutolewa kwa miezi hadi miaka. Kwa kawaida, matibabu hutolewa kwa angalau miezi 18, lakini baadhi ya watu wanahitaji kutibiwa maisha yao yote. Kwa kawaida watu hupewa doxycycline pamoja na hydroxychloroquine. Zote mbili humezwa kwa mdomo. Ili kubaini ni lini matibabu yanaweza kusimamishwa, madaktari humchunguza mtu huyo mara kwa mara na kufanya vipimo vya damu.

Hata hivyo, matibabu ya viuavijasumu mara nyingi huwa na ufanisi wa sehemu tu, na upasuaji mara nyingi unahitajika ili kubadilisha vali za moyo zilizoharibika (angalia mchoro ).

Kinga ya Homa ya Q

Hatua za kuzuia homa ya Q zinahusisha hasa kutumia usafi na upimaji unaofaa (kwa bakteria) katika vituo ambapo kondoo, ng'ombe na mbuzi hufugwa. Kunywa maziwa na bidhaa za maziwa zilizoondolewa vijidudu (hasa bakteria) pekee kunaweza pia kusaidia.

Nchini Australia, chanjo inapatikana na imetumika kuzuia maambukizi kwa watu wanaoweza kuathiriwa (kama vile wafanyakazi wa machinjio na wa maziwa, wakulima wa mifugo, na wafanyakazi wa maabara). Chanjo hii haipatikani nchini Marekani.

Kabla ya kuwapa watu chanjo, madaktari hufanya vipimo vya damu na ngozi ili kubaini kama watu tayari wana kinga dhidi ya homa ya Q. Ikiwa watu tayari wana kinga, kuwachanja kunaweza kusababisha athari kali karibu na eneo la sindano.