Chanjo ya Homa ya Ini

NaMargot L. Savoy, MD, MPH, Lewis Katz School of Medicine at Temple University
Imekaguliwa naEva M. Vivian, PharmD, MS, PhD, University of Wisconsin School of Pharmacy
Imepitiwa/Imerekebishwa Sept 2025 | Imebadilishwa Nov 2025
v16233853_sw

Chanjo ya homa ya ini A husaidia kulinda dhidi ya homa ya ini A, ambayo ni uvimbe wa ini unaosababishwa na virusi vya homa ya ini A.

Matumizi ya chanjo yamepunguza idadi ya watu wanaoambukizwa.

Aina ya Chanjo

Kuna chanjo 2 za homa ya ini A na chanjo 1 ya mchanganyiko wa homa ya ini A na homa ya ini B inayopatikana Marekani.

Chanjo zote za homa ya ini A ni chanjo zisizo hai, kumaanisha zina kipande cha virusi vya homa ya ini A ambacho hakisababishi maambukizi. Kwa sababu kipande hiki cha virusi hakina madhara, hakiwezi kusababisha maambukizi ya homa ya ini A, lakini husababisha mwitikio mkubwa kutoka kwa mfumo wa kingamwili ya mtu (tazama Chanjo hai).

Chanjo mchanganyiko ina homa ya ini A na homa ya ini B.

Kipimo na Mapendekezo ya Chanjo ya homa ya ini A

Chanjo zote za homa ya ini A hudungwa kwenye misuli.

Watu ambao wanapaswa kupokea chanjo hii

Chanjo ya homa ya ini A ni chanjo ya kawaida ya utotoni. Kwa kawaida dozi 1 hutolewa akiwa na umri wa miezi 12 hadi 23 na dozi ya pili hutolewa miezi 6 hadi 18 baadaye. Watu wazima ambao hawajachanjwa wanaweza pia kupokea chanjo hii ya dozi 2. (Tazama Vituo vya Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa [CDC]: Chanjo Zinazopendekezwa kwa Kuzaliwa Hadi Miaka 6, Marekani, 2025 na tazama CDC: Chanjo Zinazopendekezwa kwa Watu Wazima Wenye Umri wa Miaka 19 na Zaidi, Marekani, 2025.)

Watoto wote wanapaswa kupewa chanjo ya homa ya ini A. Baada ya dozi ya kwanza, watu hulindwa kikamilifu kwa miezi 6 hadi 12, na baada ya dozi ya pili, watu hulindwa kwa angalau miaka 14 hadi 20.

Chanjo ya homa ya ini A inapendekezwa kwa watoto wakubwa na vijana ambao hawakuwa wamechanjwa hapo awali.

Chanjo hiyo pia inapendekezwa kwa watu walio katika hatari kubwa ya kupata maambukizi ya homa ya ini A, kama vile:

  • Watu wanaosafiri kwenda au kufanya kazi katika maeneo ambayo maambukizi hufanyika sana

  • Watu ambao kazi yao inawaweka katika hatari ya kuathiriwa (kama vile watu wanaofanya kazi na nyani walioambukizwa virusi vya homa ya ini A au wanaofanya kazi na virusi katika maabara ya utafiti)

  • Watu wanaotumia dawa haramu (za kudungwa au zisizo za kudungwa)

  • Wanaume wanaofanya ngono na wanaume

  • Watu walio na ugonjwa sugu wa ini (kama vile homa ya ini B, homa ya ini C, sirosisi, ugonjwa wa ini wenye mafuta, ugonjwa wa ini unaohusiana na pombe, na homa ya ini ya mfumo wa kingamwili kwenda kinyume na mwili) au viwango vya juu vya vimeng'enya fulani vya ini katika damu yao.

  • Watu ambao hawana makwao

  • Watu walio na maambukizi ya VVU

  • Watu wanaotarajia mwingiliano wa karibu na mtoto aliyeasiliwa kimataifa wakati wa siku 60 za kwanza baada ya mtoto kufika Marekani kutoka kwenye eneo ambalo homa ya ini A inapatikana kwa sana

  • Watu walio katika hatari ya kupata maambukizi ya homa ya ini A wakati wa ujauzito (kama vile watu ambao ni wasafiri wa kimataifa, wanaotumia dawa haramu [zakudungwa sindano au la], ambao wanaweza kuwa katika hatari ya kuambukizwa katika kazini, wanaotarajia mgusano wa karibu wa kibinafsi na mtoto aliyeasiliwa kimataifa, au ambao hawana makazi) au ambao wako katika hatari ya kuugua sana au kufa kutokana na maambukizi ya virusi vya homa ya ini A (kama vile wajawazito ambao wana ugonjwa sugu wa ini au maambukizi ya VVU)

Watu wazima ambao hawajachanjwa ambao wanataka kulindwa kutokana na homa ya ini A wanaweza pia kupata chanjo hiyo, hata bila kuwa na sababu zozote za hatari.

Wakati wa mlipuko wa homa ya ini A, watu wenye umri wa mwaka 1 au zaidi ambao wako katika hatari ya kuambukizwa virusi vya homa ya ini aina ya A wanapaswa kuchanjwa.

Chanjo mchanganyiko inaweza kutumika kwa watu wenye umri wa miaka 18 na zaidi ambao wanahitaji chanjo ya homa ya ini A au homa ya ini B na ambao hawajawahi kuchanjwa na yoyote kati yao. Watu hupewa dozi 3 au 4.

Watu ambao hawapaswi kupokea chanjo hii

Watu ambao wamekuwa na athari mbaya ya mzio yenye kuhatarisha maisha (kama vile athari ya mmenyuko wa anafailaktiki) kwa sehemu yoyote katika chanjo ya homa ya ini A hawapaswi kuipata.

Ikiwa watu wana ugonjwa wa muda mfupi, kwa kawaida madaktari husubiri kutoa chanjo hadi ugonjwa utakapoisha (tazama pia CDC: Nani HATAKIWI Kuchanjwa kwa Chanjo Hizi?).

Athari Mbaya za Chanjo ya Homa ya Ini A

Madhara ya kawaida ni pamoja na maumivu, uwekundu, au uvimbe kwenye eneo la sindano. Baadhi ya watoto wenye umri wa miezi 12 hadi 23 wanaweza kupata homa, na baadhi ya watu wazima wanaweza kupata maumivu ya kichwa.

Kwa maelezo zaidi kuhusu madhara, angalia viambatisho vya kifurushi.

Taarifa Zaidi

Nyenzo zifuatazo za lugha ya Kiingereza zinaweza kuwa muhimu. Tafadhali kumbuka kuwa Mwongozo hauwajibiki kwa maudhui ya nyenzo hizi.

  1. Vituo vya Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa (CDC): Taarifa ya chanjo ya homa ya ini A

  2. Kituo cha Ulaya cha Kuzuia na Kudhibiti Magonjwa (ECDC): Homa ya ini A Chanjo zinazopendekezwa