Bakteremia, sepsisi, sepsisi kali na mshtuko wa sepsisi vinahusiana:
Bakteremia: Kuna bakteria kwenye mtiririko wa damu. Bakteremia inaweza kutokea kutokana na maambukizi makubwa au kutokana na kitu kisicho na madhara kama kupiga mswaki kwa kutumia nguvu nyingi. Mara nyingi, kuna idadi ndogo tu ya bakteria, na huondolewa na mfumo wa kingamwili. Katika hali kama hizo, watu wengi huwa hawaonyeshi dalili. Hata hivyo, wakati mwingine, bakteremia husababisha maambukizi, sepsisi, au zote mbili.
Sepsisi: Bakteremia au maambukizi ya mfumo fulani wa mwili (kama vile maambukizi ya njia ya mkojo au nimonia) huchochea mwitikio mkali wa mwili mzima (sepsisi), ambao kwa kawaida hujumuisha homa, udhaifu, mapigo ya moyo ya haraka, kupumua kwa haraka, na kuongezeka kwa idadi ya seli nyeupe za damu. Mwitikio huo pia huathiri viungo vingi vya ndani, kama figo, moyo na mapafu, ambavyo huanza kushindwa kufanya kazi.
Mshtuko wa sepsisi: Sepsisi inayosababisha shinikizo hatari la chini la damu (mshtuko) inaitwa mshtuko wa sepsisi. Kama matokeo yake, viungo vya ndani kwa kawaida hupokea damu ndogo sana na kusababisha kushindwa kufanya kazi. Mshtuko wa sepsisi ni hatari kwa maisha.